Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja iliyo mbele yetu ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani hizi, naomba nijielekeze kuchangia. Kwanza, pongezi na shukrani kwa Mheshimwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli. Naomba nianze kwa kumshukuru sana na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa mambo yafuatayo:-
(i) Kwa jinsi alivyounda Wizara hizi nyeti mbili na kuzifanya ziwe chini ya usimamizi wa Ofisi yake na jinsi alivyowateua Mawaziri na Naibu Waziri wenye weledi wa hali ya juu na wenye uchapakazi pia, Mheshimiwa Angellah Kairuki, Mheshimiwa Simbachawene na Mheshimiwa Suleiman Jafo.
(ii) Kwa jinsi alivyoanza kazi na kuhakikisha watumishi wa umma wanakuwa na nidhamu ya kazi, wanakuwa waadilifu na wenye uwajibikaji wa hali ya juu ndani ya Serikali aliyoiunda. Lengo likiwa ni kuleta tija kwa Watanzania wote bila kuleta itikadi za dini, vyama, kabila wala jinsia zao na kuleta maendeleo ya hali ya juu ndani ya muda mfupi na mabadiliko yanaonekana.
(iii) Kwa kubana matumizi katika uendeshaji wa shughuli za Serikali na kutoa zaidi vipaumbele katika miradi ya kuinua uchumi wa nchi.
(iv) Kwa jinsi alivyolipa kipaumbele suala zima la watumishi hewa kwani ameweza kuokoa fedha nyingi ambazo zilikuwa zinapotea bure na kwenda kwa watu wasiohusika wala kuzifanyia kazi. Badala yake fedha hizi hivi sasa zinakwenda kuendeleza miradi mbalimbali hasa kwa wananchi waishio katika kaya maskini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi anayoifanya Mheshimiwa Rais na timu yake ndani ya Serikali imeleta matunda mazuri ndani ya nchi yetu katika muda mfupi kiasi kwamba wale Watanzania ambao hawakumpigia kura wanasikitika sana. Watanzania sasa wanasema itakapofika 2020 hawatafanya makosa tena na CCM kwa nafasi ya Rais, Wabunge na Madiwani watashinda kwa 100%.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, naomba nitoe ushauri katika maeneo machache niliyoyachagua, kwanza, ni uchangiaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Wanawake na Vijana (10%). Pamoja na dhamira njema ya Serikali ya kuzielekeza Mamlaka ya Serikali za Mtaa kutenga 10% kwa ajili ya kusaidia vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana lipo tatizo kubwa la fedha za Mfuko huu kutopelekwa kwa vikundi vya wanawake na vijana kama ilivyokusudiwa kwa sababu halmashauri zilizo nyingi hazitengi kabisa fedha hizi na zinazotenga zinatenga kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa jambo hili linaonekana kama jambo la hiari katika mamlaka husika, napenda kujua, je, utaratibu huu wa kutenga 10% kwa vijana na wanawake upo kwa mujibu wa sheria? Kama ni kwa mujibu wa sheria, je, ni kwa nini halmashauri hazitengi fedha hizi? Je, ni hatua gani zinazochukuliwa dhidi ya watu wasiotenga fedha hizi? Kama utaratibu wa kutenga 10% ya Mfuko wa Vijana na Wanawake hauko kwa mujibu wa sheria, je, ni lini Serikali italeta Muswada huu hapa Bungeni ili tuweze kutunga sheria hiyo itakayowabana wale wote wasiotenga na kufikisha fedha hizo katika vikundi husika?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ucheleweshaji wa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Utaratibu wa fedha za miradi ya maendeleo katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa zimekuwa ni changamoto kubwa kwani hazitolewi kwa wakati, zinazotolewa ni kidogo na hazitoshelezi kukamilisha miradi na uwiano wa kutoa fedha hizi hauzingatiwi kwani halmashauri zingine zinapata nyingi na zingine kidogo au hakuna kabisa. Napenda Waziri atuambie hapa tatizo ni nini na Serikali ya Awamu ya Tano ina mkakati gani wa kukabiliana na changamoto hizi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, upungufu wa wafanyakazi katika mamlaka mbalimbali za Serikali. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kupeleka watumishi wa kada mbalimbali katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, bado lipo tatizo kubwa sana la watumishi katika Halmashauri za Mitaa na hasa Walimu wa sayansi katika shule za sekondari; Madaktari na Wauguzi katika Hospitali za Wilaya, Vituo vya Afya na Zahanati; Maafisa Ugani wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi; na Wakuu wa Idara katika halmashauri nyingi ni wale wanaokaimu. Mheshimiwa Waziri atakapokuwa akihitimisha hoja yake naomba atoe maelezo Serikali imejipangaje kuhakikisha inapeleka wafanyakazi hao katika mamlaka mbalimbali za Serikali ili utendaji wao uweze kuleta tija kwa wananchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, nne, maslahi ya wafanyakazi. Pamoja na jitihada zinazoendelea kufanywa na Serikali za kuboresha maslahi ya wafanyakazi bado kuna wafanyakazi wa umma na sekta binafsi wana matatizo ya mikataba; kupata mishahara midogo ya kima cha chini sana; kukosa posho zao za kujikimu au kutopatiwa kwa wakati na makazi yao ni duni sana hasa wale waishio vijijini. Naiomba sana Serikali pamoja na vipaumbele ilivyojiwekea waangalie maslahi ya wafanyakazi hasa Walimu, Wauguzi, Maaskari na wafanyakazi wa halmashauri mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, uimarishaji wa Serikali za Mitaa. Serikali za Mitaa ndiyo sekta pekee inayotoa huduma kwa wananchi siku hadi siku kwa ukaribu zaidi. Ili kuboresha sekta hii nashauri:-
(a) Serikali ithubutu na kufanya uwekezaji ili Mamlaka ya Serikali za Mtaa ziwe na vyanzo vyake vya mapato vya kutosha na kutoa mchango wake katika pato la Taifa;
(b) Mamlaka za Serikali za Mitaa zielekezwe kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuachana na kufanya kazi kwa mazoea, wawe wabunifu ili waongeze wigo wa ukusanyaji wa mapato; na
(c) Serikali za Mitaa kuna upotevu wa fedha kwa matumizi yasiyo na tija na kutozingatia matumizi ya fedha. Kwa hiyo, Serikali lazima ihakikishe kuwa kanuni za fedha zinafuatwa na fedha zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa hasa katika kuleta maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niunge mkono hoja na ahsante sana.