Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia. Kwanza niunge mkono wale wote walioonesha concern ya bajeti ndogo ya Wizara hii ya Kilimo. Tukizingatia umuhimu wa kilimo na namna tunavyoelekea kwenye uchumi wa viwanda kwenye nchi yetu, sekta ya kilimo ni muhimu sana kwa ajili ya uzalishaji wa mali ghafi lakini ajira na kutengeneza kipato kwa wananchi wetu ili waweze kununua bidhaa zitakazozalishwa na viwanda hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunapofikiria kuingia kwenye uchumi wa viwanda ni muhimu sana tukaimarisha kilimo chetu kuwa kilimo cha kisasa zaidi na hasa kuwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji. Tunaweza kuwekeza vizuri kwenye kilimo cha umwagiliaji kama tutazingatia rasilimali tulizonazo kwenye maeneo yenye resources kama maji, kwa mfano kwenye maeneo ya Ziwa Viktoria hususani eneo la Ukerewe kidogo inaleta shida kwenye eneo kama Ukerewe ambalo limezungukwa na maji wananchi wa Ukerewe kulalamika kutokuwa na chakula cha kutosha. Tuna maeneo ya kutosha ambayo Serikali inaweza kuwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji tukazalisha chakula cha kutosha tukaweza kukabiliana na hali tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nitake tu kujua kuna Mradi wa Kilimo wa Umwagiliaji kwenye Bonde la Miyogwezi na Bugolola. Kwenye bonde la Miyogwezi iliwekezwa zaidi ya shilingi milioni 600 na Serikali lakini pesa ile imewekwa pale ule mradi haukuendelea, lakini kama Serikali ingeweka mkazo ikaweka pesa nyingine ya kutosha mradi ule ukaanza kufanya kazi, kusingekuwa na tatizo la chakula kwenye eneo la Ukerewe, inawezekana wangeweza kutoa chakula zaidi nje ya eneo la Ukerewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kufanya vizuri kama hatuwekezi kwenye utafiti kwenye eneo la kilimo. Ni vizuri sana tukawekeza kiasi cha kutosha cha pesa kwenye utafiti, kutambua kwamba changamoto zinazokabili maeneo yetu hususani kwenye udongo tulionao ni zipi, ni mbegu zipi tunaweza kutumia ili tuweze kutoa mazao ya kutosha yanayoweza kutusaidia kuhimili changamoto tulizonazo za chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kuchangia ni uvuvi. Uvuvi kwenye eneo la Ziwa Viktoria ni muhimu sana na kimsingi kama Taifa uvuvi unachangia sehemu kubwa sana ya pato la wananchi wetu. Kwenye maeneo ya ziwa kwa mfano Ziwa Viktoria, sehemu kubwa ya vijana kwenye Mikoa ya Kanda ya Ziwa wanapata riziki yao na kuchangia kwenye uchumi wa nchi hii kupitia ziwa hili lakini kumekuwa na changamoto nyingi sana kwenye sekta ya uvuvi hususani kwenye Ziwa Viktoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua kutoka kwenye Wizara ni kwa nini wavuvi wetu hawafikiriwi sana kupata mikopo. Kuna Benki ya Wakulima, ni namna gani inawasaidia wavuvi? Kwa sababu wavuvi hawa kama watapata mikopo, itawawezesha kufanya shughuli zao katika mazingira mazuri na kuweza kutengeneza ajira nyingi zaidi lakini sioni kama benki hii ina msaada kwa wavuvi wetu. Hata taasisi nyingine za kifedha ni namna gani wavuvi hawa wanaweza kupata mikopo kupitia rasilimali walizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana katika mazingira yalivyo sasa wavuvi hawawezi hata kutumia rasilimali walizonazo kama dhamana kuweza kupata mikopo kwenye taasisi za kifedha. Niiombe Serikali ione umuhimu wa kuwajengea mazingira mazuri wavuvi wetu kupata mikopo ili watengeneze mitaji yao kuwa imara zaidi na kuzalisha ajira nyingi lakini na kutengeneza uzalishaji mkubwa wa mazao ya ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sekta ya uvuvi inakabiliwa na changamoto nyingi sana ambazo ningependa Serikali iweze kuzifanyia kazi. Nashukuru kwamba Serikali imeanza kuona matatizo ya tozo zilizopo kwa wavuvi lakini bado kuna tatizo kubwa la tozo nyingi kwa wavuvi wetu. Niombe Serikali iendelee kulifanyia kazi, kwa mfano, kuna tozo za SUMATRA, leseni za uvuvi na tozo za kupaki.

Ningeomba Wizara inieleze hivi inakuwaje mimi ninayemiliki gari naweza kuchukua leseni na bado nikafanya shughuli zangu na gari langu kwenye maeneo yote Tanzania nzima lakini mvuvi anapokuwa na leseni ya uvuvi akitoka Halmashauri moja kwenda nyingine analipa tena leseni nyingine ya uvuvi, akitoka Halmashauri hiyo akienda Halmashauri analipa tena leseni ya uvuvi ni kwa nini kuwa na matatizo haya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mazingira ya uvuvi yanabadilika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)