Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kupata nafasi na mimi ya kuweza kuchangia Wizara hii ya Maji. Kwa kuwa dakika chache lakini Wizara hii nyeti naomba niende moja kwa moja kwenye kitabu cha Waziri na bahati nzuri mimi nina vitabu viwili vyote, cha mwaka jana na kitabu cha mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa Ntomoko ambao niliusemea pia katika Ofisi ya Waziri Mkuu. Mradi huu wa Ntomoko unabadilishwa tu maneno kwenye vitabu vya Mheshimiwa Waziri. Kitabu cha mwaka wa jana alituletea mradi wa Ntomoko kwamba unahusisha Halmashauri mbili za Wilaya ya Chemba na Wilaya ya Kondoa. Kitabu cha mwaka huu hali ya huduma ya maji kutoka chanzo cha Ntomoko imeshindwa kukidhi mahitaji na kupunguza vijiji, yaani tunabadilishiwa maneno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mradi huu Mheshimiwa Waziri unalifahamu vizuri. Mradi wa Ntomoko ni disaster, haiwezekaniki. Leo mnakuja kutuandikia hapa ilhali mnajua kabisa nini kinachoendelea kuhusiana na suala zima la Ntomoko. Mheshimiwa Waziri, suala hili kama mnashindwa kuwawajibisha watu ambao wameweza kutenda dhambi kwa Watanzania wenzao kwa kupoteza fedha nyingi shilingi bilioni 2.4 wamezilamba, maji hakuna, wananchi wanapata shida ya maji, mna kazi ya kutubadilishia maneno kwenye vitabu, hatuwatendei haki wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hela zile si hela ambazo watu wale wanaomba, fedha ile wananchi wa Wilaya ya Chemba na wao ni miongoni mwa Watanzania wanaolipa kodi, wanatakiwa wapate hii huduma muhimu ya maji. Wilaya ile ina shida ya maji haijapatikana kuona. Kituo cha Afya cha Hamai hakina maji, nilisema, mwaka jana niliwaambia Wizara, mnaendelea kutubadilishia maneno kwenye hivi vitabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja, naomba aniambie suala la Ntomoko hatma yake ni nini? Wananchi wa Chemba tumesema huu mradi hatuutaki kaeni nao ninyi, tutafutieni mradi mwingine ambao tutapata maji. Hamuwezi kuwa mnaendelea kutubadilishia vijiji vyote, kata zote 26 hakuna maji. Mlitupa hivyo vijiji kumi navyo vimekuwa shida hakuna maji, mnataka nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya maeneo ambayo mnaendelea kufadhiliwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni miongoni mwa Mkoa wa Dodoma ndimo mnamopata kura humu, lakini bado hata hamuwakumbuki watu hawa, kwa nini mnafanya namna hiyo? Waswahili akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli. Sasa kama rafiki huyu mnamuona hana maana atakapokuja kupata rafiki mwingine msije mkamlaumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la maji DUWASA. Sijaona kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri kikiniambia kwamba kutokana na ujio wa Makao Makuu kuhamia Manispaa ya Dodoma ambayo ndiyo itakayobeba watu wengi, sijaona mpango mkakati wa upatikanaji wa maji katika Mji wa Dodoma. Tuna kata 41 katika Manispaa ya Dodoma, ni kata 18 tu ndizo zina maji; na katika hizo kata 18 haizidi mitaa 50 ambayo inapata maji katika hizo kata 18. Sasa tuna huu ujio, Mheshimiwa Waziri hujatuambia nini mkakati wa Serikali kuhakikisha maji yatapatikana pamoja na ongezeko kubwa la watu linalokuja kuingia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, DUWASA hii ina majanga ya madeni kwenye taasisi za Serikali, na naomba nizitaje na utakapokuja hapa Mheshimiwa Waziri naomba uniambie madeni haya yatalipwa lini na taasisi za Serikali. Inakuwa ni aibu na ni masikitiko makubwa sana mwananchi wa kawaida anakatiwa maji, hapati maji mpaka alipe bili ya maji, taasisi za Serikali hamtaki kulipa maji mnadaiwa mabilioni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, DUWASA inadai shilingi bilioni 1.9; kati ya hizo Jeshi la Polisi linadaiwa shilingi milioni 600, Magereza shilingi milioni 200; JWTZ inadaiwa shilingi milioni 100, JKT shilingi milioni 500, Makamu wa Rais… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzunguzaji)