Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na hatimaye kuweza kusimama leo hii katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwape pole wazazi wote waliopoteza watoto wao katika ajali mbaya ya gari la shule iliyohusu shule ya Lucky Vincent, Mkoani Arusha. Niwape pole sana na Mwenyezi Mungu awajalie ili waweze kuendelea na mambo mengine na wale watoto pia waliokwenda jana kupata matibabu nje, Mwenyezi Mungu awajalie wapone na warudi kuendelea na masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nitoe pongezi za dhati kwa sababu amechangia kwa kiasi kikubwa watoto wenye ulemavu na hasa wazazi lakini walezi kuhakikisha kwamba wanawapeleka watoto wao shule ili waweze kwenda kupata elimu. Miongoni mwa watu ambao walikuwa ni waathirika wakubwa katika suala zima la elimu ni watoto wenye ulemavu ambao kutokana na mila, desturi na tamaduni zetu wazazi kwa mitazamo tu hasi waliwaacha na kuwafungia nyumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa ujio wa Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, kuleta elimu bure hata wazazi wenyewe wameona kwamba ni wakati muafaka wa kuwapeleka watoto wao shule. Kwa hiyo, nampongeza sana na niseme tu kwamba kwetu sisi tunaona Mheshimiwa Rais Magufuli ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru pia Waziri pamoja na Naibu wake na hawa ni akinamama. Wanasema siku zote uchungu wa mwana aujuaye mzazi. Niwapongeze sana lakini pamoja na pongezi hizo na pongezi za ujumla kwa Serikali vilevile basi nizungumzie changamoto zilizopo katika suala zima la elimu na hasa kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu pamoja na kwamba hivi sasa shule nyingi watoto wamejitokeza na kwenda kupata elimu lakini nikianza na suala zima la miundombinu pamoja na kwamba Serikali imetoa vifaa, pongezi sana kwa hilo Mama Mheshimiwa Profesa Ndalichako lakini bado miundombinu ni tatizo na ni kikwazo kwa watoto wenye ulemavu kuweza kupata elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapozungumzia miundombinu ni kwa ujumla kuanzia madarasa lakini pia umbali na tatizo lingine kubwa zaidi ni vyoo. Pamoja na jitihada ambazo mmezionesha mnakwenda kujenga vyoo katika shule za msingi na shule za sekondari watoto wenye ulemavu wanapata shida sana wanapokuwa shuleni kwa sababu miundombinu ya vyoo inawafanya wasiweze kufika katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika vyoo vingi ambavyo vinatumiwa na wanafunzi wote kwa ujumla na hasa ukiangalia tundu moja wakati mwingine linatumika mpaka na watoto 25-30 kwa huyu mtoto mwenye ulemavu, mfano tu mtoto mwenye ulemavu anayetambaa, niambie mazingira yale anafikaje chooni? Inakuwa ni vigumu sana. Kwa hili, niwaombe tulete sheria kwamba kila shule ni lazima kuwepo na vyoo ambavyo vitawawezesha watoto wenye ulemavu kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, nalishukuru sana Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nimshukuru Katibu pamoja na Spika kwa sababu wanaelewa kwamba Bunge hili limetujumlisha wote lakini pia miundombinu ni rafiki inayotuwezesha kwenda katika maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri na kwa sababu watu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania na wao wanakarabati hizi shule muwape mwongozo kuhakikisha kwamba katika kila shule wanayokwenda kukarabati wahakikishe vyoo viwili vinakuwepo kwa ajili ya watoto wenye ulemavu na Walimu Wakuu waweke utaratibu maalum ambao utawezesha hawa watoto peke yao wenye ulemavu kwenda katika vile vyoo na wasiweze