Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niunge mkono hoja ya baadhi ya wachangiaji waliotaka tuongeze tozo kwenye mafuta kwenye jambo hili la maji. Hata hivyo nisikitike sana wakati nasoma hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri, nimeona alichokifanya mwaka huu ni ku-copy na ku-paste tu kwenye Mradi wa Maji wa Makonde. Kile kilichoandikwa mwaka jana ndicho alichokiandika leo, na pesa zenyewe zinazozungumzwa ni pesa za kutoka kwenye Basket Fund.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tume-fail na jambo hili la Mradi wa Makonde na kumbuka mradi huu Mheshimiwa Waziri unahudumia Wilaya takribani nne, majimbo matano ya Newala, Tandahimba, Nanyamba, Newala Vijijini, ni mradi huu tunaozungumza. Mwaka jana mmeweka bajeti hii ya Euro milioni 87 ambazo mlisema mnakopa kutoka India, lakini mwaka huu mlichokiandika mwaka jana ndicho mlichokiandika mwaka huu. Watu wetu watatuamini vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana mwaka jana tumewaeleza Serikali imetenga dola bilioni 87 ambazo hazijatekeleza chochote kile. Mwaka huu tunarudi Majimboni mwezi wa saba tunakwenda kuwapa scenario ile ile ya mwaka wa jana, wanataka kutuamini nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Rais alivyokuja Jimboni kwangu Tandahimba miongoni mwa ahadi alizokuwa ameahidi ni pamoja na kuona kwamba Watanzania wanaondokana kabisa na tatizo la maji. Mheshimiwa Naibu Waziri umefika Tandahimba, vizuri sana, umeona unapofika mwezi wa sita, wa saba, ndoo moja ya maji mpaka shilingi 2,000 hii ni hatari sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri amefika Tandahimba, Tandahimba hakuna tatizo la vyanzo vya maji, Mto Ruvuma ni kilometa 15 tu kutoka Wilayani lakini kuna kata ambazo ni kilomita 8 tu kutoka Mto Ruvuma maji yamejaa. Ukienda kata za Mihambwe, Mchichira, Mahuta, Kitama pamoja na Tandahimba Mjini kote kuna vyanzo vya maji, lakini watu wake hawana maji. Ukiangalia hotuba yako hii vizuri, hii uliyoiandika, mijini mmetengenezea pesa za kwenda kule tena pesa za ndani. Mijini ambako matatizo ya maji si makubwa kama vijinini. Lakini kwenye mradi ule wa Makonde mmetenga shilingi bilioni moja. Tena fedha za nje hizo hizo kwa ajili ya miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi ule una zaidi ya miaka 30, miundombinu yake imechakaa, na Mheshimiwa Naibu Waziri unajua. Pesa zenyewe tunazotengea ni hizo hizo za nje. Sasa kuna u-serious kweli kwa watu wale wa Kusini, watu wale wa mradi wa Makonde kweli kupata maji? Sasa mje mtusaidie hapa, mnapopeleka maji mijini ambako at least asilimia 72 wana maji vijijini kule, mimi jimbo langu lina kata 31 katika majimbo makubwa kabisa, na umbali kutoka kata moja na nyingine ni umbali wa kilomita 15 kilometa 16, watu wana shida ya maji.

Mheshimiwa Mwneyekiti, mimi naomba tena ikiwezekana tunapomaliza bajeti Mheshimiwa Waziri uje mwenyewe uone kutoka Mkwiti kwenda Tandahimba watu hawana maji watatembea umbali gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kata za Luagalo, Chaume pamoja na Nambahu kuna shida ya maji; kila unakotembea Tandahimba kuna shida ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana mnapotengeneza bajeti hizi nadhani watu wa nishati walifikiria mpango mbadala wa nishati vijijini (REA), na ninyi watu wa maji sasa tuwe na jambo la mbadala la maji, vijijini kwa sababu ndiyo sehemu ambako kuna waathirika wakubwa wa tatizo la maji. Badala ya kukaa hapa tunazungumza vitu vingine suala la maji liwe priority kwa Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ni waombe tu walizungumza wazungumzaji hapa wakizungumza kwenye mafuta. Mimi niombe watu wanakunya bia kweli kweli; bia zinanyweka kweli kweli, tusitegemee chanzo kimoja tu cha mafuta kwenye kule tuweke shilingi shilingi mia, mia au shilingi mia mbili kule ili itusaidie mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niendee kusikitika sana; bajeti ya mwaka jana ambayo imetekelezwa kwa kiwango kidogo sana na bajeti hii ya mwaka huu ina utofauti mkubwa sana na mimi napata shida na sijui Waheshimiwa Wabunge wenzangu wanaposhauri hili jambo kwamba tuongeze bajeti; kama ya mwaka jana tulishindwa kuitimiza mwaka huu tukasema tuongeze, mimi nidhani bajeti hii iliyokuwepo sasa tuone vyanzo vyake vya pesa vinakamilika na tusitegemee vyanzo vya kutoka nje.

