Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Kwanza naomba nitoe tu angalizo kwa wasomi wa nchi hii, kwa maana ya kwamba tunasisitizwa sana tusome sayansi, lakini jiografia nayo tuisome. Ukisoma sayansi usiposoma jiografia haina maana. Nasema hivyo kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jioghafia ya nchi yetu inatofautiana kutoka mkoa hadi mkoa, kanda hadi kanda, lakini wataalam wetu wanapotuhudumia wanashindwa kujua hizo jioghafia. Nitoe mfano, wanapogawa pembejeo ile kalenda ya ugawaji wa pembejeo inakuwa ya nchi nzima na inakuwa ya tarehe zinazofanana wakati jiografia ya nchi yetu haifanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri sisi kanda ya Kusini tunapanda mahindi mwezi wa 12, lakini tumeletewa mbegu mwezi wa tatu. Juzi nimepigiwa simu tumeletewa mahindi ya msaada wa chakula, sisi sasa hivi tunavuna mahindi mwezi Januari sembe Wilaya ya Liwale ilifika kilo moja Sh.2,500/=, kilo hamsini ilikuwa ni Sh.100,000/=, mwone hiyo shida ya chakula. Leo tunavuna mahindi tunaletewa mahindi ya msaada hiyo yote ni kwa sababu hatuijui jiogafia ya nchi yetu. Hili jambo ni muhimu sana na ninyi mnaogawa pembejeo lazima mjue kwamba mkoa fulani unahitaji pembejeo aina fulani tarehe ipi na kwa msimu upi, hilo nilikuwa natoa angalizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile naomba nijielekeze kwenye Bodi ya Mazao Mchanganyiko. Bodi ya Mazao Mchanganyiko ni tatizo, na bodi hii lengo lake lilikuwa ni kuimarisha hayo mazao lakini imekuwa kinyume chake. Nitoe mfano zao la ufuta; sisi Kusini sasa hivi zao la ufuta linakwenda sambamba na zao la korosho, lakini sasa hivi baada ya kuona zao la korosho limefanya vizuri kwenye stakabadhi ghalani tukafikiria ufuta sasa tuuingize kwenye stakabadhi ghalani. Sasa tunauingizaje wakati bodi yenyewe inayoshughulikia mazao mchanganyiko bado haijawa sawasawa? Hakuna sera yoyote ambayo inaelekeza namna ya kutafuta masoko ya hii zao la ufuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Lindi zao la ufuta ukiondoa korosho linashika nafasi ya pili kiuchumi, lakini tatizo letu kubwa la zao la ufuta ni soko. Hapo naomba nitoe angalizo lingine, kwamba hawa jamaa zetu wa vyama vya ushirika, nimeona kwenye page fulani hapa wamesema kwamba kazi mojawapo ni kufanya utafiti wa masoko. Vyama vya Ushirika hawawezi kufanya kazi ya utafiti wa masoko. Vyama vya Ushirika shida yao kwamba kwanza hawataki ushindani wanataka mtu mmoja a-monoply soko ili na wao wapate. Unapotokea ushindani wa kibiashara kama vile ilivyotokea kwenye korosho mwaka huu wao kwa upande wao ni hasara kwa sababu hawakupata mnunuzi wa pamoja ambaye anaweza akawapa chochote. Kwa hiyo, tukiwaachia Vyama vya Msingi wafanye utafiti wa masoko hapa tutakuwa tunajidanganya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nimesoma ukurasa wa 31 kwenye vipaumbele vya Wizara ya Kilimo. Wametaja vipaumbele kama tisa hivi pale na kimojawapo wamesema kwamba kuwawezesha vijana kushiriki kwenye kilimo, wanashiriki vipi? Nimejaribu kupitia sasa mikakati yenyewe iliyopo baada ya kuorodhesha vile vipaumbele, nikaangalia sasa mikati iliyopo kuiendea vipaumbele, maskini, sijaona chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri kwamba kuweka vipaumbele bila kuwekea mikakati kwamba tunataka tuingize vijana kwenye kilimo, kilimo cha aina gani? Hiki kilimo cha jembe la mkono ambalo Mheshimiwa Waziri wa kwanza wa Wizara hii alisema anataka kuliweka hili jembe la mkono makumbusho, lakini nalo hatuoni mikakati yake? Sasa naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hebu ajaribu kutuainishia hivi vipaumbele tisa alivyovirodhesha hapa mikakati yako ni ipi kuviendea hivi vipaumbele?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwenye kuongeza thamani ya mazao. Hapa kwenye uongezaji thamani ya mazao nimeona kwenye ukurasa wa 37 amesema sijui bodi inakusudia kuleta mashine 14. Hata hivyo, Mikoa ya Lindi na Mtwara sifuri, sasa sielewi sisi kule Mikoa ya Lindi na Mtwara hatutakiwi kuongeza thamani ya mazao yetu au ndio kwa sababu sisi tuko Kusini kama inavyosemwa siku zote? Mimi sijaelewa, kwa sababu hata mashine za kuongeza thamani zilizotajwa hapa kwetu majanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile kwenye hii sekta ya kuongeza thamani wamesema tutashirikisha watu binafsi, lakini kwenye kushirikisha watu binafsi kuna matatizo huko; hatupati wawekezaji kwenye watu binafsi kwa sababu tumeongeza kodi zimekuwa nyingi mno. Ukianzisha hiyo kampuni OSHA atakuja hapo BRELA, sijui nani sijui TBS sijui TFDA, wote wanafanya kazi moja hiyo hiyo. Sasa huyu mwekezaji atakayekuja kuwekeza hiyo faida anaipata wapi? Ndiyo maana hata hapa Waheshimiwa Wabunge wengi wanachangia kwa kusema kwamba, bidhaa zetu zinashindwa kuuzika, zinashindwa kuingia kwenye soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bidhaa zetu zinashindwa kuingia kwenye soko kwa sababu bidhaa zake ziko juu, gharama ya uzalishaji iko juu. Ndiyo maana utakuta dawa ya mswaki leo ikitoka Nairobi inauzwa bei rahisi kuliko inayozalishwa hapa kwa sababu hapa kodi zimekuwa nyingi mno. Hebu jaribu kama Serikali kuna ile wanaita collective responsibility, nafikiri Wizara zote wakae pamoja waangalie tatizo letu liko wapi? Kwa nini bidhaa zetu zinashindwa kuingia kwenye soko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba niongelee suala la maghala. Ukiingia ukurasa 36 pametajwa maghala pale panatakiwa kujengwa maghala. Hata hivyo, ukiangalia kwenye Mkoa wa Lindi na Mtwara hakuna ghala hata moja. Yaani Mikoa ya Lindi na Mtwara ni kama vile haipo nchi hii, maana kila sekta wanayoitaja nikipekua hivyo vitabu sioni wapi wameandika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la zao la ufuta. Ununuzi wa zao la ufuta naomba, mwaka huu ilikuwa tuuingize kwenye stakabadhi ghalani lakini tumekwama kwa sababu ya bodi kama nilivyosema. Kwa hiyo, naomba ikiwezekana zao la ufuta mtengenezee bodi yake kwa sababu ni zao ambalo sasa hivi limeshapata umaarufu mkubwa linaiingizia pesa nyingi nchi hii. Kwa hiyo kama ambavyo kuna Bodi ya Korosho basi hilo zao la ufuta waliondoe kwenye mazao mchanganyiko na walitengenezee bodi yake ili na sisi tunaweza kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niongelee zao la ngano. Tanzania tunasindika ngano inayofika tani kama 1,500,000 hivi kwa mwaka, lakini katika hizi tani 1,500,000 Tanzania tuna kama 0.05 percent, ndiyo ngano ya kwetu. Sielewi sera ya nchi yetu hii ni nini? Kwa sababu sasa hivi ukiondoa mchele na mahindi, ngano inaongoza kwa ulaji lakini sioni mkakati wa Wizara wa kuimarisha hili zao ukiondoa tu kwamba linazidi tu kutupotezea pesa zetu za nje. Kwa hiyo, naomba tuone mkakati wa kufufua mashamba ya NAFCO ili na sisi tuweze kunufaika na sekta hii ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna ukurasa 37 kupitia mradi wa policy and human resource development. Nimeona hapa wamesema kwamba watajenga maghala lakini kama nilivyotangulia kusema, kwamba na sisi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara na sisi tunazalisha mazao na tunaomba maghala hayo nasi kule tuwe nayo. Mwaka wa jana tumepata shida sana ya maghala ya korosho, matokeo yake tukapata shida na usafirishaji nao ambapo barabara zetu kama mnavyofahamu ni mbovu. Kwa hiyo, nawaomba sana wanapopanga mikakati yenu, wanaopanga vipaumbele vyenu wajue kwamba Mkoa wa Lindi na Mtwara nako kuna watu nako kuna uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano wa zao la viazi. Viazi Mkoa wa Lindi tunapeleka mpaka nchi za nje lakini viazi Mkoa wa Lindi mimi kule kwetu Liwale kiroba kimoja cha viazi ni Sh.10,000/= lakini ukifika Dar es Salaam kiroba kile kile unakuta kinauzwa zaidi ya Sh.100,000/=; hivi hamwoni hii hasara wanayoipata wakulima wa Mkoa wa Lindi na Mtwara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kabisa, hii yote ni kutokana na shida ya usafiri tuliyonayo katika Mkoa wa Lindi na Mtwara hasa Wilaya ya Liwale, ndiyo maana nikasema kwa umoja wenu kama Serikali kwa collective responsibility wakae kwa pamoja waangalie ni wapi kunapatikana mazao gani na yatafikaje kwenye soko, hatimaye waone kwamba watu wale wananufaika na nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo nilikuwa sina mengi, naomba tuu nishie hapo ujumbe umefika.