kuingia hao wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ni kweli kwamba Serikali imetoa vifaa kwa ajili ya watoto wenye ulemavu lakini kwa walimu bado ni tatizo. Ni tatizo kwa sababu gani? Kwa mujibu wa mwongozo wa huduma kwa watumishi wa umma wenye ulemavu ambao unasema nyenzo na vifaa vya kuongezea uwezo wenye ulemavu Wizara, Idara, Wakala wa Serikali na Mamlaka za Serikali za Mitaa zihakikishe kwamba watumishi wenye ulemavu wanapata huduma zitakazowasaidia kutekeleza majukumu yao kikamilifu kama vile nyenzo na vifaa ili kuwasaidia kuongeza kiwango chao cha kujitegemea katika maisha yao ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwongozo huu unawataka waajiri na siyo kwa Wizara ya Elimu peke yake ni waajiri wote kwa ujumla na bahati nzuri yupo hapa Mwenyekiti wa Waajiri hili pia alibebe na kusisitiza waajiri wote wanaowaajiri watu wenye ulemavu wanahakikisha ni kwa namna gani watu wenye ulemavu wanaweza kufika katika sehemu zao za kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sababu nachangia Wizara ya Elimu, hawa Walimu wana changamoto nyingi, hawana nyenzo muhimu ambazo zinawawezesha wao kuweza kufanya kazi zao kwa ukamilifu. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuoimba na kuishauri pia Serikali kuhakikisha kwamba inawawezesha Walimu hawa.

Ukiangalia katika Wizara ya Elimu hawa Walimu wenye mahitaji maalum wengi ndiyo wanaopata ajira kwa wingi huku, kwa hiyo, tuhakikishe tunawawekea miundombinu pamoja na kuwapa nyenzo ili waweze kufanya kazi zao pasipo usumbufu. Vilevile kuhakikisha wanawekwa maeneo ya karibu ili basi wasipate shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni kwamba kumekuwepo na utaratibu ambapo Serikali inaratibu wanafunzi wenye ulemavu wanaosoma katika shule tofauti, tofauti, mfano, shule ya Buigiri na Furaha kule Tabora na nyinginezo. Wanafunzi wenye ulemavu ambao wanakwenda kusoma kwenye shule hizo kwa sababu ya mila, tamaduni, desturi na mitazamo, wazazi wengi wanaona kwa nini ampeleke mtoto lakini sasa hivi wanakwenda na Serikali ikaweka utaratibu kwamba hawa wanafunzi wakati wa likizo inawasafirisha kuwarudisha nyumbani lakini mwaka jana mmefuta huu utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, Mama yangu anapofuta huu utaratibu hawa watoto wanabaki kule shuleni mwaka mzima. Kwa mzazi mwenye mtoto mwenye ulemavu mfano shule iliyopo Shinyanga ambayo sasa hivi imekuwa kama ni kituo wengi wamekwenda kuwatupa pale watoto hawarudi hata nyumbani. Sasa ule utaratibu wakiondoa kwamba hawawachukui tena kuwarudisha nyumbani yaani pale ndiyo inakuwa nyumbani kwao na kama mnavyojua tukasome lakini pia turudi nyumbani ili kujumuika na wazazi wetu. Wakituacha maeneo ya shule wasipoturudisha nyumbani ni sawa na wametutupa kwa maana kwamba sisi tunakuwa sasa ni watoto wa pale pale mpaka tumalize shule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, yeye ni mama na siku zote mama ndiyo mwenye uchungu, apigane hawa watoto warudi nyumbani kwao, kuwepo na usafiri utakaowapeleka na kuwarudisha nyumbani. Ndiyo wamewaandalia mazingira lakini pia wakiwaacha kule miaka yote inakuwa ni kama vile adhabu au ukizaliwa mtu mwenye ulemavu basi inakuwa ni kama vile ndio mkosi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunasimama hapa na kutoa michango ni kwa sababu jamii ilituwekea mazingira mazuri, wazazi wetu walikuwa wanajua umuhimu huo na ndiyo maana wakatusomesha na leo hii tuko hapa. Sasa tusipowaandalia mazingira mazuri tutawapata wapi akina Amina na Ikupa wengine.