Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma anaye rehemu, muumba mbingu na ardhi na vilivyomo. Aidha, nakushukuru wewe Mheshimiwa Mwenyekiti kwa uongozi wako madhubuti hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ina majina mengi iliyopewa kwa sababu ya utukufu na ubora wake na kwamba aliye nayo huambiwa kaelimika. Elimu ni ufunguo wa maisha, elimu ni maisha na majina mengi mengineyo kuhusu elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la msingi, elimu hasa ni ile inayomkomboa mtu katika kusimamia majukumu yake na ya Kitaifa. Taifa lolote duniani haliwezi kuendelea bila ya mfumo mzuri wa elimu na mfumo bora wa elimu duniani ni ule unaozingatia mambo muhimu kama yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu imsaidie mlengwa mwenyewe na Taifa lake kwa ujumla wake. Pia elimu imuwezeshe msomi huyu kuweza kujitegemea na aondokane na kuwa tegemezi. Pia imsadie kuijua dunia yake anayoishi hususan katika dunia hii ya utandawazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa kwetu Tanzania mfumo wetu wa elimu ni tofauti kidogo na matakwa ya mfumo bora wa elimu. Katiba yetu inataja kwamba kupata elimu ni haki ya kila Mtanzania ya msingi kabisa, lakini elimu inayotolewa hapa haikidhi haja na matakwa ya mfumo bora wa elimu. Mfumo na mitaala yetu haijengi katika kutoa elimu bora (quality education) yaani ya muhitimu kuweza kujitegemea kutokana na elimu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uboreshaji wa mfumo mzuri wa elimu ni pamoja na kuongezea bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kukidhi haja zote za elimu. India ni nchi inayoendelea kama Tanzania lakini bajeti yao katika elimu ni zaidi ya asilimia kumi, jambo ambalo limeifanya India kufanikiwa na kuwa miongoni mwa nchi bora duniani kwa kuzalisha na kuuza wataalamu mabingwa nchi zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii yote ni kutokana na uwekezaji mzuri juu ya elimu nchini India. Takwimu zinaonesha katika kampuni kubwa mashuhuri sana duniani iliyoko Marekani ya Microsoft ya tajiri mkubwa duniani, Bill Gates ina wafanyakazi zaidi ya asilimia kumi kutoka India, madaktari bingwa wengi walioko Marekani ni Wahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuiga jambo zuri si dhambi, wenzetu wamefanikiwa baada ya kuona umuhimu wa kuiongezea na kuikuza Wizara ya Elimu, hivyo naishauri Serikali itenge na kutoa pesa za kutosha kwa elimu ya ngazi zote, vyuo vya ufundi, kilimo na nyanja zote na sisi tuzalishe na kuuza wataalamu nchi za nje badala ya kuuza watumishi wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu yetu inayotolewa zaidi inapelekea kuongeza idadi ya wahitimu katika kila ngazi. Kwa mfano, idadi ya wahitimu wanaomaliza shule za msingi, sekondari, vyuo vikuu inaongezeka kila mwaka. Lakini idadi yote hii inayoongezeka kila mwaka ni tegemezi, hawana uwezo wa kujiajiri wenyewe, idadi kubwa ni lazima wapewe ajira Serikalini vinginevyo wahitimu hawa ndio hubakia wakizagaa tu mitaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi kwa Serikali, hatujachelewa bado, Serikali itilie maanani suala la mfumo bora wa elimu ili elimu itolewayo iwe ya manufaa zaidi ili utegemezi juu ya ajira kutoka Serikalini ipungue sana. Ikiwa Serikali itaboresha Vyuo vya Ufundi (VETA) na huduma kamilifu, ni imani yangu kwamba wahitimu wetu wataweza kujiajiri wenyewe na kuondoa mrundikano wa wahitimu wanaosubiri kupata ajira.