Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia dakika hizo tano ulizonipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwamba ili tuweze kuwa na wanafunzi ambao wanafundishika vizuri level zote za elimu, iwe sekondari kwa maana ya kwamba O-level na A-level lakini Vyuo vya Ufundi, Universities ni lazima tuanze na uwekezaji katika elimu, pale tunasema Pre–Primary Education yaani Elimu ya Msingi na Elimu ya Chekechea kabisa kule chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanafunzi yeyote ambaye amefundishwa vizuri, akiwa chekechea, elimu ya awali, mtoto huyu atakuwa na uwezo mzuri wa kuweza kufundishika vizuri atakapokuwa Shule ya Msingi. Akifundishwa vizuri shule ya msingi, atafundishika vizuri sekondari, elimu ya kidato cha nne lakini pia kidato cha tano na kidato cha sita, hata anapofika level ya elimu ya juu, kwa maana ya Chuo Kikuu, atafundishika vizuri na mwisho wa siku tutaweza kuwa na wasomi wazuri katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa sana kwa kuona kwamba sasa hivi katika nchi yetu kuna mkanganyiko wa usimamizi wa elimu. Tuna Wizara ya Elimu, tuna Wizara ya TAMISEMI, mimi nashangaa sana na nazungumza haya nikiwa Mwalimu, lakini pia nikiwa Msimamizi wa Elimu, kwamba tunavyoangalia Wizara ya Elimu, kwamba imepewa kusimamia miongozo, ni jambo la ajabu sana. Tunataka Wizara ya Elimu isimamie elimu, tunataka Wizara ya Elimu isimamie miundombinu ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ninavyozungumza, ukija Mtwara Mjini pale kwa mfano, tuna Shule ya Msingi Mbae, ina madarasa mawili; haina vyoo, lakini ina wanafunzi zaidi ya 630 halafu leo hii tunasema kwamba eti wanafunzi Mtwara na Lindi hawafanyi vizuri katika mitihani yao. Hatufanyi vizuri kwa sababu hatuna miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Mikoa ya Mtwara na Lindi hatufanyi vizuri katika elimu kwa sababu pia Walimu hawatoshi. Shule za Msingi, Shule za Sekondari hatuna Walimu wa kutosha. Tunaomba Wizara itusaidie hili. Mkoa mzima wa Mtwara tuna upungufu wa Walimu, hawatoshi, watuletee Walimu tuweze kufanya vizuri kama ilivyo katika mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa dakika zangu ni chache, naomba nizungumze suala hili ambalo Serikali ya Awamu ya Nne ililianzisha. Mimi nilikuwa Msimamizi wa elimu wakati huo, nilikuwa Mkuu wa Shule, Mchinga Sekondari kwa miaka mitano. Tulipewa miongozo ya kusimamia elimu kupitia BRN, lakini tangu mwaka 2016 hatuoni kuna nini? Kwa nini huu mpango unaoitwa BRN (Big Result Now) ambao Serikali iliiga kutoka nchi ya Malaysia. Ule mpango ulikuwa ni mzuri kwa sababu ule mpango ulikuwa unaleta usimamizi katika elimu kwamba Mwalimu anapofanya vizuri, anapofundisha vizuri, mwisho wa siku anakuja kupewa motivation kupitia Wizara ya Elimu na TAMISEMI, lakini sasa hivi BRN haitajwi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwamba kama kweli tunahitaji matokeo mazuri katika elimu, turudishe huu mpango wa BRN katika elimu, ulikuwa unasaidia sana kuchochea Walimu kuweza kufanya kazi, Walimu kuweza kufundisha kwa sababu walikuwa wanapewa motisha pale ambapo wanafaulisha vizuri masomo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la kuboresha elimu linaendana sambamba na kuboresha maabara. Kulikuwa na mpango wa kujenga maabara, nami kipindi kile nikiwa Mkuu wa Shule, tuliweza kujenga maabara nyingi sana, lakini mpaka leo tunavyozungumza zile maabara hazina vifaa, hazina kemikali, hazina Walimu wa sayansi ambao watakuja kufundisha yale masomo ya sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama kweli tunahitaji kuipeleka elimu yetu mbele, lazima Wizara ya Elimu iliangalie suala hili la maabara tupeleke kemikali mashuleni. Jambo la umuhimu zaidi ni usimamizi wa elimu kwa Wakuu wa Shule. Wakuu wa Shule ndiyo nyenzo pekee ambapo tukiwatumia ipasavyo, hawa Walimu wanaweza kusimamia elimu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu wa elimu bure hivi sasa hasa katika Shule za Mikoa ya Lindi na Mtwara, hakuna michango inayokusanywa, hakuna pesa za ulinzi wala taaluma na hizi shule maeneo mengi ziko vijijini, ziko maeneo ya vijiji na Halmashauri zenyewe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.