Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba niendelee kama walipoanzia wenzangu kupongeza juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali yetu katika kuhakikisha kwamba matatizo ya maji Chalinze yanafikia mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliwahi kupata nafasi ya kukutana na Mheshimiwa Rais, tukazungumza naye na kumweleza juu ya tatizo kubwa wanalopata wananchi wangu wa Jimbo la Chalinze. Alimwagiza Waziri Mkuu na Waziri Mkuu alikuja, alipofika katika kile chanzo chetu cha Wami, aliyoyaona, mwenyewe anayajua. Mheshimiwa Waziri alikuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu ninaposimama leo hii, nataka nimkumbushe tu Mheshimiwa Waziri kwamba katika kipindi kile ambacho tulimpa yule Mkandarasi pale, sasa zimebaki wiki mbili na nusu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anasimama, napendelea wananchi wa Chalinze wamsikie, anasemaje juu ya yule Mkandarasi na Wizara inajipangaje sasa kutoa maelekezo mapya baada ya kuonekana kwamba kazi ile inasua sua?

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo pia naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri jambo. Kwenye suala la maji katika Jimbo la Chalinze anajua kwamba, kuna viwanda ambavyo vinaendelea kujengwa sasa, lakini viwanda vile vinaweza kupata matatizo ya kuanza kutokana na kukosekana kwa maji. Mimi kama Mbunge nilifanya initiative za kuzungumza na wawekezaji wenzetu wa Trifod na Bwana Shubash Patel wakakubali kutoa vifaa kwa ajili ya kusaidiana na CHALIWASA chini ya Engineer wetu Christa Msomba ili kuhakikisha kwamba pale kwenye chanzo chetu wakati ninyi Serikali mnajipanga, wao wawekezaji wako tayari kuja kusaidia kuweka miundombinu vizuri. Inaonekana kwa upande wa ma-engineer au Wizarani kumekuwa na utata kidogo katika kutoa ruhusa ya wao kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, uko msemo kule kwetu Pwani wanasema, “anapokuja mgeni, basi mwenyeji ndio anapata nafuu au anapona.” Hawa wawekezaji wanataka kumsaidia kazi ya kuweza kujenga chanzo pale, wakati yeye yuko Bungeni hapa anaomba pesa kwa ajili ya kuweza kujenga miundombinu. Namwomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili kwa jicho la karibu sana. Wananchi wa Chalinze hawahitaji siasa, wanataka maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, liko jambo la mabwawa. Wananchi wa Chalinze wameahidiwa mabwawa hasa wale wanaotoka katika Kata ya Kibindu. Kuna bwawa tuliahidiwa na Mheshimiwa Waziri Profesa Maghembe kwamba atatujengea bwawa kubwa na wananchi wa Kibindu wataondoka katika taabu kubwa ya maji wanayoikabili. Kule Mjembe walitoa eneo pamoja na wananchi wa Gole, lakini mpaka leo ninapozungumza Mheshimiwa Waziri, hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kitabu cha hotuba ya bajeti hapa, nayo ameelekeza kwamba atajenga mabwawa mengi, lakini cha kusikitisha zaidi bwawa lile la Mjembe Gole limepotea hewani, silioni humu ndani na sijui tunaelekea wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uzuri Mheshimiwa Maghembe yuko humu ndani, kwa hiyo, akimwuliza anaweza kumthibitisha hilo na akampa maelekezo ni jinsi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, nitoe ushauri pia katika eneo la mabwawa. Tunaona maji mengi sana yanayopotea, tunaona maji mengi sana ambayo yanaingia baharini ambayo sisi kama Taifa tumeshindwa kuyatumia kwa ajili ya manufaa ya walio wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie Mheshimiwa Waziri, nimeona humu ndani ametenga fedha kwa ajili ya Bwawa la Kidunda, lakini tunatambua aliwahi kusema mzee wetu mstaafu Alhaj Ali Hassani Mwinyi, Rais wetu aliyemaliza muda wake, kwamba kupanga ni kuchagua. Natambua kwamba katika bajeti hii hajapanga lolote kuhusiana na ujenzi wa mabwawa zaidi ya lile la Kidunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe tu Mheshimiwa Waziri, yale maji yanayopita pale Ruvu kwenye Kituo chetu kinachozalisha maji kwa ajili ya wanywaji wa Dar es Salaam, yanakwenda yanamwagika baharini; nimeshuhudia juzi nikiwa kwenye ndege wakati nakuja Dodoma, maji mengi yametapakaa katika bonde lile, hata wananchi wa Bagamoyo wanashindwa kwenda mashambani. Jawabu lake ni kutengeneza bwawa lingine ambalo linaweza likazalisha maji mengi na likapeleka maji hata katika maeneo ya Miji kama ya Pangani hata kule Tanga Mjini ambapo wajomba zangu nao wanalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile niongee juu ya jambo kubwa la kukatika kwa umeme. Wengi wameyasilimulia hayo, lakini nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri, ndani ya Halmashauri ya Chalinze, CHALIWASA wananchi wanalipia maji, isipokuwa kuna tatizo kwa upande wa Serikali kupe...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.