Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa hata hizi dakika tano. Kwanza kabisa, kwa haraka haraka, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Waziri kwa namna wanavyoshughulikia zao la tumbaku katika Mkoa wetu wa Tabora. Zao la tumbaku lilikuwa na changamoto nyingi sana, tumekuwa tunalalamika sana, lakini sasa tunakoelekea zao la tumbaku litamnufaisha mkulima wetu wa tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipongeze kwa hizi tozo ambazo zimepunguzwa katika zao letu la tumbaku. Baadhi ya watu wanasema hizi tozo hazimsaidii mkulima, lakini tozo hizi zimemgusa mkulima, zimemgusa mnunuzi, mwisho wa siku inagusa bei ya mkulima. Nina uhakika kabisa tunakokwenda, bei ya tumbaku itakuwa inamnufaisha mkulima wetu kwa sababu tozo nyingi zitakuwa zimepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba watusaidie kitu kimoja, tuna grades za tumbaku kama 67, hatujamsikia Mheshimiwa Waziri akilizungumzia hili kwa mapana ili kuondoa grades zilizopo kumsaidia mkulima wetu wa tumbaku auze katika grades ambazo zitamsaidia mkulima wetu wa tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, naomba nigusie pia suala la mbolea kwenye tumbaku na mahindi. Nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa wazo la bulk procurement, itasaidia sana. Ilikuwa vichekesho, mbolea ya kupandia ilikuwa inakuja wakati wa kukuzia, mbolea ya kukuzia ilikuwa inakuja wakati tunavuna. Kwa hiyo, ilikuwa haitusaidii sisi kama wakulima wa mazao ya tumbaku na mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kidogo nimwombe Mheshimiwa Waziri anieleze, asali ni zao linalofahamika au halifahamiki na Serikali yetu? Kwa sababu nimejaribu kupitia kitabu chake sijakuta sehemu hata moja ameizungumzia asali, asali ni zao ambalo linasaidia kipato cha mkulima katika maeneo yetu. Igalula na Urambo tunarina asali nyingi sana na ni asali bora kabisa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atueleze ana mkakati gani na wakulima wa asali ambao hawajatengenezewa mazingira yoyote ya kufanya asali yao iweze kuwasaidia kuongeza kipato. Vilevile Mheshimiwa Waziri, asali hii ikisimamiwa vizuri inaweza ikaongeza pato la nchi. Naomba Mheshimiwa Waziri aniambie kama anafahamu kuna sehemu wanarina asali na asali hii inaweza kusaidia nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie wafugaji kwa haraka haraka. Sisi katika Jimbo la Igalula tuna wakulima na wafugaji lakini hata siku moja hujawahi kusikia tuna migogoro kati ya wakulima na wafugaji. Ninachotaka nishauri, wafugaji wetu tusiwaone kwamba ni tatizo katika maeneo yote ya nchi, wafugaji wetu wana haki kama watu wengine katika nchi hii. Bahati mbaya sana hatujawa na mkakati mzuri wa kuwasaidia wafugaji wetu, hatujawatengenezea mazingira ya kufugia, maeneo ya kwenda kufugia, leo lazima tutamlaumu mfugaji kwamba ni mkorofi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna maeneo mengi ya reserve lakini labda tufanye tathmini, hayo maeneo yanastahili kuendelea kuwa reserve mpaka sasa? Maeneo mengi ya reserve watu wa maliasili wamekuwa wakiyatumia kama maeneo ya kupatia kipato. Wafugaji wetu wakienda kule wanakamatwa, wanatozwa faini kubwa bila sababu lakini ukiangalia Serikali haijatenga mazingira mazuri ya kumwezesha mfugaji huyu akafuga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niulize, hivi mkata mkaa na mfugaji wa ng’ombe, nani anaharibu sana mazingira? Inaonekana sana mfugaji akipeleka mifugo kwenye maeneo ya reserve anaharibu mazingira lakini magunia ya mikaa yanayoondoka kila siku katika maeneo yetu ni mengi sana. Naomba Serikali imwangalie sasa mfugaji, akitengewa maeneo mazuri, nina uhakika hatutakuwa na migogoro hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi katika Jimbo la Igalula tuna maeneo ambayo tulishatoa mapendekezo tuwaongezee wafugaji kilometa tano ili waweze kufanya shughuli zao za ufugaji. Mheshimiwa Waziri, sisi katika Jimbo letu hatuna migogoro lakini kama hatutatengeneza mipango mizuri ya wafugaji wetu migogoro itakuja na Waziri ndiyo atakuwa amesababisha migogoro hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Tizeba, tunamwambia mambo mengi hayafanyiki, lakini niombe Wizara ya Fedha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.