Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa sana anayoifanya pamoja na Waziri husika wa Ulinzi na Usalama pamoja na wanajeshi kwa ujumla. Niwapongeze kwa kazi nzuri wanayoifanya ya uzalendo kwa nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nizungumzie sana suala la ulinzi na usalama hasa kwenye mipaka yetu. Mheshimiwa Waziri alipokuwa anawasilisha amezungumzia mpaka mrefu wa Mashariki. Mimi niiombe tu Wizara hii ielekeze nguvu sana kwenye mpaka wa Mashariki hasa kwenye maeneo ya Mkoa wa Pwani, Lindi na Mtwara ili kuhakikisha mipaka hii inaimarishwa vizuri. Maeneo haya kwa sasa yameanza kuwa na dalili za ugaidi. Ni dalili ambayo Jeshi la ulinzi ni vema likajipanga vizuri kudhibiti yale yanayojitokeza ili kuokoa Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuzungumzia ni mpaka wa Magharibi, kwa maana ya Ziwa Tanganyika. Niipongeze sana Serikali kwa kutuletea kituo cha Jeshi la Ulinzi kwenye eneo la jimbo langu pale Kata ya Ikola. Kituo hiki ni kituo muhimu na kimesaidia vitu vingi sana hasa mali za raia ambao kipindi cha nyuma walianza kuwa na wasiwasi mkubwa baada ya Waasi wa Kongo wale waliokuwa wakizidiwa wanakimbilia nchini kwetu na kufanya uhalifu kiasi kwamba wananchi wa mwambao wa Ziwa waliishi bila amani lakini baada ya kuweka kile kituo, ukweli kimewasaidia sana wananchi na amani ipo ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali hasa kupitia Wizara hii, tunaomba kile kituo mkiangalie kwa makini sana vitendea kazi ambavyo wanafifanyia shughuli pale havitoshelezi. Wanajeshi ambao wako pale hawana gari zuri la kufanyia kazi, hawana boti za doria ambazo kimsingi ni vitendea kazi vinavyohitajika ili viweze kusaidia usalama wa nchi yetu. Mimi nilikuwa naomba eneo hili liangaliwe sana, sambamba na kuwawekea umeme kwenye kituo chao ambacho wanafanyia kazi. Hata hivyo, bado wanajeshi wanaofanyakazi kwenye maeneo haya ni wazalendo kweli kweli; hata zahanati hawana. Mimi nilikuwa naomba Wizara iangalie umuhimu wa kuweka angalau kituo kidogo pale ambacho kitasaidia afya za wanajeshi kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kupitia SUMA JKT ambao tumewapa maeneo makubwa sana kwenye Wilaya ya Mpanda kwa ajili ya uwekezaji. Kuwapa nafasi ya kutengeneza mazingira ya uwekezaji kwenye Wilaya yetu kutasaidia sana kutoa elimu kwa wananchi hasa wa Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapojipanga kuwekeza kupitia SUMA JKT, niombe yale maeneo ambayo watakuwa wamepewa wafanye kazi ya kuwasaidia wananchi wanaozunguka miradi ile ya maendeleo kwenye eneo hilo. Hii ni sambamba na kuwashirikisha, kuwapa elimu hasa kwenye suala zima la kilimo,ufugaji pamoja na kusaidia pembejeo kama watakuwa wanazo kwenye maeneo yale ili Jeshi liwe na dhamana ya kutengeneza mazingira ya kwao na kusaidia wananchi ambao kimsingi Halmashauri imetoa eneo bure bila kutoza gharama ya aina yoyote. Ninaomba sana katika hili Serikali kupitia JKT lisaidie kwenye maeneo hayo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali, JKT wamepewa maeneo yale ni pamoja na kuomba msaada wa kusaidia suala zima la uhifadhi mazingira. Eneo hilo ni miongoni mwa maeneo ambayo yamekuwa na uvamizi wa mazingira ambayo wananchi wanaingia kwenye misitu; sasa tunaamini ujio wa SUMA JKT utasaidia pamoja na kutatua tatizo lile la uharibifu wa mazingira ambayo kila mara unakuwa inajitokeza kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hali ya usalama, tuna misitu mikubwa sana ambayo ni pamoja na Msitu wa Tongwe Mashariki, Msitu wa Tongwe Magharibi. Kimsingi eneo hili linahitaji msaada sana ambao tutahitaji SUMA JKT watakapokuwa wanafanya shughuli zao za uzalishaji watusaidie na hali ya kutunza usalama kwenye maeneo yale na ikizingatiwa maeneo ambayo tayari tulikuwa ni maeneo yaliyokuwa na wakimbizi, kwa sasa hivi ni maeneo ambayo tayari wamekuwa Watanzania wapya. Hata hivyo wapo wachache ambao wanafikiria mazingira bado ni yale yale. Kwa hiyo, tutaiomba Serikali idhibiti wale wachache wenye malengo mabaya tofauti na Serikali ili waweze kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niombe sana ushirikiano na Serikali kwa ujumla, kwamba tunaomba sasa nafasi za kazi zitakapotoka wananchi wa maeneo yale wapewe kipaumbele ili waajiriwe na Jeshi la Kujenga Taifa kwa sababu ni nafasi pekee ambayo tumeipata itakayowasaidia Watanzania wote kwa ujumla na Mkoa wa Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante.