Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema, pia nitumie nafasi hii kukushukuru na kukupongeza wewe binafsi, Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na viongozi wote wa Bunge kwa ujumla kwa jinsi ambavyo mnaliongoza Bunge letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza na kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kusimamia vizuri Serikali kwa niaba ya wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mwaka 2016/ 2017 sikufanikiwa kuchangia bajeti kutokana na kifo cha mama yangu mzazi, hivyo basi naomba nitumie fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kuniteua katika nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile namshukuru Makamu wetu wa Rais, Rais wa Zanzibar pamoja na Waziri wetu Mkuu kwa jinsi ambavyo wananiongoza na kunipa maelekezo na ushauri mbalimbali katika kutimiza wajibu wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa namshukuru sana Waziri wangu Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako kwa ushauri na mwongozo wake kwangu, ambao umekuwa ukiniongezea ufanisi katika utendaji wangu wa kila siku. Nimekuwa nikijipambanua siku zote kama silaha ya msaada kumbe yeye ni rada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niwashukuru watumishi wote wa Wizara na Taasisi zake chini ya uongozi wa Dkt. Leonard Akwilapo, Naibu Makatibu Wakuu Profesa Simon Msanjila na Dkt. Avemaria Semakafu kwa ushirikiano wanaonipa na kutekeleza majukumu yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naishukuru familia yangu na vilevile nimkumbuke mama yangu mzazi kipenzi Bi Xavelia Mbele pamoja na Marehemu wote waliotangulia wakiwemo wale watoto wa Arusha, ndugu na marafiki wote tunawaombea wapumzike kwa amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea nawaona wapiga kura wangu wa Jimbo la Nyasa wakitabasamu mioyoni mwao kuwa walinichagua Mbunge sahihi, mimi ni mtumishi wao, kwani wao ni bora zaidi, nawapenda sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijibu hoja za Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo, na hivyo naanza kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianzia na DIT suala la kupeleka wakaguzi maalum kutokana na kuchelewa kwa ujenzi, lakini pia matumizi makubwa ya fedha. Kimsingi tayari barua ilishaandikwa kwa Mkaguzi Mkuu wa Ndani yenye Kumbukumbu Na. PL/AC.19/119/01 ili afanye ukaguzi maalum wa mradi huo. Taarifa itakapokamilika itawasilishwa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii. Vilevile napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa mradi huo sasa umeendelea vizuri na umefikia asilimia 95.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia na hoja ya kutaka kufahamu sifa za kujiunga na Taasisi ya Teknolojia - DIT. Kimsingi hapa nitatamka tu sifa za msingi, lakini ni vyema mkawasiliana na chuo au kupitia tovuti yao kuweza kupata taarifa kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kuna ngazi mbili, ngazi ya kwanza ni ya diploma ya kawaida ambayo muombaji anatakiwa awe na sifa za kidato cha nne na awe amefaulu angalau pass nne kuanzia ā€œCā€ na vilevile kwa upande wa degree awe na diploma ya kawaida na GPA ya tatu au awe na cheti cha kidato cha sita na awe ana point angalau nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na dhana kutoka miongoni mwetu ambayo kupitia michango nimeweza kufahamu kwamba kuna hisia kwamba vyuo vya ufundi sasa hivi vimepungukiwa na viwango tofauti na ilivyokuwa awali. Nipende tu kuwajulisha Waheshimiwa Wabunge kwamba hali ya sasa ni kwamba vyuo hivyo vimeboreshwa zaidi kwa kuweka ngazi mbalimbali zinazowezesha unyumbufu katika utoaji kozi hizo. Kwa hali ya mwanzo ilikuwa ni kama unasoma kwa mfano kozi ya ufundi sanifu ilikuwa ni lazima uhakikishe unamaliza kozi nzima na ukikatisha ulikuwa hupati cheti kabisa. Sasa hivi mfumo unakuwezesha kusoma hatua kwa hatua na kila ngazi unayoifikia unapata cheti ambacho kinakuwezesha kufanya kazi zako na pia kuweza kurudi pale inapohitajika kurudi chuoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la VETA, hilo limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi sana juu ya mahitaji ya VETA. Tatizo kubwa ni upatikanaji wa fedha. Niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge, kwa wale ambao maeneo yao yana majengo na yana ardhi za kuweza kutupa ili kuendeleza tunaomba basi mkamilishe upatikanaji wa hati, ili maeneo hayo yanapoletwa kwetu yasiwe na mgongano. Kwa misingi hiyo napenda kuwapongeza Wabunge ambao wameisha chukua hatua kama hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mbunge wa Busokelo ambaye alifuatilia na akafuatilia hati kwa Mheshimiwa Mwandosya na hivi sasa chuo cha VETA kimeishakamilishwa na wanafunzi wanasoma. Lakini pia nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wanajituma katika kuchangia katika suala la elimu, wapo wengi. Nafahamu kuna ambao wamechangia uboreshaji wa shule kama Loleza, Mheshimiwa Mbene kwenye eneo lako na wengine wengi naomba tuendelee kushikamana katika hali hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira