Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu muumba mbingu na ardhi na vilivyomo. Nikushukuru wewe kwa nafasi hii uliyonipatia ili na mimi nichangie, ingawa kwa muhtasari, katika Wizara hii muhimu sana kwangu kwa sababu imenilea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizobarikiwa na rasilimali muhimu za bahari, maziwa na mito. Tanzania Bara tunao mwambao wa bahari wenye kilometa 750 ambapo Unguja na Pemba wanazo kilometa 675. Maeneo haya ni muhimu kwa Taifa letu kwa sababu yana samaki wengi wa kila aina pamoja na vivutio vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa masikitiko makubwa na ni bahati mbaya sana Serikali imeshindwa kudhibiti eneo hili na chanzo hiki cha utajiri. Eneo hili muhimu linakumbwa na changamoto mbalimbali ambazo zinarejesha nyuma na kuvunja moyo wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya changamoto zinazokabili eneo hili la utajiri wetu ni pamoja na wavuvi haramu; (wavuvi wanaotumia mabomu, wavuvi wanaotumia nyavu zenye matundu madogo na wengine wanatumia gesi). Changamoto zote nilizotaja hapo juu ni baadhi tu lakini zote ni hatari sana. Kwa mfano, uvuvi wa kutumia mabomu unaharibu mazingira vibaya sana, unaharibu mazalia ya samaki (matumbawe), mapengo ya mikoko pamoja na kuharibu maji ya bahari; wanaua samaki wengi wadogo wadogo pamoja na kuharibu mazalia mpaka mayai ya samaki, hakuna kinachobaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya nyavu zenye matundu madogo vile vile ni hatari kwa sababu hazibakishi zinavua mpaka samaki ambao hawafai hata kwa kula, hivyo inakaribiana na bomu, gesi pamoja na wanaotumia kemikali; athari zake zinafanana ingawa uvuvi wa kutumia kemikali na gesi ni hatari zaidi kwa sababu ni sumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niangazie kidogo katika wizi wa kimataifa katika Bahari Kuu kwa meli za kigeni. Pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali lakini bado tatizo hili lipo na ni hasara kwa Taifa. Meli za kigeni bado zinafanya magendo katika bahari yetu na kuangamiza uchumi wa nchi yetu. Wataalam wanasema uvuvi haramu unalikosesha Taifa letu kila mwaka asilimia 80 ya mapato ambayo yanapatikana katika sekta ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uvuvi huu haramu unawakosesha mapato wavuvi wadogo wadogo wapatao 40,000 ambao wanashindwa kupata samaki wa kutosha. Udhibiti wa Bahari Kuu bado ni dhaifu na ndiyo maana wahalifu wanaendelea na uhalifu kila siku ambao unatukosesha zaidi ya dola milioni 220 kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu tulipokamata Meli ya MFV TAWARIQ 2009 kuna meli gani nyingine ambayo imekamatwa? Takribani miaka saba (7) mpaka nane (8) hivi sasa. Je, Mheshimiwa Waziri hivi ndiyo tuseme hakuna meli zinazovua katika bahari yetu? Nishauri, ni lazima sasa Serikali iwekeze katika Bahari Kuu kwa maslahi ya Taifa na watu wake.