Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, hatimaye nikushukuru wewe kwa kuniona na kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawapongeza sana Mawaziri wa Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Sambamba na hilo, naomba niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya. Kikubwa zaidi, niipongeze Serikali kwa kipaumbele ambacho imeweka kwenye Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, naomba niwape pole Watanzania wote kwa matatizo ambayo yametokea nchini kwetu na siyo matatizo mengine bali ni matatizo haya ya mvua ambayo ipo kila kona na yameweza kuathiri maisha ya wananchi wa Tanzania. Vile vile nirudie kutoa pole kwa watoto wetu ambao wamepoteza maisha wakati wakiwa kwenye harakati zao za masomo wakielekea huko kwa ajili ya kufanya mitihani ya kujipima wao wenyewe. Mwenyezi Mungu awalaze mahali pema peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai, maji ni utu, maji huleta heshima na ustawi kwenye familia; lakini siyo familia pekee, bali na jamii kwa ujumla. Kwa mantiki hiyo, tunaamini kwamba Tanzania ina changamoto kwenye eneo hili la maji. Kila mtu kwa njia moja au nyingine anaguswa na changamoto hii ya maji, iwe ni wa mjini iwe ni wa kijijini anaguswa na changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa zaidi changamoto hii inamgusa mwanamke, kwa sababu mwanamke ndiye mtafutaji wa maji katika familia. Kama nyumbani hakuna maji, mwanamke hawezi kukaa kitako; lazima atoke sehemu moja hadi nyingine kuhakikisha kwamba amepata maji ili maisha yaendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mantiki hiyo, tunaiomba Wizara ya Maji iongeze hiki kiwango, lakini kama siyo kuongeza, tuangalie vyanzo vingine ambavyo vitatusaidia kuongeza hii bajeti yetu ya maji. Kama Waheshimiwa Wabunge wengine waliotangulia walivyosema, tuchukue ile tozo ya sh.50/= tuongeze kwenye maji hatimaye tuwe na sh.100/=. Tukiweka sh.100/= itatusaidia kuongeza bajeti yetu. Kwa mantiki hiyo basi, ile bajeti ya mwaka 2016 ndiyo irejee na kuwa bajeti ya mwaka huu kwa taratibu zake zinazohusika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naelekea kwenye Jimbo letu la Lindi Mjini. Tatizo la maji kwenye Jimbo la Lindi Mjini ni kubwa, tena sana. Lindi Mjini hakuna maji, Lindi Mjini hali ni tete. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikuja Lindi na akasema ifikapo tarehe 3 Julai, lazima tuhakikishe kwamba maji yamepatikana. Serikali mtuambie, je, maji yatapatikana au hayatapatikana? Tunasubiri kauli ya Serikali ili mwanamke huyu tumtue mzigo.

Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Naomba mengine niyaandike kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.