Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba ya bajeti nzuri na utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mkakati wa ujenzi wa viwanda ili Tanzania ifikie hadhi ya nchi ya uchumi wa kati ifikapo 2025. Ni jambo la tija sana kwa uchumi wa nchi yetu na ukombozi kwa suala la ukosefu wa ajira kwa vijana na wananchi wetu. Serikali imezuia eneo la SEZ Bagamoyo jumla hekta 9,080. Mwaka 2008. Serikali ilitathmini eneo lenye ukubwa wa hekta 5,742 katika Vijiji vitano vya Zinga, Kondo, Pande, Mlingotini na Kiromo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wafidiwa walioainishwa ni 2,180 na fidia ya wakati huo ilikuwa ni shilingi bilioni 60. Mpaka hii leo hekta 2,399 zimetwaliwa, wafidiwa 1,155 wamelipwa jumla ya shilingi bilioni 26.4. Wananchi 1,025 hawajalipwa mpaka leo; miaka 10 sasa tangu mwaka 2008! Wananchi hawa wanadai jumla ya shilingi bilioni 51 (pamoja na interest).

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa wamesubiri miaka 10 kulipwa fidia na wamepata madhila mengi. Mheshimiwa Waziri atakapofanya majumuisho atuambie, lini wananchi hawa watalipwa fidia zao? Kwa vile mwekezaji ameainisha eneo atakalotumia kuwa hekta 3,000 tu: Je, hekta zilizobaki zitalipwa na nani? Lini? Kwa bajeti ipi? Mtindo huu wa kumtaka mwekezaji alipe fidia ya ardhi inapunguza vivutio vya uwekezaji katika nchi yetu, Serikali irudishe utaratibu wa Serikali kulipa fidia ili kushawishi wawekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa bandari Bagamoyo ni sehemu ya SEZ ya Bagamoyo. Ila katika mradi kuna wananchi 687 ambao wamepunjwa fidia zao. Sasa wameshahakikiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali. Serikali iwalipe fidia zao halali wananchi hawa. Mbona katika bajeti hii ya 2017/2018 haina kasma kwa ajili ya malipo ya fidia hii? Mheshimiwa Waziri awape jibu sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu wa ujenzi wa bandari Bagamoyo utahamisha kaya zinazofikia 2,000. Wananchi hawa waliahidiwa makazi mapya katika shamba la Kidogoni - Bagamoyo. Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda ni shahidi wa jambo hili, yeye alilisimamia alipokuwa DG, EPZA. Nyaraka mbalimbali za EPZA zinaonesha mpango na ahadi hiyo. Kwa vile Mwekezaji yuko tayari kulipa fidia, naiomba Serikali ifanye maongezi na mwekezaji afidie shamba la Kidogoni ili wananchi wahame eneo la bandari haraka.

Mheshimiwa Waziri atakapofanya majumuisho atueleze ni lini wananchi wanaopisha mradi wa bandari watapewa eneo la makazi yao mapya? Kuhusu mradi wa ujenzi wa bandari ya Bagamoyo, Serikali yetu imesaini mikataba ifuatayo: MoU Septemba, 2012; Framework Agreement, Machi 2013; na Implementation Agreement, Desemba, 2013. Kutia saini Fremework Agreement kulishuhudiwa na Rais Mstaafu Mheshimiwa Kikwete na Rais wa China Mheshimiwa Xi Jingping.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni mwaka wa tano. Kwa vile CMPort Holding na mbia wako Oman wana mtaji na uzoefu; na kwa vile CMPort watalipa fidia ya ardhi, naiomba Serikali yangu Tukufu Iharakishe majadiliano na Mwekezaji huyo ili ujenzi wa bandari ya Bagamoyo uanze mapema. Tangu tumeanza majadiliano mwaka 2012, CMPort wamekamilisha mikataba ifuatavyo:-

(i) Sri Lanka, tayari wanaendesha Colombo International Container Terminal (CICT).

(ii) Nigeria, tayari CMPort inaendesha Tin-Can Island Container Teminal.

(iii) Togo, tayari, CMPort inaendesha Lome Port Container Terminal.

(iv) Djibouti, tayari CMPort inaendesha bandari ya Djibouti na Container Terminal.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi zinatuacha nyuma! Mheshimiwa Waziri akija kufanya majumuisho atuambie ni lini Serikali itakamilisha Mikataba na CMPort Holding? Ni lini ujenzi wa Bandari, Bagamoyo utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.