Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka 2016/2017. Kumekuwa na ongezeko la watoto walioandikishwa kuanza shule, Serikali imebeba gharama kubwa za kumsomesha mtoto na kushirikiana na wazazi na walezi wa wanafunzi hawa kupitia programu ya elimu bila malipo. Bado changamoto zilizopo za upungufu wa madarasa kwa shule zote za sekondari na shule za msingi, upungufu wa nyumba za walimu kwa shule zote hizi za sekondari na shule za msingi,

Pia upungufu mkubwa wa matundu ya choo kwenye shule hizi za sekondari hasa zaidi kwenye shule za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia upungufu wa walimu kwenye baadhi ya shule za sekondari na shule za msingi na upungufu wa vitabu vya kufundishia na vitabu vya wanafunzi haya ni mambo muhimu ambayo Serikali inayashughulikia kwa nguvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limetokeza suala la watoto wa kike kupewa mimba mashuleni. Serikali inapaswa kuendelea kulikataza na kulisimamia suala hili kwa kuhakikisha wanaume wanaokatisha masomo ya wanafunzi hao wa kike kwa kuwapa mimba wanaadhibiwa kwa mujibu wa sheria za nchi. Pia ni muhimu kwa Serikali na hususan Halmashauri za Mikoa na Wilaya kuhakikisha zinajenga hostel za kutosha kwa ajili ya wanafunzi wote wa kike na kuwakinga wanafunzi hao. Hostel hizi zitapunguza sana tatizo lililopo la wanafunzi wasichana kupata mimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu la Morogoro Kusini kuna shule nyingi za sekondari ambazo zimejengwa kwa nguvu kubwa za wananchi lakini zina changamoto hizi za mimba. Tunaomba Wizara itoe fedha za kutosha kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro Vijijini ili tuondoe tatizo hili la aibu la wanafunzi wa kike kupewa mimba mashuleni. Mazingira ya wanafunzi hawa ni mabaya sana na yanasababisha kupata mimba hizo. Tukiwezeshwa kujenga hostel za wanafunzi wa kike kwenye shule hizi, tutaondoa tatizo lililopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jimbo langu la Mororogo Kusini tunalo eneo tayari la kuanzisha shule za VETA. Bado naikumbusha Serikali iweze kutupa msaada tuweze kuanzisha chuo hicho kwa kipindi kijacho cha mwaka 2017/2018 - 2018/ 2019. Sambamba na hilo jimbo la Mororogoro Kusini imeziteua shule za sekondari Matombo na shule ya sekondari Misewesewe ya wasichana iliyopo kata ya Mngazi kuanzisha kidato cha tano (form five) kuanzia mwaka 2017/2018. Matayarisho yamekamilika kwa shule hizi hususan shule ya sekondari ya Matombo ili ianze kupokea wanafunzi wanaoingia kidato cha tano kuanzia mwaka ujao wa fedha wa 2017/2018. Nimepata taarifa kwamba kumekuwa na ucheleweshaji wa kuwezesha mpango huu kutokana na urasimu Wizarani. Naomba Wizara ihakikishe tunalikamilisha mapema ili wanafunzi waweze kupata elimu ya form five ndani ya Wilaya ya Morogoro Vijijini kupitia shule zetu hizo mbili zilizoteuliwa ambazo kwa kiasi kikubwa zimecheleweshwa kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.