Haya tuliyoyaomba kwenye mafuta, kama alivyozungumza Mheshimiwa Mwenyekiti wakati alipotoa ufafanuzi mwanzo kuhusu suala la maji kwamba mtakapokaa kwenye kile kikao cha bajeti mtakapokuja hapa na majumuhisho basi tuone kwenye mafuta tumeongeza shilingi mia kwenye bia tumeongeza shilingi mia mbili. Tuongeze ongeze ili tatizo la maji Tanzania liwe limekwisha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri jana nilikutumia ki-note hapa kidogo, ki-memo nikiwa naomba ili tuwasaidie Wizara tulisaidie Taifa, sisi tumeomba Mamlaka ya Maji Tandahimba kwa vyanzo vya maji tulivyokuwa na mapato yetu haya ya korosho na ikitokea na Serikali ikakubali kutupa asilimia tano ya bei ya soko maana yake ni kwamba tunaweza tukaisaidia Serikali Tandahimba kukawa hakuna tatizo la maji. Sasa niombe tu barua zetu kwa sababu tumeshapeleka TAMISEMI kama ulivyoniambia kwamba nipeleke TAMISEMI, tulishapeleka na walitupa majibu kwamba wameshaleta dokezo kwenu; kwa hiyo tatizo liko kwenye Wizara yako; ukaangalie makabirasha yako vizuri. Kama Tandahimba tutapata Mamlaka ya Maji tukapokuja mwaka kesho kutwa hapa tutakuwa tunazungumza lugha nyingine nzuri kidogo kwenye jambo la maji. Vilevile niendelee kukuomba Mheshimiwa Waziri Tandahimba pale nishukuru sana ulitupa pesa ambazo zingeweza kusaidia kuweka mashine ya pump pale Tandahimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bahati mbaya nyingine kubwa mmetupa engineer wa maji wa Wilaya tuliyokuwa naye miaka zaidi ya tisa hakuna maji Tandahimba na mambo mengine ya ajabu sana tumewahi kumpa pesa mpaka za Halmashauri pale kuweza kujenga pump pale maji hayatoki. Watu wa utumishi walimpa transfer ya kumwondoa Tandahimba aende sehemu nyingine kwa sababu ana muda mrefu, lakini mmefanya lobbing mmerudisha tena pale, yaani maana yake mnamleta engineer ambaye mnajua hawezi kusimamia mambo ya maji, mnamuacha pale tuendelee kupata shida watu wa Tandahimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nakuambia Mheshimiwa Waziri kuwa engineer yule mliyemleta tukimaliza Bunge mkiendelea kumuacha pale na sisi hatuna maji tutamwondoa sisi kwa maandamano makubwa kabisa. Nazungumza kwenye Bunge hili, tutamwondoa kabisa kabisa. Haitawezekana anapewa pesa; kuna mradi wa maji amekuja Naibu Waziri wa TAMISEMI; Mheshimiwa Selemani Jafo, unazinduliwa mradi wa maji ambao inatoka hewa badala ya maji, na manasema mradi umekamilika. Mradi unakamilikaje ikiwa maji hakuna na mnauzindua na mnasema tumekabidhi mradi tayari na ikiwa mamiolioni ya fedha Watanzania mmelipa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, amekuja Mheshimiwa Selemani Jafo pale Mahuta, amezindua mradi ule wa maji wa Mkupete, umezinduliwa mradi hewa, watu wa Mkupete hawana maji, hata Mheshimiwa Waziri ukija mradi ule mmetumia mamilioni ya pesa maji hayatoki. Bado mnataka engineer yule tukae naye, anazindua miradi ambayo haina maji na viongozi mnakuja na mnasema mradi umezinduliwa, maji hakuna tunakaa na engineer kama yule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunahitaji engineer ambaye atatoa matokeo chanya ya maji. Hata ukatuletea profesa na ma-degree manne matano saba mkasema huyu ndiye professor wa maji na maji hatuyapati. Sisi wana Tandahimba tunasema huyu ni profesa uchwara tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji mtuletee mtu anayetupa maji na si kutuletea vyeti tu na vyeti vyenyewe ni vya hewa na tunaona balaa lake hili. Kwa hiyo, tunahitaji mtu mwenye capacity ya kule maji. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kule kwetu uje, ile sehemu imekuwa ni sehemu ya mwisho kwenye kila jambo. Barabara mwaka jana mmeona walivyotufanyia, wametenga kilometa 50 mpaka leo tunapozungumza tunapozungumza ni story. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa isiwe watu wa Kusini ni watu wa story tu, tumeshateseka kwa muda mrefu kusini tulishasahauliwa muda mrefu, kwa hiyo kwenye priority ya mambo haya, mnaposema maji tengeni maji pelekeni Kusini ili na sisi tujione ni Watanzania na tuna haki sawa na Watanzania wengine badala ya kutupa miradi tunarudi majimboni tunaisifia Serikali, maana unavyoleta kabrasha hili ninapokwenda mimi ninawasomea wananchi pale. Nasema safari hii bwana Serikali imetenga dola bilioni 87 saba kwa ajili ya maji, watu wanashangilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na bahati mbaya Makamu wa Rais alikuja Tandahimba mwaka wa jana akawahakikishia watu wa Tandahimba kwamba tumepata pesa mtapata maji, maji hakuna. Haya mnayoyafanya ndiyo kaburi la Chama cha Mapinduzi maka 2020 haya. Haya mnayoyafanya haya msije mkaleta mabomu, watu hawana maji hawawezi kuchagua CCM wakati haitekelezi mahitaji yake, hawawezi, msije mkatafuta labda akina Nape wanasema hivi sijui
…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)