Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kuhusiana na makadirio ya matumizi ya fedha ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inashuhudia mabadiliko makubwa katika mifumo ya maisha na mazingira ya kiusalama yasiyotabirika. Katika mazingira haya, ulinzi wa mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na uhuru wa nchi yetu ni jambo la kufa na kupona linalopaswa kupewa umuhimu mkubwa na wa kipekee sasa kuliko wakati mwingine wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika zama hizi za mabadiliko makubwa ya teknolojia na changamoto za ushindani katika ukuzaji uchumi wa viwanda, kama nchi usalama wetu na uhuru wetu unategemea sana uwepo wa jeshi imara la kisasa lenye weledi, vifaa vya kisasa, uzalendo na nidhamu ya hali ya juu. Hivyo basi ni wajibu wetu kama Taifa kuhakikisha inakuwepo bajeti ya kutosha itakayoliwezesha jeshi letu kukabiliana kikamilifu na changamoto za sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mkinga inapakana na nchi jirani ya Kenya. Katika jitihada za kuimarisha ulinzi Halmashauri ya ilitenga fedha za kujenga daraja ili kuwezesha ulinzi na ukaguzi wa mpaka wetu. Hii ni kutokana na ukweli kuwa kabla ya uwepo wa daraja hilo, ukaguzi wa mpaka wetu ilibidi ufanyike kwa kupitia Kenya. Kazi ya kujenga daraja hilo ilikabidhiwa kwa JWTZ. Natoa pongezi kwa JWTZ kwa kukamilisha kazi ya kujenga daraja hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuiomba Serikali iongeze nguvu katika ulinzi wa mipaka yetu kwa kuweka miundombinu muhimu kama barabara na madaraja yanayokidhi viwango na mahitaji ya kijeshi katika maeneo yote ya Wilaya za mipakani.

Aidha, fedha na jukumu la kujenga miundombinu muhimu katika maeneo haya ya kimkakati, kiulinzi na kiusalama lisiachwe mikononi mwa Halmashauri bali liwe jukumu la moja kwa moja la JWTZ.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Mwakijembe ni miongoni mwa kata 22 za Wilaya ya Mkinga. Kata hii ipo katika mpaka wetu na nchi ya Kenya na kwa miongo kadhaa wananchi hawa wamefanya kazi kubwa ya kuwa walinzi wa mpaka wetu. Naipongeza sana Serikali kwa uamuzi wake wa kuimarisha ulinzi katika Kata ya Mwakijembe kwenye mpaka wetu na nchi ya Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wakati naipongeza Serikali kwa hatua hii, utekelezaji wake umekuwa na dosari na hivyo kuitia doa Serikali. Doa hili linatokana na JWTZ kutwaa mashamba ya wananchi bila kutoa fidia stahiki kwa wananchi. Inasikitisha kuwa Jeshi lilitumia mabavu kuwapora wananchi ardhi yao tena kwa kufyeka mazao yaliyokuwa mashambani. Hali hii imeleta manung’uniko na wananchi wanaona wamedhulumiwa na Serikali yao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kihistoria eneo hili limekuwa mali ya wananchi kwa miongo na vizazi kadhaa. Hata pale Halmashauri ilipoamua kuanzisha skimu ya umwagiliaji, iliamua kuyajumuisha maeneo haya ya wananchi kwenye skimu lakini ikahakikisha umiliki wa maeneo hayo unaendelea kuwa mikononi mwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ifanye tathmini ya haraka kwa ardhi ya wananchi iliyotwaliwa ili wananchi hawa waweze kulipwa fidia stahiki. Wananchi ambao mashamba yao yametwaliwa ili kuwekwa kambi/ makazi ya jeshi ni Ndugu Benard Kinyili (ekari moja); Ndugu Ngoma Joseph (ekari moja na nusu); Ndugu Hamisi Joseph (ekari moja na nusu); Ndugu Mlewa Malonza (ekari mbili) na Ndugu Mwanza Kiziku (ekari mbili).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nikiamini kuwa malalamiko ya wananchi wa Mkinga yatapatiwa ufumbuzi wa haraka.