Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi siku ya leo kuchangia katika hotuba hii muhimu ya Wizara ya Kilimo, Uvuvi na Mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha leo kusimama katika Bunge letu kuchangia hoja hii. Pili, niishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kile kilichokifanya katika Wilaya ya Tunduru kwa kukamilisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, ambao umewezesha wananchi wa Tunduru kupata fursa kubwa ya kusafirisha mazao yao kwa wakati na kwa muda mfupi kuelekea kwenye masoko ya Dar es Salaam na maeneo mengine. Ninaishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nitakuja kwenye hoja ya Hotuba ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. La kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuunda mbinu nzuri ya usambazaji wa pembejeo, pembejeo ilikuwa ni kero kubwa sana hasa kwa wakulima wa Tunduru na maeneo mengine kwa sababu mfumo wa ruzuku ulikuwa unagombanisha wakulima pamoja na viongozi wao. Hata hivyo naomba sana jambo hili lichukuliwe maanani sana na lifanyike haraka kwa sababu wale wenzetu, wafanyabiashara ambao walikuwa wanafanya biashara hii hawatapenda mfumo huu uweze kufanikiwa. Kufanikiwa kwa mfumo huu inatakiwa mbolea ije mapema na kwa wakati na isambazwe katika maeneo yote ili wakulima waweze kununua mapema ili waweze kufanikisha malengo ya kilimo chao.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kilimo huwezi kuliongelea bila kuliongelea suala la ushirika. Mimi ni mwana ushirika, nimekuwa mtumishi wa ushirika miaka minane, kwa hiyo kuna jambo ambalo ni muhimu Serikali ilitilie maanani sana; na a hii mara ya pili naliongelea suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Tume ya Maendeleo ya Ushirika. Tume hii tangu imeundwa mwaka 2013 bado haijawa na uongozi kwa maana ya Mwenyekiti na Makamishna wake, jambo ambalo linafanya utendaji wa kazi kuwa hafifu zaidi kwa sababu wanafanya bila kuwa na uongozi kamili unaosimamia ushirika.

Pamoja na hayo hata watumishi wa Tume ya Ushirika walio wengi wanakaimu. Unajua mtu akikaimu muda mwingi maamuzi yanakuwa ya mashaka mashaka kutokana na kutokuwa na title kamili ya nafasi yake anayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Wizara ifanye juu chini ili wale wanaokaimu wapewe nafasi ya kuweza kuwahudumia Watanzania na kama hawafai basi wateuliwe wengine ili kuhakikisha kwamba Tume hii inaenda vizuri. Pamoja na hilo, watumishi wa Tume wapo katika ngazi mbili tu, ngazi ya Taifa na Mkoa, huko Wilayani hakuna mwakilishi wa Tume. Walio wengi wanategemea Maafisa Ushirika ambao wapo chini ya Mkurugenzi wa Halmashauri. Hawa wote wanafanya kazi ya ushirika, lakini wanakuwa chini ya Mkurugenzi, Mkurugenzi ana Mamlaka ya kumpa kazi nyingine nje ya ushirika ili aweze kutimiza malengo yake kama Mkurugenzi wa Halmashauri. Kwa hiyo naomba suala la watumishi kutoka Makao Makuu Mkoani basi wafike mpaka Wilayani ili kazi ya Tume iende sawa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukizungumzia suala la Tume huwezi kuacha shirika hili la COASCO. COASCO ndio wasimamizi wakubwa, ndio wanaokagua vyama vya ushirika vyote nchini. COASCO hawana watumishi wa kutosha, vyama vyetu vinachukua muda mrefu bila kukaguliwa. Na nilizungumza mara ya mwisho, hata kama ni mtoto wangu umempa ndizi auze mwezi mzima hujamkagua, siku ukienda kumkagua mambo hayataenda vizuri. Hilo ndilo linajitokeza kwenye vyama vyetu vya ushirika. Vyama vyetu vya ushirika vinakaa muda mrefu bila kukaguliwa, naomba sana muimarishe kitengo hiki cha COASCO kwa maana ya fedha na watumishi ili kuhakikisha kwamba kila mwaka chama cha ushirika kinakaguliwa ili kujua hesabu zake zinaenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la korosho. Mfumo wa Stakabadhi Ghalani Tunduru ulikwama kwa muda mrefu, mwaka 2011/2012 wakulima hawakupata mafao yao kwa kuwa Mfumo wa Stakabadhi ulileta hitilafu na wakulima wa Tunduru walikosa zaidi ya milioni mia sita themani kutokana na bei ya mazao yalivyouzwa kuwa nje na matarajio ambayo yalikuwepo. Kutokana na hili mwaka jana tumejitahidi tukawahamasisha wakulima wakakubali na sasa mfumo umeenda vizuri, bei imekwenda vizuri, nashukuru tena kwa barabara zile, imeleta wanunuzi wengi Tunduru.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo bado kuna wakulima mpaka leo wanadai korosho zao ambazo ziliuzwa chini ya mfumo wa Stakabadhi Ghalani. Jambo ambalo linarudisha nyuma jitihada tulizozifanya mwaka jana kuwalazimisha wale wakulima waingie kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani.

Kwa hiyo, naomba Wizara kupitia Tume ya Ushirika iende ikakague vyama vile, tuone ni wangapi wamekosa na tuone namna gani hatua gani inachukuliwa kwa wale ambao wamehusika katika kutumia pesa zile za wakulima na wao kusababisha kukosa hela halali kwa ajili ya korosho zao ambazo waliziuza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado ninaenda huko huko kwenye korosho kwenye suala la export levy. Export levy tangu imeanzishwa ilikuwa na lengo kubwa la kuzuia usafirishaji wa korosho nje zikiwa ghafi, na ku-encourage kubangua korosho tukiwa ndani ya Tanzania. Hata hivyo lengo hili bado halijakamilika mpaka leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, export levy asilimia 65 inaenda Bodi ya Korosho, katika asilimia 65 kuna kiasi cha fedha kinachotakiwa kitumike katika kuendeleza ubanguaji; lakini tangu imeanzishwa export levy hakuna kiwanda chochote kilichojengwa hadi leo. Naomba sana Mheshimiwa Wizara kupitia Bodi ya Korosho wafikirie namna ya kuitumia export levy kubangua korosho kwa wananchi wetu na kutumia export levy kuwakopesha wale walioonesha nia ya kuweza kubangua korosho ili kuongeza kipato cha mkulima wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, ningepena sana Serikali iliangalie suala la kuainisha pembejeo kwa wakulima ili uzalishaji uende sambamba na kalenda ya kilimo kama inavyoeleweka kila mara ambapo kilimo kinatumika. Tunduru na Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla ni wakulima wazuri, tuna mahindi mengi, Mpunga Tunduru tunalisha takribani asilimia nusu ya Mkoa wa Lindi na Mtwara wanapata mazao ya mpunga kutoka Tunduru. Mkituletea mbolea mapema naamini wananchi wetu watanunua mbolea hiyo mapema ili waweze kuzalisha zaidi na kuweza kuepukana na njaa kwa maeneo mengine ambayo hayazalishi kwa wingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.