Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mimi ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo (HUSM). Ahsante sana kwa nafasi hii uliyonipa. Nianze kwa kumpongeza sana Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo imegusa kila kona, bahati mbaya imekuwa dozi kubwa imewafanya wenzetu wapate kiwewe na kukimbia humu ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Waziri Mkuu na michango ya Waheshimiwa Wabunge kuna hoja zimeguswa. Baadhi ya hoja tutazishughulikia kwenye bajeti ya Wizara tutakapoileta, lakini nimesimama nishughulike na hoja moja ambayo kwa kweli inapotoshwa sana. Ni vizuri tukaweka kumbukumbu na rekodi sawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kurusha Bunge moja kwa moja; la kwanza, yanazungumzwa mengi lakini kuna mambo hayasemwi. Jambo la kwanza, mpango wa kuanzisha Studio ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ulipitishwa na Bunge hili na pesa zake zikatengwa. Hili jambo wenzetu hawataki kuwaambia Watanzania! Wanasema ni mpango ambao umebuniwa, unapitishwa kinyemela kwa lengo la kutaka kuwanyima Watanzania kuona Bunge lao. Huu ni uongo, tena uongo wa mchana peupe, kwa sababu mpango huo ulipitishwa hapa, Mheshimiwa Freeman Mbowe na wenzake walikuwepo na mpango huu waliupitisha. Hili la kwanza, ni vizuri tukaweka rekodi sawasawa.
Mheshimwa Mwenyekiti, la pili, kunasemwa hapa kama vile Bunge hili limezuiwa lisionekane kabisa, kwamba pana total blackout ya kuoneshwa Bunge hili. Nadhani either ni kutoelewa, uelewa mdogo au wanafanya makusudi baada ya kukosa hoja za msingi za kuja kuzijadili hapa, sasa wanaanza vioja ili ionekane liko tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichofanyika, pengine nitafute lugha rahisi wenzetu watuelewe; utaratibu umebadilishwa wa kulionesha Bunge letu, kama ambavyo utaratibu mwingine wowote unaweza ukabadilishwa. Dar es Salaam pale, barabara ya Samora ilikuwa ni barabara inapitisha gari kwenda na kurudi. Kwa sababu ya tatizo la foleni, ule utaratibu ukabadilishwa. Sasa utaratibu ukibadilishwa, anakuja mtu anazira kwenda barabarani kwa sababu utaratibu umebadilishwa kupunguza foleni. Nadhani hapa pana shida ya kuelewa au pana makusudi au pana kushindwa kazi kwa sababu ya kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupitisha mpango wa kuanzisha Studio ya Bunge utaratibu wa kurusha Bunge hili ukabadilishwa na umebadilishwa kwa makusudi yafuatayo:-
Moja; Bunge hili wakati linarushwa mchana, wananchi waliokuwa wanapata fursa ya kuliona Bunge letu, idadi yake ukilinganisha na idadi ya watakaoliona Bunge usiku, kwa takwimu, siyo kwa maneno ya kelele, kwa takwimu, idadi yake inaongezeka. Maana yake ni nini? Maana yake tunatoa fursa kwa Watanzania wengi zaidi kuliona Bunge, kushuhudia kazi za Bunge kuliko ilivyokuwa inatokea mwanzo. Kwa watu ambao wamezoea kupiga kelele, wala hili siyo tatizo, jambo jema, Watanzania wametuelewa na tunasonga mbele bila matatizo. (Makofi/ Kelele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ambalo hawasemi, Waziri wa Habari, tena Waziri wako, hawasemi na hii ni tabia yao; nami naomba Watanzania wawasamehe na wala sina mashaka, Jumatano watarudi hapa tutaendelea na mjadala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nalo ni kubwa Watanzania hawaambiwi, utaratibu wa kuweka Studio hapa Bungeni unarahisisha urushaji wa matangazo ya Bunge bila kulazimisha Vituo vya Habari vya Utangazaji kuja Dodoma na kuleta mitambo yao na gharama za Watumishi kuwaleta Dodoma. Kazi hiyo inafanywa na Studio ya Bunge. Uelewa mdogo!
Kazi hiyo inafanywa na Studio za Bunge, inapelekwa kwenye satellite, chombo chochote kila uwezo wa ku-link na kuchukua matangazo haya na kuyarusha kwa gharama nafuu na hivyo inaongeza idadi ya watazamaji, inapunguza gharama na inafanya kazi ya Bunge hapa ionekane zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uongo wa kusema utaratibu huu…
MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, naomba mtulizane, tumsikilize Mheshimiwa Waziri.
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, uongo wa kusema kwamba utaratibu huu unawanyima haki wananchi, pengine tukubaliane, wenzetu wanaposema tafsiri ya mwananchi wanamaanisha mwananchi yupi? Huyu mama ntilie! Huyu mpiga debe! Huyu Machinga! Au wanamzungumza mwananchi yupi?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Sisi tunamzungumza mwananchi ambaye anaamka asubuhi, anakwenda kufanya kazi zake, jioni anarudi nyumbani kwenda kupumzika, anapata muda wa kutosha wa kuliangalia Bunge na kushuhudia kinachoendelea hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninajua wenzetu wana agenda nyuma ya hili, lakini Watanzania wametuelewa, dhana ya Hapa Kazi Tu imeiweka Serikali hii madarakani, tuendelee bila kurudi nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie pia Watanzania hili, jambo ambalo hawaambiwi; inaonekana kama vile utaratibu huu ni wa ajabu sana, lakini Tanzania siyo nchi ya kwanza kwa Bunge lake kuwa na Studio yake na kufanya kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabunge yote ya Jumuiya ya Madola yameweka Studio za Bunge, yanafanya utaratibu huu tunaoufanya, tena sisi tumeenda mbali tumetoa uhuru kuliko ule uliotolewa na Mabunge mengine. Vile vile Serikali na Bunge tumezungumza na Wanahabari na kuwahakikishia kwamba utaratibu huu kwa Bunge letu ni mpya. Kama mpya, unaweza ukawa na upungufu wake katika utekelezaji wake. Serikali na Bunge tuko tayari kukaa na Wanahabari tukaangalia upungufu uliopo katika utekelezaji wa mpango huu, tukauboresha, tukautekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo, tunaomba watuunge mkono. Wameendelea kutuunga mkono na tutaendelea kufanya hivi; Watanzania wanatuelewa, dunia inatuelewa na wasiotuelewa leo watatuelewa kesho, wala siyo mara ya kwanza wao kutoelewa kwa mara ya kwanza. Tutaendelea namna hiyo, tutafanya na tutasonga mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kuwapongeza na kuwashukuru sana, Wabunge wa Chama cha Mapinduzi kwa uzalendo wao na kuamua kubaki hapa kujadili na kutimiza wajibu wao wa Kikatiba, tofauti na wenzetu ambao wanalalamika Katiba inavunjwa, lakini wao wanatoka na kuivunja zaidi Katiba hii wanayodhani wanaitetea. Naomba niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wa CCM na nimalizie kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.