Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumpongeza Waziri wa Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Profesa Maghembe pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Engineer Ramo Makani kwa kazi kubwa inayoendelea katika kukuza utalii nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana na kumshukuru Katibu Mkuu, Meja Jenerali Malinzi pamoja na timu yake ya wataalamu kwa kazi nzuri. Nawashukuru kwa tuzo ya uhifadhi wa mazingira ya Jane Goodall kupitia taasisi yake ya Roots & Shoots kwa kushirikiana na Makumbusho ya Taifa. Nawapongeza sana kwa kuendeleza Maporomoko ya Kalambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nikiwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, nilijitahidi kadri ilivyowezekana kuona jambo hilo siku moja linawezekana. Mara nyingi mhamasishaji akiondoka na wazo linakufa, lakini kwa jambo hili imekuwa tofauti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwa kuibua vivutio vingine kama jiwe la Mbuji na Mapango ya Makolo/ Matiri. Kama nilivyochangia wakati wa semina, ipo haja ya kuviibua vivutio vingine na kuvilinda kwani vivutio kama miamba ya hapa Dodoma, mkichelewa mtakuta watu wameshavivunja na kugeuza kokoto, jambo ambalo hamuwezi kurejesha tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuache utani, Southern Circuit inayoacha Ziwa Nyasa mmefikiria nini? Kwa hiyo, Nyasa itakuwa ni Southern of Southern? Lengo langu ni kuwaomba kuwa ikiwezekana basi, ijumuishwe humo na utalii na fukwe ni vema upewe uzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Nyasa tumekubaliana kuanza kidogo kidogo, hivyo kila tarehe 30 Desemba ya kila mwaka ni kilele cha Tamasha la Utalii - Nyasa. Nawashukuru kwa support mliyotupatia mwaka huu. Sasa tuko kwenye maandalizi; na kila mwaka lazima tuseme angalau tumefanya nini. Hivyo tusaidiwe katika kuipanga fukwe hiyo, kuipamba (beautification) na kuboresha utoaji wa huduma hasa kwa akina Mama Lishe na waongoza watalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kutembelea Jimbo langu na kutoa ushauri muhimu kwetu. Miundombinu ya barabara ni tatizo, naomba Wizara yenu kuendelea kutusemea katika vikao vya Wizara mbalimbali ili Mbinga - Mbambabay iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jiwe la Pomonda nalo lipewe uzito (lipo Liuli – mchezo wa kuruka majini) litangazwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nawashukuru sana TFS kwa kazi walioyoanza ya kupata miti Nyasa na naomba kuwasilisha.