Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora kwa mwaka wa fedha 2016/2017

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora kwa mwaka wa fedha 2016/2017

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya njema aliyotujalia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza hotuba za Mawaziri, Mwenyekiti wa Kamati, Kambi ya Upinzani na kuna hotuba nzuri ambazo zinaleta msisimko kwamba, Watanzania hakika Rais hakukosea kuwateua hawa Mawaziri kuwa Mawaziri katika Wizara wanazozihudumia. Niwahakikishie tu wale ambao wana wasiwasi kwamba, watumishi hewa wataendelea katika Serikali yetu, haipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wale waliokuwa wanakwamisha tatizo hili la watumishi hewa kuondoka katika Serikali yetu wameondoka na wengine tunao humu humu ndani. Naomba pia Serikali iangalie namna sasa ya kuhakikisha kwamba hizi milioni 50 ambazo zitakwenda kila Kijiji ziwe na utaratibu maalum wa kuzifuatilia. Vijana au wanawake na makundi mbalimbali ambayo yamekwishaunda SACCOS yao na SACCOS yao ina uongozi unaoaminika, wao wapewe hizi milioni 50 kwa utaratibu maalum ambao pia utaruhusu kufuatiliwa kwa karibu kwa sababu hizi hela najua ni revolving fund, wengine watahitaji hizi fedha kwa ajili ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi kabla hazijatolewa makundi yapate elimu nzuri na zaidi ya yote yawe na uongozi, pia zifuatiliwe kwa karibu kuhakikisha kwamba, hazitumiki ovyo kama fedha ambazo zimewahi kutolewa na Serikali na hatukujua zimetumikaje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Manispaa yangu ya Dodoma Mjini, tuna upungufu wa watumishi 590 wa kada mbalimbali. Kukosekana kwa Watumishi hawa kunafanya maendeleo yasifuatiliwe kwa ukaribu zaidi. Mheshimiwa Waziri unayehusika na utumishi wa umma nakuamini kwa kazi zako nzuri na ofisi yako kwa sasa naiamini, kwamba tutakapoleta barua kwani tuliandika barua mwezi wa Machi mwaka huu hatutajibiwa, naomba sasa nitakapokuletea hiyo copy ya barua uhakikishe kwamba wale watumishi wa kada mbalimbali katika Halmashauri yetu ya Manispaa ya Dodoma tunawapata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna ukosefu wa Walimu 105 wa Sayansi na Walimu wa sayansi wamesomeshwa hapa UDOM (University of Dodoma), siyo vizuri Manispaa ya Dodoma tukakosa Walimu 105 wa Sayansi ambao wangewasaidia wanafunzi wetu. Sasa hivi tunajenga maabara na maeneo mengine katika Manispaa yetu tumekwishakamilisha maabara, lakini Walimu 105 hawapo. Nakuomba Waziri unayehusika na Wizara hii tusaidie kupata Walimu hao 105 na wale watumishi 590 hasa wa kada za chini ambao ni watendaji katika vijiji vyetu, watendaji katika mitaa yetu, watusaidie katika kusimamia maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Manispaa ya Dodoma haina ofisi. Tunafanya kazi katika shule iliyokuwa Sekondari ya Aghakan na wameshatuandikia barua wakitaka majengo yao. Iko siku tutakuta vifaa na samani na kila kitu vikiwa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kupewa barua na aliyekuwa Waziri wa Ujenzi Dkt. Kawambwa kwamba tunapewa ofisi ambayo inatumika na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwa sasa, lakini kwa sababu Mkuu wa Mkoa wa Dodoma hana ofisi na jengo lake linalojengwa kila mwaka tunaomba fedha, lakini fedha zinazoletwa ni kidogo mno hazisaidii kitu chochote, naiomba Serikali yetu sikivu, tumeomba pesa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Halmashauri ya Manispaa, tumeomba pesa kwa ajili ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, tunaomba hata kama ni floor moja ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, hata kama ni ground floor, basi ijengwe imalizike ili Mkuu wa Mkoa aweze kuhamia kwenye Ofisi yake na Halmashauri ya Manispaa wapate ofisi yao. Pale tunapofanya kazi kama Manispaa huwezi kuongeza hata kibanda cha mlinzi kwa sababu majengo yale siyo ya kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, hata hospitali ya Wilaya hatuna. Tumeomba bilioni 25 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya, Dodoma imekua, watu wako wengi, Wabunge wenyewe mmeongezeka, kwa hiyo hatuna hospitali ya Wilaya. Naomba sana kwamba zile bilioni 25 tulizoziomba, basi tufikiriwe kupewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wilaya ya Bahi hawana Hospitali, asilimia 80 ya wagonjwa wanaokuja Hospitali ya Mkoa wa Dodoma wanatoka Wilaya ya Bahi, kwa sababu hawana hospitali ya Wilaya. Naiomba Serikali yetu sikivu waone namna ya kujenga Hospitali ya Wilaya Bahi na hospitali ya Mkoa ibaki kama hospitali ya rufaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba maslahi ya Watumishi wa kada za chini sasa kwa sababu Mheshimiwa Rais ameagiza kwamba kusiwepo madeni kwa watumishi kama Walimu, Manesi, Maafisa Ugani, Polisi na kadhalika, Serikali ione kwamba madeni yale ya nyuma ambayo wanadaiwa na watumishi yahakikiwe na kama yamekwisha hakikiwa basi Watumishi walipwe haki zao maana naiamini Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwamba inafanya kazi kwa uhakika na kwa juhudi nyingi, kuhakikisha kwamba watumishi wanapata maslahi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu ya Chamwino tuna jengo la Halmashauri pale. Lile Jengo Mkandarasi anadai bilioni tatu ili kukamilisha ujenzi wa Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino. Naomba sana Serikali ikamlipe Mkandarasi anayejenga Ofisi ya Halmashauri ya Chamwino ili watumishi wale wawe katika jengo moja, kwa sababu Watumishi wa Wilaya ya Chamwino wamesambaa, wengine wako Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, wengine wanafanya kazi kwenye nyumba za watu binafsi, wengine wapo kwenye nyumba zisizoeleweka, lakini Mkandarasi akipata bilioni tatu alizoziomba jengo lile litakuwa limekamilika.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yetu ya Chemba pia hatuna Hospitali, hatuna nyumba za Watumishi, hatuna maji, hatuna kitu chochote. Naiomba Serikali yetu sikivu sasa ione namna kwa sababu Wilaya ya Chemba ni Wilaya mpya. Pia tuna mradi wa umwagiliaji wa maji wa GAWAE tuliomba milioni 533. Naiomba Serikali ione namna ya kupata hizi fedha ili kazi ya umwagiliaji kwa wananchi maana Dodoma ni Mkoa kame sasa iweze kutekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatamani kuwashusha wanawake wa Wilaya ya Bahi ndoo vichwani. Tuliomba shilingi milioni 400 kuvuta maji kutoka katika Kijiji cha Mkakatika. lakini tulipewa milioni 100 tu. Naiomba Serikali katika bajeti hii itukumbuke tunatamani wanawake wa Wilaya ya Bahi katika eneo la Makao Makuu ya Wilaya wapumzike kubeba ndoo vichwani. Tukipata milioni 400 tutapata maji Bahi katika Makao Makuu ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia hotuba za upande wa pili katika Bunge hili wakijinasibu kwa mambo mengi, kwamba Serikali inagawa maeneo na kulipa watumishi pesa nyingi na kuweka miundombinu badala ya kusimamia miradi michache ya maendeleo, hatuwezi kuacha kuwalipa watumishi, miundombinu ndiyo maendeleo…
(Hapa Kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.