Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Namshukuru Mungu kwa kutuwezesha kufika hapa asubuhi ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nichangie katika hotuba hizi mbili, kwanza kwa kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa ushindi walioupata katika uchaguzi mkuu uliopita. Nampongeza sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, nampongeza sana Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, nampongeza sana Rais Dkt. Ali Mohamed Shein wa Zanzibar kwa ushindi walioupata na kuaminiwa na wananchi kuwaongoza katika Awamu hii ya Tano. Napenda kuwapongeza vilevile Waheshimiwa Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais na viongozi hawa wakuu watatu niliowataja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nataka kuwatia moyo kuwa sasa hivi wanachokifanya kinaonekana, wananchi wanakikubali na hao wanaosema tunamsifia Rais Magufuli, Rais Magufuli ameanza kusifiwa mpaka na nchi za nje, nchi za Ulaya, watamsifia bure kama hafanyi kazi? Nataka hilo ndugu zangu tuliweke kwenye perspective. Nataka kuwapa moyo, tulikuwa tunapigiwa kelele humu ndani kila siku tunaambiwa muangalieni Kagame, muangalieni Kagame, Magufuli sasa anafanya style ile ile ya Kagame mnamsema, inaonekana hamna jema. Mheshimiwa Magufuli na Mawaziri wako songeni mbele, Tanzania inawaona, wananchi wanawakubali na wanawapongeza na wako tayari kufanya kazi pamoja na ninyi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa pongezi hizo, nataka na mimi nichangie kuhusiana na masuala mazima ya utendaji wa Wizara hizi mbili hasa katika kuleta maendeleo ya wananchi katika maeneo ya Tawala za Mikoa na Mitaani.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natokea Ileje ambayo ni mojawapo ya Wilaya zilizoko pembezoni lakini zenye fursa kubwa sana za maendeleo kwa maana ya kilimo, ufugaji, uvuvi lakini inakabiliwa na tatizo kubwa la umaskini ambao unatokana na miundombinu mibovu. Ileje karibu inafikia miaka 40 sasa tangu ianzishwe kwa maana kuwa ilianzishwa tangu enzi za utawala wa kwanza wa nchi hii, lakini Ileje haijawahi kuona barabara ya lami hata moja. Matokeo yake mazao yote yanayozalishwa Ileje, uwezeshwaji wote unaofanyika Ileje, wananchi hawawezi kuinuka kwa sababu hawana kipato kinachotokana na biashara ya uhakika ya mazao yao au ya juhudi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Ileje imebarikiwa kuwa na rasilimali nzuri sana na hali ya hewa nzuri sana. Jiografia yake ni ngumu kidogo lakini vilevile ni baraka kwetu lakini bado tunakabiliwa na tatizo kubwa la miundombinu inayotuunganisha kwanza na Wilaya nyingine lakini vilevile kata kwa kata, vijiji kwa vijiji. Kutokana na muinuko na mabonde tunahitaji madaraja na vidaraja vingi sana Ileje na hivi vyote bado havijakamilika. Naomba sana Waheshimiwa Mawaziri mtakapokuja hapa mbele mtusaidie Ileje tunapataje barabara za lami zitakazotuwezesha na sisi kuendelea katika mfumo huu wa hapa kazi tu kwa kasi ambayo inategemewa. Ileje ina-potential ya kuzalisha kwa ajili ya viwanda vingi sana vya kuchakata mazao lakini hatuwezi kufanya hivyo kwa sababu hatuna miundombinu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna matatizo vilevile ya ukusanyaji wa mapato, hatuna vyanzo vya kutosha vya mapato kwa sababu hatufanyi biashara lakini vilevile tuna matatizo ya maghala na masoko ya uhakika kwa ajili ya kuuza mazao yetu. Ileje imepakana na nchi jirani za Malawi na Zambia. Kuna uwezekano wa biashara kubwa sana pale lakini hatuna masoko ya uhakika, hatuna vituo vya uhakika vya forodha vya uhakika kwa ajili ya kufanya biashara hizo. Nataka kuwaomba sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI utakapokuja hapa utuambie sisi utatujengea lini border post yenye uhakika ili na sisi tufaidi biashara kama Wilaya nyingine zinavyofaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika sana pamoja na kusema kuwa Ileje inazalisha kwa wingi sana lakini nikiangalia katika bajeti iliyopangwa kwa kilimo tu peke yake kwa Ileje ni shilingi milioni 10. Mikoa mingine ambayo haina potential kubwa kama hiyo ya uzalishaji inapewa mamilioni ya pesa. Naomba sana mkija hapa muangalie mtakavyo re-allocate na sisi ambao tuna potential ya kuzalisha na kulisha nchi nzima tuweze kupatiwa fedha ya kutosha kuboresha miundombinu yetu ya kilimo, ufugaji na uvuvi ili tuweze kuchangia katika Pato la Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna tatizo kubwa sana la upungufu wa walimu, upungufu wa watendaji katika sekta ya afya na hata Mahakama. Tumekuwa tukipata vibali lakini bado hatujaweza kuajiri kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Tunaomba sasa mtusaidie, shule zimeongezeka, wanafunzi wameongezeka tutahitaji walimu zaidi na hata hawa wachache tuliokuwa nao tuna tatizo kubwa la utoro kwa sababu wengi hawapendi kufanya kazi Ileje kwa sababu ambazo tayari nimeshazitaja. Kwa hiyo, naomba sana sisi ambao tuko kwenye Wilaya za pembezoni msitusahau, mtuchukulie pamoja na wengine wote tuendelee kwa pamoja kwa sababu ni haki yetu na vilevile ni sawa kwetu sisi kupata fursa hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja.