Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii nyeti na muhimu kwa Taifa letu, Wizara ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia, ningeomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi na uwezo huu lakini niwashukuru sana wananchi wa Mikumi kwa kuweza kuniamini na kunikopesha kura zao, nawaahidi nitawalipa maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwanzo kabisa naomba nitumie nafasi hii kuwapa pole sana ndugu zangu wa Kilosa ambao siku mbili zilizopita tumepata maafa makubwa ya mafuriko. Wenzetu wawili wamefariki dunia, Mungu awalaze mahali pema peponi lakini pia familia nyingi zimetaabika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie hapo hapo ni kwamba katika Wilaya ya Kilosa imekuwa kama ni kawaida sasa hivi ikifika kipindi cha mvua basi mafuriko yanakuwa ni lazima. Hii imesababisha kuleta matatizo makubwa. Hivi ninavyozungumza mpaka sasa Watanzania wenzetu 4,765 wameathirika na mafuriko hayo, kaya zilizoathirika ni 1,238, nyumba 144 zimebomoka kabisa na heka za mashamba 3,707 zimeharibika kabisa na wenzetu wapo kwenye hali mbaya sana. Pia visima 18 vimeharibika kabisa, kwa hiyo, wenzetu wanapata taabu ya maji na vitu kama hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali, imekuwa kama kawaida kwa kule Kilosa ambapo inaonekana tatizo kubwa ni miundombinu ya barabara, madaraja pamoja na kingo za mito ambazo zinazidiwa na maji. Sasa hivi tunapozungumza ile barabara ya Mikumi - Kilosa ya kilometa 78 haipitiki kabisa. Ukitaka kutoka Mikumi kwenda Kilosa inabidi uzunguke mpaka Morogoro, ufike Dumila halafu ndiyo uelekee Kilosa kitu ambacho kinaleta taabu sana kwa wananchi wengi wa Jimbo la Mikumi. Taarifa hii tumeileta Ofisi ya Waziri Mkuu na imeahidi kutusaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, natoa ombi kubwa katika Kata ya Masanze tatizo kubwa ya mafuriko haya yaliyoleta maafa makubwa yamesababishwa na tuta la Mto Miyombo ambalo kila siku mvua zikinyesha zimekuwa zikileta taabu sana katika maeneo yale. Kwa Kilosa kwa ujumla wake Bwawa la Kidete ambalo limekuwa likimwaga maji kwenda pale Kilosa limekuwa likileta matatizo sana na ndiyo maana unaona kila mwaka tunakuwa na kazi ya kukarabati reli maeneo ya Godegode na Fulwe ambapo kila siku imekuwa ikisombwa na haya maji. Kwa Kata ya Tindiga kingo za Mto Mkondoa ndiyo zimebomoka na kuleta athari kubwa sana kwa wananchi wetu wa Kata ya Tindiga.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana Serikali tujaribu sana kuboresha miundombinu hii ili tuache kupiga zile kelele za kuomba misaada kila siku. Mwezi wa kwanza tu hapa nilimuomba Mheshimiwa Waziri, Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama akatusaidia tani 200 na sasa hivi tena tumeleta maombi tusaidiwe tani 100, tutakuwa tukiomba hivi mpaka lini? Tunaomba tutafute solution, tuangalie jinsi ya kukarabati mito au miundombinu hiyo. Nawaomba sana mngeiwezesha Wizara ya Mazingira kwa kuuboresha Mfuko wa Mazingira ili uweze kutumika katika kuboresha vitu kama hivyo. Vinginevyo kila siku tutakuwa tukilia ndugu zetu wanakufa na tunapeana pole.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kata ya Ruhembe tumekuwa tukipiga kelele kuhusu kuvuka Daraja la Ruhembe ambapo ndugu zetu wamekuwa wakitaabika. Ndilo hilo daraja ambalo kuna mwalimu mmoja ambaye ni Afisa Elimu amefariki dunia kwa sababu alikuwa anataka kumuokoa kijana aliyekuwa anabebwa na maji. Serikali ilishafanya upembuzi yakinifu wa daraja lile, ni daraja muhimu na la msingi, naomba itengeneze daraja hili ili kuokoa Watanzania wa Kata ya Ruhembe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nataka niongelee kuhusu utawala bora. Utawala bora ni pamoja na ushirikishwaji, uwazi na uwajibikaji. Tumekuwa kila siku tukisema na kupiga kelele tukiwaomba Wenyeviti wa Vitongoji na Vijiji watusaidie kwenye kampeni mbalimbali kwa sababu wenyewe ndiyo wanahusika na wananchi moja kwa moja. Mfano suala la elimu bure wahusika wa kwanza ni Wenyeviti wa Vitongoji na Vijiji. Tumekuwa tukiomba walipwe posho lakini imekuwa ngumu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbaya zaidi sasa hivi imefika kipindi viongozi wetu wa Serikali katika Wilaya zetu, mfano sisi Kilosa kuna Mkuu wa Wilaya ya Kilosa amekuwa akiingilia sana madaraka ya Wenyeviti wa Vitongoji na Vijiji kiasi kwamba amewafanya wakae na woga na kuwa na hofu kubwa. Hapa napozungumza Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbuyuni amesimamishwa na ofisi imefungwa na hili suala nililipeleka kwa Waziri wa TAMISEMI. Pia Mkuu wa Wilaya amefungia shimo la mchanga la Ruaha na kutisha kijiji cha Ruaha na kusema kwamba atauondoa uongozi wa Ruaha ni kwa sababu tu za kisiasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Ruaha ina vijiji vinne na vyote vimechukuliwa na CHADEMA, huo ndio ukweli. Ina vitongoji 21 na vitongoji 20 vimechukuliwa na CHADEMA, huo ndio ukweli na Diwani ni wa CHADEMA. Sasa msitake kuzuia haya maendeleo ya watu wa Ruaha kwa sababu tu za kiitikadi. Siku zote mmekuwa mkituomba tuonyeshe ushirikiano na tuwe pamoja lakini mnapokuwa mnanyanyasa viongozi wa vitongoji na vijiji inatuwia vigumu kuweza kupata yale maendeleo ambayo tumekusudia kuyapata. Ili kuboresha suala la utawala bora tuendelee kushirikiana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mkuu wa Wilaya ya Kilosa ameenda mbali zaidi, nilimuomba ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kuja kutusaidia kule kwa wakulima wa miwa ambapo aliingilia uozo uliokuwa unaendelea katika chama cha RCGA. Kwa sababu alisoma ripoti ya Tume iliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa na Mwenyekiti wake ni Mkuu wa Wilaya ilikuwa ikisema kwamba ule uongozi haufai, Mheshimiwa Mwigulu kwa ujasiri na kuwapenda Watanzania aliuondoa ule uongozi na kuweka uongozi mpya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kilichotustaajabisha ni kwamba yule Mkuu wa Wilaya anapinga maamuzi ya bosi wake yaani anasema Waziri alikurupuka…
MHE. JOSEPH L. HAULE: Anasema Waziri alifanya haya mambo bila kumshirikisha. Mkuu wa Wilaya ni nani mbele ya Waziri wake? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwambia Mheshimiwa Waziri ripoti hiyo ndiyo ipo vile, wakulima wale wa miwa wanakushukuru sana kwa sababu hata bei ya miwa imepanda kutoka 72,000 mpaka 79,000. Sasa hivi inavyoonekana hata percentage ya kuingiza miwa imepanda kutoka asilimia 45 kwenda asilimia 60 yaani wakulima wa nje wanaingiza asilimia 60 na wenye kiwanda wamekubali asilimia 40. Haya yote ni matunda ya wewe kutembelea kule lakini Mkuu wa Wilaya anataka kukukwamisha anasema wewe ni jipu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niende mbali zaidi, Mheshimiwa Mwigulu umeonyesha ushirikiano mzuri na kweli umeonyesha kwamba sio mzalendo wa tai bali ni mzalendo kutoka moyoni, nakupongeza sana ndugu yangu.
Nimshauri tu Ndugu yangu Mheshimiwa Nape kwa sababu Mheshimiwa Mwigulu alikuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chama Tawala na anafanya haya mambo kwa ajili ya Watanzania basi na wewe kwa sababu ulikuwa Mwenezi hebu achia TBC ionekane wazi na Watanzania waweze kukuelewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakwenda kwenye suala la afya. Suala hili kwenye Wilaya yetu ya Kilosa limekuwa ni zito kwani hospitali yetu ya Wilaya imekuwa na taabu nyingi, dawa zinachelewa kufika, tunapoomba dawa MSD zinachelewa na nyingine hawana kabisa na malipo yanakuwa yameshafanyika hatuwezi kupata dawa nyingine. Kitu ambacho kimetuumiza ni kwamba tumekosa misamaha ya kodi. Hospitali ya Kilosa iliagiza ambulance na kuiomba Serikali isamehe kodi ili waweze kuingiza ambulance ile lakini Serikali ilikataa kutoa kodi hiyo kwa kitu ambacho kingeweza kuwasaidia Watanzania wenzetu kule. Watanzania wanataabika na wanahitaji msaada mkubwa, inapofika sehemu tunaagiza vifaa tiba vya hospitali za Serikali ambazo zinakimbiliwa sana na Watanzania walalahoi basi tuangalie uwezekano wa kuweza kuwasaidia Watanzania kwa kuruhusu na kusamehe kodi zile. Kwa Kilosa haijafanyika hivyo na hili limekuwa ni pigo kubwa sana kwa sababu Hospitali ya Kilosa inahudumia wananchi wengi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi katika Zahanati ya Mikumi, zahanati ile ni kama haipo. Nilipoongea na Daktari wa zahanati ile ameniambia ile zahanati ipo lakini kama haipo. Tunategemea Hospitali ya St. Kizito ambayo ni ya private, ni ya mission na inapewa milioni sitini kwa mwaka lakini bado walalahoi wanashindwa ku-afford gharama za matibabu pale. Naomba Serikali kupitia Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI aweze kuboresha Hospitali ya Mikumi ili walalahoi wajisikie kwamba ni hospitali yao na waweze kutibiwa kwa bei rahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Hospitali ya St. Kizito kuna kaya maskini ambazo zinapata msaada lakini imeonekana zikienda pale zinakuwa charged kwa pesa nyingi, maskini mnamsaidia kwa kumpa chakula inakuwaje unamuomba hela za dawa? Mtengenezee hospitali yake ya pale Mikumi ili aweze kwenda akajisikia yupo kwake. Pale kwenye Zahanati ya Mikumi sasa hivi hata kupima malaria ni shida na watu wanalalamika, tumewashawishi sana waingie kwenye mfuko wa afya lakini wakienda pale hata kupima inakuwa ni shida wanaambiwa kapime dirisha lile kachukue dawa dirisha lile as usual. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nihamie kwenye suala la elimu…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.