Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Ahmed Juma Ngwali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ziwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka kuendeleza pale ambapo pameachwa na Mbunge wa Mkinga, Mheshimiwa Dunstan Kitandula juzi Jumamosi alipokuwa akichangia. Niseme tu kwamba Mheshimiwa Dunstan Kitandula alikuwa ni Makamu Mwenyekiti wangu wa Kamati ya Uchumi, Viwanda na Biashara katika msimu uliopita ikiongozwa na Mwenyekiti makini, Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hoja mbili tu na zote zitahusu mambo ya uvuvi. Nilipochukua kitabu hiki nilikuwa nikiangalia kwenye cover ya kwanza hapa nikaona hii eco culture, nilipoiona nikaona mambo mazuri, nikafungua ndani hakuna kitu kabisa, niseme ukweli. Unapozungumzia eco culture huwezi kuzungumzia kutengeneza bwawa fulani ambapo mabwawa yenyewe yametengenezwa na wananchi, lakini unazungumzia dhana pana sana ambayo ni lazima Serikali iwe imejipanga katika kuhakikisha kwamba hiyo eco culture (ufugaji wa samaki) ambao sasa hivi karibu nusu ya watu duniani wanakula samaki wa kufuga, inafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uwe na eco culture lazima uwe na fishing habours ambazo hutuna. Katika bajeti ya mwaka 2016/2017, ametenga shilingi milioni 500 pesa za ndani kwa ajili ya utafiti pamoja na shilingi milioni 24 za nje kwa ajili ya utafiti. Hebu tukitoka Waziri nitampa clip, Kenya wametenga bilioni 6.6 kwenye eco culture sasa lazima uwe na hizo fishing ports ambazo zitakuwa na dry dock, kutakuwa kuna maji ya kutosha, kutakuwa na facilities zote, ndiyo unaweza kufanya jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia inatakiwa uwe na fisheries laboratory, hakuna lab zozote za kukagua hao samaki kama wana viwango au hawana. Inatakiwa kuwe na fish market, soko la nje na la ndani la kuuza samaki hao lakini pia ahamasishe walaji wa samaki kwa sababu kiwango cha kimataifa sasa hivi cha ulaji wa samaki, kila mtu anatakiwa ale kilo 20 kwa mwaka, Tanzania tunakula nusu yake, tunakula kilo nane kwa mwaka. Kwa hiyo, lazima fedha hizo zitengwe kwa ajili ya kuhamasisha watu wale samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia unatakiwa uwe na ile fish landing site. Sehemu ambayo utaweka hizi eco culture zako, ufugaji wa samaki ambayo imefanyiwa uchunguzi wa kutosha lakini na mazingira lazima yawe yameandaliwa, sijui kama Sekta ya Mazingira wana study yoyote waliyotoa juu ya suala hilo la ufugaji wa samaki. Vilevile unatakiwa uwe na viwanda vya kuchakata hao samaki, huna. Unatakiwa uwe na cold chain facilities pamoja na ice plant, huna. Sasa hao samaki jamani wana mipango gani, watuoneshe hiyo mipango ambayo kweli wanayo kwa ajili ya huo ufugaji wa samaki. Hamna mipango yoyote na haimo humu, humu wameandika tu, wamekaa na wataalam kaandikiwa Waziri, wame-copy sijui mahali gani, wameweka, hakuna kitu, hiki hapa kitabu hakuna chochote ndani yake, hiyo ilikuwa hoja yangu ya kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kuu inahusu uvuvi katika Bahari Kuu. Uvuvi katika Bahari Kuu, hicho nacho ni kichekesho cha mwaka. Kwanza nataka kujua, wametoa leseni ngapi kwa mwaka huu na meli ngapi zilizokuja kuvua katika Bahari Kuu na meli ngapi zilizokamatwa lakini na mapato. Nataka kujua katika Bahari Kuu mwaka 2016/2017 wamepata kiasi gani? Nilikuwa nikizungumza na Zanzibar Makao Makuu juu ya suala la mapato wakaniambia na ni uhakika, vinginevyo itakuwa wamefanya tofauti hawakuwaambia wenzenu wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015/2016 fedha zilizopatikana katika uvuvi wa Bahari Kuu ilikuwa ni Dola za Kimarekani milioni 2.9 lakini mapato 2016/2017 yameshuka mpaka dola laki 6.9, mapato yameshuka. Watuambie kwa nini mapato yakashuka kwa kiwango hicho, ni kwa nini vinginevyo watakuwa wanafanya tofauti, Zanzibar hawajui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu tatizo lenyewe hizo pesa zinagawiwa katika mafungu matatu; 50 percent inakwenda kwenye mamlaka, asilimia 30 inakwenda kwa Jamhuri ya Muungano na asilimia 20 inakwenda Zanzibar. Sasa ukizigawa hizo pesa, dola 600,000 maana yake Mamlaka zinakwenda kama dola 300,000, ukija ukigawa 30 percent maana yake zinakwenda kama dola 100,000 na kidogo Jamhuri ya Muungano, Zanzibar zinakwenda dola 60,000. Sasa niulize, jamani ni kweli wako serious? Mapato ya Bahari Kuu nchi inapata dola 100,000, sawasawa na msimamizi wa ghala la unga la Bakhresa? Nchi inapata dola 100,000 mapato ya Bahari Kuu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu sasa walipoona hilo hawaliwezi, wakaja tena na jambo la ajabu, wakaja kubadilisha regulations. Wanasema wanataka kubadilisha regulations kwenye sehemu za kodi lakini tuzungumzie kuhusu bycatch, tuzungumze pia na mabaharia. Hizo regulations ambazo wamebadilisha, wanataka sasa kwamba wale wavuvi wanaovua Bahari Kuu, zile meli zikishapata samaki wale bycatch eti ichukue ije iwauzie katika nchi husika. Sasa mtu anavua katika Bahari Kuu mbali huko aje na meli mpaka ufukweni ambapo hiyo bandari yenyewe huna kwanza lakini na hiyo gharama ya mafuta na mambo mengine atazipata wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu uvuvi wa tuna ni uvuvi wa ndoano kwa hiyo haiwezekani. Halafu utajuaje kwamba wamepata bycatch wangapi, wala huna utafiti, wewe unaona meli ikiingia inakwenda kuvua utajuaje sasa, huwezi kujua. Kwanza nataka kujua ni meli ngapi zilizovua safari hii? Hizo meli zenyewe za kuvua hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda unakwenda mbio, nizungumzie suala zima la meli za uvuvi. Tanzania imesajili meli za nje ambazo zinapeperusha Bendera ya Tanzania 407, 407 ukizitia pale Dar es Salaam pote pale baharini zikipeperusha Bendera ya Tanzania huwezi kuona kitu. Katika hizo meli 407, Waziri hajui meli za uvuvi zilizosajiliwa ni ngapi au Waziri atuambie meli za uvuvi zilizosajiliwa ambazo zinazopeperusha Bendera ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambazo yenyewe haikusajili Jamhuri ya Muungano wala Zanzibar haikusajili imesajiliwa na Kampuni ya Feltex iliyopo Dubai, kwa hiyo hajui. Pia hajui ana mabaharia wangapi anasema sasa, katika hizo kanuni wanazobadilisha wataingiza mabaharia katika meli ambazo zitakuja kuvua, nani unampa leseni halafu unamwekea masharti, haiwezekani. Hata hizo kanuni mnazozibadilisha ni kiini macho tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watafanya vilevile kama lilivyokuwa zao la ngozi, zao hilo tuliweka 20 percent kodi kusafirisha nje, halafu tukaweka 40 percent kodi kusafirisha nje, lakini viwanda hakuna. Mwisho mwaka 2012 tukaweka kodi asilimia 90 ambayo ngozi ikawa inasafirishwa kwa njia ya magendo kwa sababu hata ukiiacha hapa inaoza. Sasa ndiyo hilo wanalofanya wao, wataweka kodi kubwa, wataweka sheria nyingi, mapato hayo wanayoyapata, hiyo 100,000 watakuwa hawapati, hilo ndilo tatizo lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisema asilimia 90 kama ya ngoziā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.