Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Viwanda na Biashara pamoja na timu yake yote kwa ujumla kwa hotuba yake nzuri inayoonesha matumaini makubwa na zana nzima ya Tanzania ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama inavyofahamika kuwa Wilaya ya Lushoto ni ya Wakulima wa matunda na mbogamboga, na ndiyo biashara inayoipatia Halmashauri mapato makubwa. Pamoja na hayo asilimia kubwa ya matunda yale na mbogamboga vinaoza kwa kukosa soko. Kwa hiyo, niombe pamoja na kuishauri Serikali yangu iwakumbuke wakulima wa Lushoto kwa kuwawekea kiwanda angalau hata kimoja tu ili mazao ya wakulima yasiharibike.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama inavyofahamika Tanga ni Mkoa wa Viwanda lakini viwanda vilivyokuwa Mkoa wa Tanga vyote vimekufa, mfano kiwanda cha nondo, kiwanda cha sabuni, kiwanda cha nguo, kiwanda cha katani, kiwanda cha Mkumbara, kiwanda cha mbolea, kiwanda cha chai cha Mponde kimefungwa mpaka leo. Wakulima wa chai wanapata tabu hawajui hatma ya kiwanda kile na maisha yao yamekuwa ya tabu mno na ukizingatia kiwanda kile hakina tatizo lolote.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara ya mwisho Waziri alisema kiwanda cha chai Mponde ameshakikabidhi kwenye Mfuko wa Jamii (LAPF), lakini mpaka sasa Mfuko huu wa Jamii haujaonekana na wala hawajaonesha nia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba Mheshimiwa Waziri, uwafuatilie watu hao then utupe majibu ya kuaminika wawekezaji hawa watakwenda kufungua kiwanda kile. Pamoja na majibu hayo utakayoyatoa pia tungeomba ukayatoe wewe mwenyewe kwa wakulima wale kwani imefika hatua hawatuamini kabisa sisi viongozi wao. Msema kweli ni mpenzi wa Mungu kiwanda kile mpaka sasa kina miaka minne sasa hakuna muafaka, leo tusipopata majibu ya kuridhisha tutashika shilingi juu ya hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Mwisho kabisa nimwombe Mheshimiwa Waziri, aikumbuke Tanga na aikumbuke Wilaya ya Lushoto.