Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri na Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wa viwanda na biashara katika ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Zipo changamoto nyingi katika kutekeleza sekta zilizopo chini ya Wizara husika hasa changamoto ya urasimu usiokuwa wa lazima kwa wawekezaji katika sekta ya viwanda nchini. Wawekezaji ni lulu inayosakwa na mataifa mbalimbali duniani ni lazima kuwa makini. Nashauri Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakikisha kwamba Tanzania Investment Centre (TIC) inatoa huduma zote zinazotakiwa kwa mwekezaji katika sehemu moja hasa suala la vibali na uhakiki ufanyike under one roof.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Viwanda na Biashara ni Wizara mtambuka inayopashwa kufanya kazi zake kwa kushirikiana na wadau na Wizara zingine kama vile Wizara ya Fedha kupitia sekta za mabenki, bima na TRA. Benki zinapofanya kazi zake vizuri na kuwa na riba rafiki katika uwekezaji mitaji katika sekta ya viwanda na kodi mbalimbali zinazotozwa zikiwa rafiki zitasaidia katika sekta zilizoko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa viwanda nchini kunategemea kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa malighafi kama vile chuma na umeme wa uhakika. Kwa kuwa nchi yetu imejaliwa kuwa na utajiri mkubwa kwa uwepo wa kiwango kikubwa madini ya chuma na makaa ya mawe na kwa kuwa makaa ya mawe yanapatikana Mchuchuma na Chuma cha Liganga, katika zoezi zima la uzalishaji chuma, makaa ya mawe hutumika na kinachozalishwa huwa ni chuma pamoja na umeme.

Nashauri Wizara kupitia Shirika la Maendeleo Nchini (NDC) lifanye kila linalowezakana kuhakikisha kwamba uzalishaji wa chuma Mchuchuma na Liganga unakamilika kwa sababu upatikanaji wa chuma na umeme nafuu utarahisisha uwekezaji katika viwanda nchini. Pia uwepo wa usafiri madhubuti wa reli na barabara na huduma bora katika bandari zetu hasa bandari ya Dar es Salaam kwani hili ni lango kuu la shughuli za kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini kutasaidia ukuaji wa sekta ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Viwanda na Biashara inao mchango mkubwa katika ukuaji wa sekta ya viwanda vya nguo katika Ukanda wa Ziwa ambako zao la pamba linazalishwa kwa wingi. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya nguo na ukamuaji wa mafuta, kwani uongezaji thamani wa mazao yetu utaleta tija kwa wakulima wetu na kuboresha maisha yao na kuchangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara.