Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa fursa ya kuiona siku hii ya leo, lakini vile vile naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Mwijage, Waziri wa Viwanda, kwa kweli ametutendea haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii hotuba kwa mtu ambaye anataka kuisoma na kuielewa, kwa kweli hakupaswa hata kuwa na maswali humu ndani. Nampongeza sana kwa kuwa hotuba hii imesheheni kila aina ya taarifa. Kuna takwimu, kuna maelezo, kuna mchanganuo; sasa sijui mtu unalalamika kuwa dhana ya viwanda huioni, unataka uione vipi?

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuipongeza sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, safari hii huu mkakati jamani utafanyika. Kwa vielelezo hivi vilivyomo humu ndani ni wazi kabisa viwanda vitakuja kufanyika. Mifano, tumeshaiona, viwanda vipya vimeshajitokeza vingi sana; someni haya majedwali jamani! Kama hamtaki kusoma hii literature yote kubwa, nendeni huku nyuma kwenye majedwali, yameainishwa kiwanda kipi, wapi, ukubwa gani, kwa faida ipi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niipongeze sana Serikali yangu, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na watendaji wote walioko chini yake. Kwanza tunaambiwa kabisa katika maendeleo yoyote ya uchumi duniani, nchi lazima iwe na political commitment. Commitment tumeiona kwa kupitia Rais wetu na Marais wengine wote waliopita. Commitment ya kuwa na viwanda nchi hii imekuwepo na sasa hivi ndiyo imetiliwa mkazo zaidi kwa kuweka kabisa mkakati wa kuwa sasa hivi tunaelekea kwenye maendeleo ya viwanda peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa suala linalofuata ni taasisi. Tunaambiwa kabisa ili nchi iendelee au ionekanae kuwa inaendelea inapaswa kuwa na taasisi muhimu. Taasisi hizo zinahusiana na masuala ya hatimiliki. Sisi chini ya Wizara hii tuna Taasisi ya Property Rights, tuna Taasisi zinazosimamia ubora wa mazao au bidhaa, tuna taasisi zinazosimamia miundombinu ya viwanda vidogo na vikubwa, tuna taasisi zinazoshughulikia usuluhishi wa migogoro kwenye biashara, tuna taasisi ambazo zinakwenda kujenga ufanisi wa viwanda kuanzia vidogo kabisa hadi vile vikubwa; tuna sheria ambayo inasimamia, tuna mkakati wa kimaendeleo wa viwanda wa tangu 1996 mpaka sasa hivi ambao umerejewa na sasa hivi umeboreshwa. Sasa zaidi ya hapo tunawezaje kusema kuwa hatuna mwelekeo wa viwanda? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitoka hapo tunakuja kwenye masuala mazima ya utekelezaji wa huo mkakati mzima wa viwanda nchini mwetu. Tunaona jinsi ambavyo kwa sasa hivi kwa mtazamo huu wa Serikali ya Awamu ya Tano kuwa sasa hivi viwanda hivi vinakwenda kuwajumuisha wananchi wengi zaidi. Kama zamani ilikuwa inaonekana viwanda viko sehemu chache tu za nchi, sasa hivi viwanda vinakwenda mpaka vijijini kwetu, vinakwenda mpaka kwenye Wilaya zetu, vinakwenda kwenye Halmashauri zetu, maeneo ya mikoa na wilaya ambayo yako tayari kwa ajili ya viwanda yameainishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri zetu wote wana ufahamu na uelewa kuwa wanahitaji kuwa na viwanda; tuna program zilizokuwepo chini ya Wizara hii zilizokuwa zikisema kila Wilaya iainishe zao moja ambalo wanaliona hilo ndiyo litakuwa linafaa kwa ajili ya kuendelezwa hadi kufukia level ya kiwanda; na hayo yamefanyika. Tuna Taasisi muhimu za kusimamia kama SIDO; kila mtu aliyesimama hapa amezungmzia SIDO, ni kwasababu ameuona umuhimu wake. Sana sana tutakachoweza kusema kwenye Serikali ni kuwa SIDO iwezeshwe zaidi kwa maana ya mitaji, kwa maana ya wafanyakazi, kwa maana ya program za kwenda kusambaza katika kila eneo kama ambavyo