Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Nianze kwa kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi pamoja na timu yao yote ya Wizara kwa namna ambavyo wanafanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze sana kwa sababu ya kuja na mpango mzuri hasa unaohusiana na mbolea. Kuna mambo mengi yamesemwa kuhusiana na mbolea lakini mimi nataka tu kutahadharisha mambo mawili au matatu. Mpango wenyewe ni mzuri wa kununua mbolea kwa pamoja, ni mpango mzuri sana. Mambo matatu tu ninayotaka yaweze kufanyika kwa wakulima wangu waliopo Maswa na Mkoa wa Simiyu kwa ujumla, moja ni bei. Najua mtatoa bei elekezi kwa sababu wale wauzaji wasije wakavuka pale, kwa hiyo, naomba bei iwe nafuu, kama itakuwa nafuu hakuna shida.

Pili, ni kufika kwa wakati, mbolea hiyo ifike kwa wakati kwa wakulima wetu, isipofika kwa wakati kama walivyochangia Wabunge wengine itakuwa haina maana sana.

Lakini la tatu kwenye mbolea, nataka tu kusema kwamba mbolea hii sasa ipatikane maeneo yote, siyo ukanda fulani tu upewe mbolea na ukanda mwingine usipate mbolea. Kwa sababu sasa tutakuwa na uhakika wa kuipata mbolea hii na inapatikana kwa wote basi ipatikane kwa wakulima wote nchi nzima. Hongereni sana kwa mpango huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze kwa kutoa tozo hizo ambazo zilikuwa zimerundikwa kwenye kilimo. Waheshimiwa Wabunge tozo hizi zilikuwa zinakwamisha mambo mawili, moja ni bei za mazao kwa ajili ya wakulima wetu zilikuwa zinakuwa chini kwa sababu tozo nyingi zipo pale. Pia zilikuwa zinakwamisha uwekezaji kwenye sekta hii ya kilimo, mifugo na uvuvi. Kwa hiyo, tunawapongeza sana kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze pia kwa kusimamia vizuri ushirika, ulishaanza kulegalega na kwenda tenge, lakini kwa ujio wenu naona sasa mambo yanaanza kurekebishwa kwa sababu wale walafi wa pesa mnaanza kuwachukulia hatua. Hongereni sana na endeleeni na maeneo mengine ambayo yamebakia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nawapongeza ni la pembejeo, mmesimamia vizuri habari ya pambejeo, ule wizi uliokuwa ukifanyika mmeusimamia vizuri na mpo imara katika hilo. Nataka muendelee kusimamia namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka sasa niishauri Serikali kwenye eneo la kilimo hasa kwenye uwekezaji. Uwekezaji kwenye kilimo umekuwa ni mdogo sana. Kwa muda wa miaka mitano iliyopita uwekezaji upande wa ukuaji wa kilimo ni mdogo sana. Kwa muda wa miaka mitano iliyopita kilimo kimekua kwa wastani wa asilimia 2.8, ni asilimia ndogo, lakini ukilinganisha ukuaji wa watu kwenye nchi yetu ni asilimia 2.7. Sasa ukijaribu kulinganisha ukuaji wa kilimo na ukuaji wa idadi ya watu karibu ni ule ule. Sasa ukikumbuka kwamba ukuaji wa kilimo ndiyo ukuaji wa kipato chetu maana yake ni kwamba kipato cha Watanzania wengi ambao wanaajiriwa kwenye kilimo hakijakua kwa kiasi kinachoweza kusemwa ni kikubwa, haujakua sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mfululizo wa ukuaji wa kilimo umekuwa ukiendelea kushuka kila wakati, kila mwaka umekuwa ukishuka. Mwaka 2014 kilimo kilikua kwa asilimia 3.4, mwaka 2015 asilimia 2.3 na mwaka 2016 asilimia 2.1. Sasa ukuaji huu ni mdogo sana. Tunapoendelea na ukuaji wa kilimo ukiwa mdogo hivi ni hatari kwetu kwa sababu bado tunategemea kilimo lakini pia ni hatari kwa Sera ya Viwanda ambayo Serikali yetu inaiendesha sasa hivi maana yake malighafi kutoka viwandani itakuwa ni kidogo na matokeo yake vile viwanda ambavyo Mheshimiwa Mwijage anaalika wawekezaji kila wakati na siku mbili zilizopita alikuwa akituelezea hapa kwamba ameweza kuanzisha viwanda vingi, vinaweza kuwa na hatari ya kufungwa baadaye kwa sababu ya vitakosa malighafi kwasababu ya ukuaji mdogo kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali iendelee kuwekeza kwenye kilimo kwa sehemu kubwa sana lakini pia Serikali hii iendelee kuhamasisha wawekezaji wengine hasa sekta binafsi ili iweze kuchangia kwa sehemu kubwa kwenye kuwekeza kwenye kilimo. Vinginevyo kama tukiitegemea Serikali yenyewe tu hatutafika kukamilisha kuwa na malighafi zitakazotosha kwa viwanda vile ambavyo tunategemea vianzishwe kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuwa tukitembelea Mkoa wa Shinyanga na Mwanza tulikuta kiwanda cha nyuzi cha pale Shinyanga kinachotumia raw materials (malighafi), pamba kwa wingi kimesimamisha uzalishaji wake. Tatizo mojawapo ilikuwa ni kwamba wamepungukiwa na pamba kwenye kiwanda chao. Kwa hiyo, tuongeze uwekezaji kwenye kilimo ili tuhakikishe kwamba malighafi nyingi zitakazopatikana zinatumika kwenye viwanda vyetu ambavyo vimekwisha kuanzishwa tayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninalotaka kuzungumzia ni umuhimu wa umwagiliaji kwenye nchi yetu. Nimekuwa nikizungumza habari ya umwagiliaji sana, lakini ni muhimu sana kwa wakati huu kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi ambayo tunafahamu sasa hivi mazingira ya dunia yamebadilika, kumeongezeka joto na mambo mengine na ukame unaongezeka. Sasa tusipotia nguvu kwenye umwagiliaji tutakuwa bado tunarudi nyuma kwa sababu kilimo cha kutegemea mvua hakitoshelezi mahitaji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha umwagiliaji kina faida nyingi, moja mkulima atalima muda wote kwa hiyo atakuwa na ajira mwaka mzima. Vilevile wawekezaji wanaokuja kuwekeza kwenye viwanda watakuwa na uhakika wa kupata malighafi wakati wote wa uzalishaji wa viwanda vyao. Pia umwagiliaji unatusaidia wakulima kwa sababu badala ya kulima mara moja utalima mara mbili ama mara tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna fursa kubwa sana kwenye suala la umwagiliaji kwenye nchi yetu. Takwimu tulizonazo zinasema tuna hekta milioni 29 zinazofaa kwa umwagiliaji lakini eneo linalomwagiliwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.