Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Kamanda wake Mahiri Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi nzuri na ya wazi ya kupeleka nchi yetu katika uchumi wa viwanda. Juhudi za wazi zinajionesha, kwa kipindi cha mwaka mmoja na nusu wa uongozi wake, viwanda vimeanza kuchipuka, SIDO imekua sana na wananchi wamekuwa wakijitokeza kuanzisha viwanda katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri inayofanyika. Mheshimiwa Waziri, pamoja na juhudi zote hizi zinazofanyika, bado Mkoa wa Ruvuma, Serikali na Wizara yake, haijatoa msukumo wa kuingiza Mkoa wa Ruvuma katika viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua Serikali ina mpango gani wa kuingiza viwanda Mkoani Ruvuma? Kipo Kiwanda cha Tumbaku ambacho mwezi Januari, 2016 Mheshimiwa Waziri Mkuu, alikitembelea na kujionea mwenyewe hali ya kiwanda hicho na alitoa maelekezo ya namna ya kufufua kiwanda hicho. Je, ni mipango gani ya Wizara ya kufufua kiwanda hicho?

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Songea hawana kiwanda chochote na hivyo kukosa ajira na manufaa yatokanayo na uwezo wa viwanda. Tegemeo letu kubwa ni pale ambapo Serikali ilionesha dhamira ya kuanzisha viwanda kwa kutenga eneo la EPZA pale Songea Mjini, lakini ni masikitiko makubwa kwamba hadi sasa eneo la EPZA limepimwa na watu wamehamishwa, lakini hawajalipwa fedha zao za fidia kutokana na ardhi na mali zao katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa hadi sasa, hawana mahali pa kwenda, umaskini umewapata, maana hakuna ardhi ya kilimo, hawana makazi wala hawana maendeleo wanayoweza kuyafanya kutokana na kushindwa kupata maeneo ya kufanyia shughuli za maendeleo. Pia wanazuiwa kuendeleza maeneo waliyokuwa wakiishi na kutakiwa kupisha shughuli za EPZA.

Mheshimiwa Naibu Spika, inatukatisha tamaa sana kwa namna tunavyoona wale wananchi wakipata shida katika eneo ambalo walikubali kulitoa kwa dhamira nzuri ya shughuli za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, tunawapatia lini wananchi hawa fidia zao wanazozidai? Ni imani yangu kuwa kuwalipa fidia wananchi hawa kutafuatia juhudi za kazi za Serikali kuanza kulitangaza eneo hili la Songea Mjini kwa wawekezaji waanze kuwekeza viwanda katika Mkoa wa Ruvuma.