Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hii Wizara ya Viwanda na Biashara. Kipekee kabisa, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya Wizara hii. Pamoja na pongezi hizo, ninayo maswali hasa katika Mkoa wangu wa Geita.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipokuwa nikiangalia bajeti hii ya leo ya 2017/2018, kweli imezungumzia kwa habari ya kuwezesha kuwekeza kwenye miundombinu. Katika ukurasa wa 122 wa kitabu, umezungumzia kwamba Wizara imejipanga kujenga miundombinu hasa ya viwanda katika Mikoa mbalimbali ikiwemo na Geita, Dodoma pamoja na Katavi. Vilevile imejipanga kujenga mabanda ya viwanda kumi katika Mikoa hiyo hiyo ya Dodoma, Geita, Katavi, Manyara na Simiyu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kujenga hiyo miundombinu, lakini katika bajeti hii Mheshimiwa Waziri hajaweza kuzungumzia kabisa habari ya kufufua viwanda. Katika Mkoa wa Geita tunavyo viwanda ambavyo vimekufa.

Kwa mfano, kuna kiwanda cha kuchambua pamba pale Kasamwa. Vilevile katika Wilaya ya Chato tunaona jinsi ambavyo hakuna ambacho amekiandika katika hotuba hii. Kwa hiyo, wakati Mheshimiwa Waziri atakapokuwa ana-wind up naomba kufahamu kwamba Serikali inajipangaje kufufua hivi viwanda ambavyo kwa muda mrefu havifanyi kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivi vilipokuwa vinafanya kazi viliweza kuajiri vijana wengi katika Mkoa wa Geita na wengi walinufaika na kufaidika, lakini hapa sijaona. Kwa sababu azma ya Awamu ya Tano ni awamu ya viwanda; na nchi ya Tanzania kuelekea kwenye viwanda, kwa hiyo, ni vyema tuangalie uwezekano wa kuweza kufufua viwanda ambavyo kwa muda mrefu havifanyi kazi ili wananchi katika maeneo waweze kufanya shughuli katika viwanda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika Halmashauri ya Wilaya yangu ya Geita, kuna watu walitoka Wizara ya Viwanda na Biashara, walisema wanataka kuanzisha Kiwanda cha Sukari katika Tarafa ya Butundwe pale Salagurwa, lakini nimejaribu kuangalia kwenye kitabu cha bajeti sijaona mpango wowote katika suala hili. Napenda kupata maelezo kuhusiana na uanzishwaji wa kiwanda hicho katika Tarafa ya Butundwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu Mkoa wa Geita hatuna viwanda kwa kweli. Wananchi wameitikia sana huu wito wa kuwa na viwanda katika Taifa la Tanzania na wanasubiri viwanda hivyo. Leo hii tunaona jinsi ambavyo muda unakwenda, lakini hatuoni viwanda. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anieleze kabisa anapo-wind up hasa katika Mkoa wangu wa Geita juu ya suala la viwanda, tunajipangaje? Tunawekaje mkakati ili wananchi waweze kunufaika na viwanda hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najaribu kuangalia katika suala la miundombinu; nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali hasa kupitia Wizara ya Ujenzi kwa kuweka mpango wa kujenga barabara ya lami kutoka Kahama kwenda Geita kupitia Bukoli. Barabara hii itawezesha kusafirisha bidhaa mbalimbali pamoja na kuwezesha suala zima la viwanda katika eneo la Mkoa wa Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba katika upande wa barabara Serikali inajitahidi, napenda pia kuulizia upande wa umeme. Vijiji vingi havina umeme. Kama kweli tuna nia ya dhati ya kufanikisha suala la viwanda, ni vizuri Serikali iweze kuhakikisha sasa inafanya utekelezaji wa mpango wa kuleta umeme hasa vijijini, kwa sababu ni kweli kwamba Serikali ina mpango wa REA awamu ya tatu kuleta umeme katika vijiji mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningependa pia kusikia kutoka Wizara ya Nishati na Madini, waniambie kwamba ni lini sasa watahakikisha umeme unawaka katika vijiji na hasa katika Vijiji vya Halmashauri ya Wilaya ya Geita ili kuhakikisha kwamba ile azma ya viwanda inaweza kufanikiwa kwa sababu kuna umeme?

Mheshimiwa Naibu Spika, wawekezaji wanapokuja mahali, wanaangalia kama kuna miundombinu muhimu inayohitajika; kama hakuna umeme, wawekezaji hawawezi kuja; kama hakuna barabara, hawawezi kuja na kama hakuna maji, haiwezekani wawekezaji wakaja katika eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa maji, tuna Ziwa Victoria, liko pale. Serikali iwezeshe upatikanaji wa maji ya uhakika ili wawekezaji wanapokuja waweze kukuta miundombinu ikiwa safi kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Waziri alizungumzia kiwanda cha kutengeneza matrekta kule TAMCO, Kibaha, lakini sasa hajaelezea kiundani kwamba ni namna gani basi wananchi wataweza kupata matrekta kwa ajili ya kuwezesha kilimo? Naomba pia Mheshimiwa Waziri anapo-wind up aweze kuwaeleza wananchi namna tutakavyoweza kupata matrekta ili tuweze kuimarisha kilimo na kufanikisha suala la viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la elimu; nikiangalia Mkoa wa Geita tuna wilaya tano, hatuna hata Chuo cha VETA hata kidogo. Haiwezekani tukafikia uchumi wa viwanda bila kuwa na elimu; bila kuwa na VETA. Kwa hiyo, naiomba Serikali kupitia Wizara ya Viwanda, ishirikiane na Wizara ya Elimu kuhakikisha kwamba kila wilaya, sawasawa na Sera ya Taifa ya Elimu na Ufundi Stadi, kwamba kila wilaya inatakiwa iwe na Chuo cha VETA. Kwa sasa katika mkoa wetu hatuna Chuo cha VETA hata kimoja. Wilaya zote tano hatuna Chuo cha VETA. Hata katika mkoa hatuna Chuo cha VETA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, natumia fursa hii kumwomba Mheshimiwa Waziri kushirikiana na Mawaziri wengine wa Wizara ya Elimu pamoja na TAMISEMI tuhakikishe kwamba tunakuwa na Chuo cha VETA katika kila Wilaya katika Mkoa wa Geita ili wananchi, hasa vijana wetu wanaomaliza elimu ya sekondari ambao hawaendelei na masomo mengine, waweze kupata elimu ya ufundi stadi, hatimaye waweze kufanikisha azma ya kuweza kufikia maendeleo ya viwanda. Bila ujuzi, haiwezekani kabisa kufikia maendeleo ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, katika suala zima la maji; napenda kuiomba Serikali kwamba iwekeze zaidi hasa katika miundombinu ya maji. Kwa sababu ukilinganisha na maeneo mengine hakuna maji, lakini sisi katika Kanda ya Ziwa tuna Ziwa Victoria ambapo tukilitumia vizuri tuna uhakika wa kuweza kupata malighafi. Tunalo zao la pamba na mazao mengine ambayo yanakubali. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anapo-wind-up aweze kuelezea. Watu wa Mkoa wa Geita wana shauku ya kuwa na viwanda… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.