ya Serikali ni kuendelea kuwa na VETA katika kila Wilaya, lakini kwa sasa tutazingatia kuimarisha VETA zilizopo kwa kuziongezea mabweni, walimu pamoja na vifaa vya kufundishia na kujifunzia, lakini vilevile kuhakikisha kuwa tunaimarisha vyuo vingine kama FDC ili viweze kuchukua wanafunzi na kukidhi mahitaji yanayoendana na hali ya sasa. Kwa upande wa FDC ni kwamba FDC nyingi yaani vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vinaonekana kuwa na hali mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshafanya mkutano tayari na wakufunzi wa vyuo hivyo, tuna vyuo jumla 55, na mwaka huu tumeshatenga shilingi bilioni 12 kwa ajili ya kuanza ukarabati katika vyuo hivyo, lakini pia kufuatilia mitaala itakayowezesha kufanya kozi zitakazosaidia wananchi kwa ujumla kwa mahitaji ya soko hasa katika kwenda katika uchumi wa viwanda, vilevile kuzingatia makundi mbalimbali ikiwemo watoto wa kike ambao hawakupata fursa ya kuendelea na masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa COSTECH. COSTECH imekuwa ikiendelea kutengewa fedha, kwa mfano kwa mwaka huu 2016 ilipata shilingi bilioni 45.26 katika fedha hizo kuna ambazo zimetekeleza miradi ya upande wa pili wa nchi (Zanzibar). Kwa mfano SUZA katika mradi wa vifaranga vya kaa, Taasisi ya Utafiti wa Kilimo cha Mpunga na Viazi Kizimbani, Mwani kwenye Institute of Marine Sciences. Pia kwa upande wa Bara kuna taasisi kama TIRDO na nyingine nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Serikali itaendelea kutenga fedha na kuhakikisha kuwa mfuko huo wa COSTECH unatumika vizuri, ambao tunaita MTUSATE na kuweza kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuleta matokeo ambayo yanatarajiwa hasa katika kuongeza thamani ya mazao yetu pamoja na fursa tulizonazo nchini. Vilevile tumeendelea kuongeza nguvu na jitihada katika kituo chetu cha TEHAMA na kiatamizi ambacho kinahusika na masuala ya kuibua vipaji mbalimbali vya vijana wetu ambavyo viko pale katika Ofisi za COSTECH - Kijitonyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la walimu wa masuala ya sayansi. Nipende tu kukufahamisha kwamba ni kweli tuna upungufu katika eneo hilo, lakini hata hivyo Serikali imeisha jitahidi kwa mwaka huu, imeweza kuajiri walimu wa sayansi na hisabati 4,129 na baada ya uhakiki wa vyeti vya walimu 3,081 basi ajira hizo zitaendelea tena. Nipende tu kusema kwamba Serikali imekuwa ikiendelea na jitihada hizo ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wetu wanapata elimu inayostahili kwa kupewa walimu wenye sifa pamoja na vifaa vya kufundishia na kujifunzia kama vifaa vya maabara.

Vilevile kwa upande wa mafundi sanifu wa maabara Serikali kwa kushirikiana na vyuo vya ualimu kwa kushirikiana na TCU na NACTE wataandaa mitaala na kuanza mafunzo kwa ajili ya kuongeza wataalam wa maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala linalohusu ya tatizo la ujinga katika nchi yetu. Kama ambavyo nimejibu swali la msingi namba152 la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga tarehe 5 Mei, 2017, ni kweli tuna watu wasiojua kusoma na kuandika yaani vijana na watu wazima asilimia 22.4 kwa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012. Zipo jitihada mbalimbali za kuhakikisha kwamba tunapunguza tatizo hilo kupitia MUKEJA, lakini pia kupitia Mpango wa Ndiyo Ninaweza, kuimarisha stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu na vilevile kuhakikisha kwamba wanafunzi wote wanaotakiwa kuanza shule wanakwenda shule ili kupunguza ongezeko la watu hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba watoto wote wanaotakiwa kwenda shule wanakwenda kuanzia elimu ya awali na hivi tumeanzisha hata shule shikizi pamoja na kuongeza idadi ya walimu wa elimu ya awali na hivyo kuwezesha kupata wanafunzi wengi zaidi katika eneo hilo. Tunatarajia ifikapo mwaka 2022 wakati wa sensa ijayo Taifa letu liwe limepunguza ujinga na kufikia angalau asilimia si zaidi ya 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie juu ya lugha ya alama. Tayari Wizara imeshaanza jitihada za kutengeneza vitabu kwa ajili ya kufundisha lugha ya alama. Tunategemea hali hiyo itawezesha wanafunzi na wazazi wao kupata mawasiliano ya kirahisi lakini pia hata sisi wenyewe kuifahama lugha hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kuna jambo ambalo limejitokeza leo na katika siku hizi za karibuni, niombe kuungana na Mheshimiwa Waziri wangu kwa masikitiko makubwa juu ya mapungufu yaliyojitokeza katika uchapishaji wa vitabu. Hivyo tunawaomba radhi kwa niaba ya wananchi kwa mapungufu hayo. Hata hivyo Mheshimiwa Waziri wangu atalizungumzia suala hili kwa kina zaidi. Nomba radhi kwa niaba ya Wizara yangu.

Mheshimiwa Mwenyekit, baada ya maneno haya nizidi tu kusema kwamba tumedhamiria kama Wizara kuona kwamba elimu inaendelea kutolewa ikiwa bora na kila aina ya tatizo tutajitahidi kadri inavyowezekana kulifanyia kazi na kuhakikisha kuwa wananchi wa Tanzania wanapata fursa ya kusoma vizuri na kupata ajira katika soko linaloendana na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba kuunga hoja tena.