Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ulinzi na Usalama, JKT na wasaidizi wake wote na Wakuu wa Majeshi kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais Magufuli kwa kazi nzuri sana ya kuendelea kuiweka nchi yetu katika hali ya usalama na amani. Unaposikia amani inakuwepo si kazi rahisi, ni kazi ya Mheshimiwa Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda kwenye mchango wangu, na leo nitaongelea mikataba ya kimataifa; kwanza niweke vizuri Taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani ambayo imepotosha mambo mengi. Moja ya eneo ambalo imepotosha wanashauri kwamba jeshi litumike kufanya economic espionage; hii si kazi ya jeshi, economic espionage si kazi ya jeshi, tuwaachie wanaohusika na hiyo wafanye si wanajeshi. Lakini maeneo mengine ambako wamepotosha yako mengi, wanazungumzia kuhusu Al-Shabab na Boko Haram. Bahati mbaya hawajui hata historia ya Somalia wala ya Nigeria. Al-Shabaab ni kikundi cha kikabila kiko Somalia, ni watu wa kabila fulani huwa wanapingana na kabila lingine wamejiandaa na silaha zao ndiyo wanafanya mambo ya Al- Shabaab.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Boko Haram vilevile ina ukabila, ina element za ukabila kule Nigeria, lakini pia ni kutokana na matatizo ya kiuchumi, wanajiona kwamba wametengwa, wako marginalized ndiyo maana wameunda kikundi cha Boko Haram wanashambulia wananchi wengine wenzao wa Nigeria si mambo waliyoyasema wao ambao ni upotoshaji mtupu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia suala la Malawi, kwamba Malawi imesema haitakubali usuluhishi, wameyapata wapi? Usuluhishi huu bado, unafanywa na Kamati Maalum inaongozwa na Mheshimiwa Joaquim Chissano, Rais Mstaafu wa Msumbiji na usuluhishi haujatolewa. Sasa kusema Malawi wamekataa wamekataa wapi na lini? Kwa hiyo, hili wao ndio wachonganishi, wanachonganisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya kuingia kwenye Kamati za Siasa za CCM, huu ni uchonganishi na upotoshaji. Tumewahi kuwa na Wakuu wa Mikoa ambao si wana-CCM, tuna mifano hai. Mkuu wa Mkoa wa Geita hakuwa mwana-CCM, alikuwa haingii kwenye Kamati ya Siasa. Tulikuwa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma hakuwa mwana-CCM alikuwa haingii kwenye Kamati ya Siasa ya Mkoa, labda kama anaitwa kutoa taarifa maalum kwa sababu CCM ndicho Chama Tawala, kina majukumu ya kusimamia Ilani ya Uchaguzi. Hata wewe Waitara leo ukiwa Mkuu wa Wilaya ukaitwa kwenye Kamati ya Siasa utakwenda tu, huna ujanja kwa sababu CCM ndiyo inayoendesha Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona niyaweke sawa haya ili kuondoa upotoshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la usalama na ulinzi. Nimesema namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuweka nchi yetu katika hali ya usalama, lakini nishauri kidogo, usalama upo lakini lazima tuzidi kuuimarisha na kuulinda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasikia hivi karibuni kuna mashambulizi pale Mikoa ya Pwani, hasa Mkoa wa Pwani wenyewe, Rufiji, Kibiti watu wanauawa, jana au juzi kauawa Katibu wa CCM mmoja na wengine, lakini miaka miwili iliyopita tulisikia mauaji ya watu kule Tanga na mengine yalitokea pale Mwanza ya watu wengi na inaaminika kwamba haya mauaji yalifanywa na Al-Shabaab.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hii inayofanywa kule Pwani hatujui lakini inawezekana ikawa ni Al-Shabaab wanakuja wanaingia kwenye maeneo yetu, wanaleta madhara ambayo ni kuua watu. Sasa kuna taarifa kwamba Al-Shabaab wanaanza kufanya ushirikiano na Boko Haram, na kuna taarifa kwamba haya makundi mawili ya kigaidi wanajaribu kutafuta silaha za sumu (biological weapons), ambazo wazitumie kwenye mapambano yao na raia wasiokuwa na hatia huko Somalia, Nigeria na kwingineko. Tunasikia wanavyofanya Kenya wanaua watu huko shuleni, wanaua wanafunzi vyuo vikuu, wanafanya maangamizi sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama watapata silaha za sumu kama wanavyojitahidi kufanya, itakuwa ni hatari kubwa sana hata kwetu. Kama kweli waliingia wakafanya mauaji pale Tanga miaka miwili iliyopita, halafu wakiwa na silaha za sumu tutakuwa katika hali ngumu sana ya kiusalama. Tanzania na Somalia haziko mbali sana, kati yetu kuna Kenya tu kama kilometa 400 kutoka Somalia mpaka Tanga pale kwa kwenye Maji; kwa hiyo kuna haja ya kuimarisha ulinzi katika maeneo haya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.