Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kwenye hotuba ya bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano chini ya kiongozi wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada kubwa ya kukuza uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka huu wa 2016/ 2017, haukuwa mzuri hasa bajeti ya maendeleo kutokana na fedha kidogo zilizotolewa na Hazina ambazo ni asilimia
3.31 tu ya fedha zilizoidhinishwa na Bunge. Naishauri Serikali yetu ihakikishe fedha zote za maendeleo zinazoidhinishwa na Bunge kwa Wizara hii zitolewe kwa wakati ili tulete mabadiliko makubwa ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya bajeti ya Waziri wa Kilimo Mifugo na Uvuvi haikueleza kwa namna gani Serikali itamaliza migogoro ya wafugaji na wakulima. Jimbo langu la Morogoro Kusini limekumbwa kwa kiasi kikubwa sana na migogoro ya wafugaji na wakulima na wananchi wanaathirika, wapo waliopoteza maisha yao, waliopata ulemavu na waliopata umaskini. Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi haijasema Serikali imejipanga vipi kuitafutia ufumbuzi wa kudumu wa migogoro hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufugaji wa sasa wa ng’ombe kwa utaratibu wa kuchunga mashambani hauna tija. Wizara ijipange kufanikisha ufugaji wa kisasa wa zero grazing. Nchi za Botswana na Namibia zinaweza kuwa mfano mzuri wa kuigwa, tujipange na sisi kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo katika bajeti hii bado hakijapewa umuhimu unaostahili kwa kuzingatia rasimali zinazotengwa, kilimo cha trekta na umwagiliaji ndicho kitakacholeta mapinduzi ya kilimo nchini. Kwenye bajeti hii, mikopo ya kununua trekta ni kidogo mno. Mfuko wa Taifa wa Pembejeo umepanga kutoa mikopo ya matrekta 71 tu kwa nchi nzima, kiasi hiki ni kidogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali lazima ijenge miundombinu ya kilimo, barabara, trekta nyingi za kutosha, vifaa vya umwagiliaji pia Serikali ihakikishe mbegu bora na mbolea ya kutosha inapatikana kwa wakati. Kwa upande wa Jimbo la Morogoro Kusini tunayo maeneo mazuri sana ya kilimo cha trekta na umwagiliaji mfano eneo la Kongwa, Kilengezi, Selembala, Magogoni, Lundi, Dutumi na Kisaki ni maeneo makubwa yanayolima mahindi, mpunga, ufuta, mihogo, viazi na kadhalika. Tunaomba Serikali ituwezeshe wakulima wetu wapate mikopo ya nyezo hizo za kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa upande wake itengeneze barabara za kwenda mashambani ili zipitike muda wote wananchi watalima sana. Taarifa ya Serikali kuwa zao la muhogo limepata soko China ni habari njema kwetu, tunaomba kufahamu utaratibu utakaotumika na chombo gani kinachosimamia hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeeleza dhamira yake ya kuifanya nchi ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda. Hivyo, nashauri Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi itengeneze mpango wa uzalishaji wa mazao yatakayoingia katika viwanda vitakavyojengwa nchini kuandaa upatikanaji wa raw materials za viwandani mfano miwa kwa viwanda vya sukari, matunda kwa viwanda vya juisi na vinywaji baridi na kadhalika. Mashamba ya mazao haya yatakuwa makubwa na ni vema kuanza kuandaliwa vinginevyo viwanda vyetu vitajengwa hakuna raw materials. Kwenye uzalishaji huu, matumizi ya sayansi na teknolojia uongezeke ili tupate mazao mengi ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, sekta ya uvuvi bado kuimarika tunahitaji mapato yaongezeke mara dufu. Nashauri tuingie ubia na makampuni ya nje yenye meli kubwa za uvuvi kwenye uvuvi wa bahari kuu badala ya utaratibu wa sasa wa kutoa leseni kwa makampuni hayo ya nje kutoka China, Hispania, Seychelles, Taiwan, Ufaransa na Mauritania. Serikali haipati mapato ya kutosha kwa utaratibu huu kuliko kama tungeingia nao ubia. Msumbiji wanafanya hivyo na wamekuwa na mapato mazuri. Wanayo matatizo mengi ya jinsi walivyotumia fedha zao kununulia meli za uvuvi lakini hiyo ni tofauti na mpango wa ubia ninaoushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.