Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niunge mkono hoja ya Wizara ya Elimu. Pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kufanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa sekondari. Tuna tatizo kubwa sana kwani maeneo mengi yana upungufu wa majengo ya shule za sekondari. Pamoja na juhudi kubwa inayofanywa na wananchi kwa kujitolea asilimia 20 bado Halmashauri zinashindwa kuwasaidia kumalizia majengo ya shule. Niiombe Wizara iangalie uwezekano wa kusaidia kuboresha majengo na kujenga shule mpya pale ambapo ni stahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwenye Wilaya mpya ya Tanganyika tupatiwe msaada wa fedha za kumalizia shule za sekondari za Tongwe, Bulamata sekondari, Ilangu sekondari na Mazwe sekondari. Shule hizi zinahitaji msaada wa Serikali wa kuzifanyia ukarabati na kuongeza madarasa na nyumba za walimu na kujenga maabara pamoja na vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa na matatizo ya uchakavu wa majengo na ukosefu wa vyumba vya madarasa kwenye shule zetu za msingi, bado tuna tatizo kubwa la ukosefu wa walimu. Tunaomba Serikali iangalie umuhimu wa kuongeza walimu wa kufundisha kwenye mashule hizi hii ikiwa ni pamoja na kuongeza marupurupu ya walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu madai ya walimu, kuna malalamiko makubwa ya walimu kuidai Serikali stahili zao ikiwemo kutopandishwa vyeo, kutolipwa posho zao za likizo, nauli na posho za madaraka. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aje na majibu ya uhakika juu ya suala zima la madai ya walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyuo vingi vya ufundi vina hali mbaya sana kwa kukosa vitendea kazi hasa vya kufundishia jambo ambalo linasababisha vishindwe kukidhi malengo ya kuanzishwa vyuo hivi. Niombe Serikali iboreshe Chuo cha VETA Mpanda kwani hakina vitendea kazi pamoja na walimu. Chuo hiki kinategemewa sana na wananchi wa Mkoa wa Katavi. Naomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.