sera inasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutazungumzia BRELA. BRELA zamani ilikuwa inasajili majina ya Makampuni kwa maana ya wakubwa. Sasa hivi hata akinamama zangu kule kijijini wanaweza kusajili majina ya Kampuni zao au shughuli zao wanazozifanya. Hii imerahisishwa kiasi kwamba hata hawana haja ya kutembea kwenda Dar es Salaam au kwenye Kanda yoyote, hata kwa kutumia mitandao tu ya simu, Mabenki ambayo yameunganishwa. Sasa jamani unalalamika kuwa eti sijui urasimu; urasimu umepunguzwa kwa kiasi kikubwa. Ni sisi sasa kama viongozi katika Halmashauri zetu kuhamasisha wananchi kuwaelewesha jinsi gani ya kutumia nyenzo hizi ambazo Serikali imeziweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia suala la Stakabadhi ya Mazao Ghalani. Jamani, nani atakayeendelea kubisha sasa kuwa huo siyo mfumo ambao umewasaidia sana wakulima kupata bei bora kwa ajili ya mazao yao? Tuombe sasa mfumo huu wa stakabadhi uenezwe Tanzania nzima maana yake ulikuwa kwenye mazao machache, lakini vile vile haukuwa kila mahali. Wale wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo na wengi wao wakiwa ni wanawake wangependa sana na wao sasa kujumuishwa katika mfumo huu na kwa hali hiyo haya maghala na huu usimamizi upelekwe mpaka kwenye Wilaya zetu ili sasa wananchi wetu waache kurubuniwa na madalali wa mazao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia sera. Jana kuna mtu alikuwa anakashifu Sera ya Viwanda ya 1996 ambayo inaisha mwaka 2020. Mambo mawili makuu ambayo sera hii ilikuwa imelenga; kwanza ilikuwa ni kusambaza viwanda nchi nzima. Jamani, sera ikiwa inasema kitu kama hicho, ina ubaya gani? Inazungumzia inclusiveness ya viwanda nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera hii vile vile ilikuwa inazungumzia kueneza viwanda kwenye maeneo ya pembezoni. Mimi natoka kwenye eneo la pembezoni; Ileje ni Wilaya ya pembezoni na kwa muda mrefu sana tumekaa kwa kweli hatuna maendeleo makubwa sana zaidi ya kuwa ni wakulima wazuri, tunazalisha vitu vizuri. Sasa hivi naona Mkoa wa Songwe na wenyewe uko katika maeneo ya kuja kuwekezwa kwenye viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ktika Wilaya yangu, tayari SIDO wameshakuja kupata eneo na wako tayari kuja kuanzisha viwanda; Wilaya yangu sasa hivi inakwenda kubadilika, siyo ile Ileje ambayo mlikuwa mmezoea kuisikia. Wengine hata mlikuwa hamjui Ileje iko wapi? Sasa hivi mnaijua Ileje iko wapi. Ileje inaenda kupata barabara ya lami kubwa itakayofungua uchumi ule kwa kiasi kikubwa sana. Ileje kwa uzalishaji wake, sasa hivi inaenda kupata miundombinu ya Kituo cha Forodha mpakani na Malawi. Haya yote ni maendeleo. Tunaenda kupata Chuo cha Uhamiaji cha Kikanda, yote haya ni maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachosema mimi, kilimo chetu sasa hivi kinaenda kufanya usindikaji wa hali ya juu. Nasema barabara ile itakapoanza tu, Ileje itakuwa kama mzinga wa nyuki, shughuli zitavyoanza pale. Sasa hivi tu tayari tuna watu wengi sana wako tayari kuja Ileje, wanavizia barabara ikifunguliwa tu! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, anisikilize. Afanye kazi kwa karibu sana na Waziri wa Maji ambaye namshukuru Mungu safari hii ametuwekea fedha ya kutosha kuboresha miundombinu ya maji Ileje. Mheshimiwa Mwijage, Ileje tunalima sana mazao mengi; nafaka, mazao ya biashara kama pareto, tunalima soya, alizeti, mihogo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba viwanda Ileje nimeshaongea na Mheshimiwa Waziri mara nyingi, maeneo yapo tunamkaribisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi, najua hii hoja naweza nikaizungumza kutwa nzima.