Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninamshukuru Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu, pia kuniwezesha kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Nichukue nafsi hii kipekee kumpongeza Mheshimiwa Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mchango wangu kuiomba Wizara kufuatilia vivutio ambavyo vinaonekana vidogo vidogo, lakini vikiwekewa mazingira mazuri, miundombinu na kuvitangaza, vinaweza kuwavutia watalii kuja kuvitembelea na kuiingizia Serikali pesa nyingi na kuinua uchumi wa Taifa letu. Nasema hivi kwa sababu mfano kule kwetu Kyerwa, tuna vivutio vingi ambavyo vikitangazwa vitaingizia Wizara pesa za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna maji ya moto ya Omokitagata, maji haya watu wanapoyaoga au wanapokanyaga kwenye maji hayo hupokea uponyaji wa magonjwa mbalimbali. Pia tuna Hifadhi ya Rumanyika Orugundu, tuna maporomoko ya Mto Kagera ambavyo ni vivutio, ninaomba Wizara kuvitembelea na vyenyewe viwe kwenye vivutio vya Taifa ili kuongeza wigo mpana wa utalii kuliko kila wakati wanapelekwa maneo yale yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, kwa tatizo lilijitokeza kwenye Hifadhi ya Rumanyika Orugundu, kutokana na chanzo cha maji kilicho kilometa moja ndani ya hifadhi ambacho kilikuwa kinatumiwa na wananchi wa kata ya Bugomora na sehemu ya Kata ya Kibale. Chanzo hiki kimekuwa mkombozi wa wananchi wa kata hizo kuwapatia maji safi na salama, lakini baadae Meneja alivunja kisima hicho kilichojengwa na wafadhili na kuwazuia wananchi kutumia chanzo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumweleza Mheshimiwa Waziri na kuona umuhimu wa kuwapatia wananchi maji safi na salama kwa sababu ndicho chanzo pekee cha kuwapatia maji, Mheshimiwa Waziri aliruhusu wananchi wangu kuendelea kutumia chanzo hicho cha maji, nakushukuru sana kwa kuwajali wananchi wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa muingiliano wa wananchi na hifadhi, naomba Mheshimiwa Waziri kwa sababu wananchi hao hawana chanzo kingine cha kuwapatia maji safi na salama na ili kuendeleza ujirani mwema kati ya wahifadhi na wananchi walio jirani na hifadhi, Wizara ione namna ya kuwasogezea maji ya chanzo hicho karibu na wananchi kwa kutumia chanzo hicho, au kama inawezekana eneo hilo la kilometa moja lirudishwe kwa wananchi kama ilivyokuwa mwanzo, maana chanzo hicho mwanzo kilikuwa kwa wananchi na ndio maana wafadhili waliweza kukijengea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee juu ya hifadhi zetu; hifadhi zetu lazima zitunzwe bila kuingiliwa na kitu chochote. Nchi yetu tunakabiliwa na janga la ukame kwa sababu ya uharibifu wa mazingira, tusipokuwa makini nchi yetu inaelekea kuwa jangwa kwa sababu ya baadhi yetu kutosimama kwenye nafasi zetu tulizopewa kusimamia hifadhi zetu ambazo zilitengwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii wafugaji wanakosa maeneo ya kufugia kwa sababu maeneo yaliyotengwa na Serikali yaliachwa bila usimamizi na yakaingiliwa bila kufuata sheria zilizowekwa, ndiyo maana leo hii tunasema Serikali iruhusu hifadhi zetu ziingizwe mifugo, hili siyo sahihi na halikubaliki. Mfano kwangu Kyerwa mwaka 1987 Serikali ilitenga maeneo ya wafugaji na yakatangazwa kwenye Gazeti la Serikali na kupewa GN 620. Maeneo haya yamevamiwa na kubadilishwa matumizi wafugaji hawana maeneo ya kufugia, tunadai Serikali iruhusu mifugo kuingizwa kwenye mapori ya hifadhi zetu, naiomba Serikali kufuatilia maeneo yote yaliyotengwa ili yarudishwe kwenye matumizi ya mwanzo ndipo tutaondoa mgogoro wa ukosefu wa maeneo ya kufugia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.