Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa dakika ni chache sana, nami nichukue fursa hii kuwatakia pole Watanzania wote ambao wamekubwa na majanga mbalimbali hususan ya watoto wetu kule Arusha; lakini pia Watanzania wote kule Rufiji ambao wamekumbwa na matatizo mbalimbali ya ujambazi ambayo niseme tu kwa hali ya kawaida, tatizo hilo la ujambazi limeacha wajane wengi na watoto wengi yatima. Naliomba Bunge lako wakati mwingine tunapochangia kwenye mambo ya sherehe, basi mnikumbuke kule Rufiji, mnifikirie kwani nina wajane wengi na watoto yatima wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kutoa pole kwa wale wote waliokumbwa na mafuriko makubwa kule Rufiji hususan Kata yangu hii ya Mohoro, kwa kina Chii kule mpaka kwa mzee Mikindo, Kata ya Mwasemi, Kipugila, Ikwiriri, Umwe, Mgomba, Ngarambe pamoja na Chemchem.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe watu wa Rufiji msemo mmoja katika Quran unaosema kwamba kullama yuswiibana, illamaa qataba Allah lana, ikimaanisha kwamba nothing will happen to us, except what Allah has decreed for us. Hakuna linaloweza kutokea mpaka pale ambapo Mwenyezi Mungu amelipanga litokee baina yetu. Mwenyezi Mungu ametuandikia kila jambo litakalotokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niendelee kuwatia moyo wananchi wangu wa Rufiji wasibabaike na jambo linaloendelea na hili ni tatizo la amani, waendelee kuijenga nchi yao, kwani Tanzania hii ni ya kwetu sote nasi tutaendelea kuwapigania huku katika Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini pia wale ambao wamesoma vitabu mbalimbali watakumbuka kitabu cha “Comperative Government and Politics,” watatambua ni namna gani Mheshimiwa Rais ataweza kulisaidia Taifa hili hapo mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nampongeza sana na tuseme tu kwamba nchi hii inamhitaji sana. Mabadiliko makubwa katika nchi kama Bangladesh ambao wameweza kubadilika kwa kipindi cha miaka 10, tunaamini kabisa kwamba Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli anaweza kuivusha Tanzania kutoka hapa ilipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mengi ya kuzungumza, lakini niseme kwa uchache tu kwamba suala hili la maji limezungumzwa katika Ilani yetu ya Uchaguzi. Ukiangalia Ilani yetu ya Uchaguzi; Serikali imeundwa na Chama cha Mapinduzi na utekelezaji ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Pia tunaongozwa na Kanuni za Uongozi wa Chama cha Mapinduzi. Kwa mujibu wa Ilani, katika ukurasa wa nne wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi, inasisitiza Serikali kufanya yale yote yanayoletwa ndani ya Serikali kwani ni yale ambayo yanaongozwa na Ilani.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 66 wa Ilani yetu ya Uchaguzi inasisitiza katika kusogeza huduma za kijamii karibu na kwa wananchi. Suala la maji safi na salama limezungumzwa katika ukurasa wa 83 wa Ilani, nami nataka nijikite katika ukurasa wa 85 wa Ilani yetu ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ambayo imedhamiria kutua ndoo kichwani kwa mwanamke. Niseme tu kwamba kwa mujibu wa ukurasa 85, Ilani imedhamiria kuongeza asilimia 53 ya maji vijijini mpaka kufikia asilimia 70. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme, kule kwangu Rufiji niliwahi kufanya ziara katika kijiji kimoja pale Kikobo. Wananchi wa Kikobo wamehama kijiji kile kwa sababu ya tatizo la maji na walichonieleza ni kwamba kule Dar es Salaam ukiwa na pesa kidogo unaonekana unatoka kipara kichwani, lakini akinamama wa eneo la Kikobo wanatoka vipara kwa sababu ya kubeba ndoo kwa muda mrefu. Wanasafiri na maji kwa zaidi ya kilometa saba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tatizo hili ni kubwa sana kwa nchi yetu, nami niseme tu kwamba sisi tulishaanza utekelezaji wa Ilani. Mimi binafsi nilishaanza uchimbaji wa visima mbalimbali katika eneo langu, yale maeneo korofi kabisa!

Mheshimiwa Naibu Spika, nimechimba visima katika Kata ya Mgomba Kusini, Mgomba Kati, Ikwiriri Kati, Nambanje, Mpalange, Mtanange tunakwenda kuchimba pamoja na Mpima; lakini pia Mpalange kwa Njiwa kote tunakwenda kupeleka visima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako maeneo korofi ambayo tunaamini kabisa Serikali ikiweza kutusaidia, tutaweza kutatua kero ya maji. Hapa nazungumzia katika Kata ya Chumbi, hususan katika Kijiji cha Nyakipande, pamoja na Miangalaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dhati kabisa, napenda niwapongeze watani wangu hawa wawili kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja pamoja na marekebisho yatakayofanywa na Wizara. Ahsante.