Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kuboresha miundombinu na upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na umuhimu wa maji, changamoto kubwa ya utekelezaji wa bajeti ya maji ni ufinyu wa mapato uliopelekea Wizara kupokea asilimia 19. 8 tu ya fedha zote za bajeti ya maendeleo zilizoidhinishwa na Bunge kufikia Machi 2017 kwa mwaka 2016/2017. Changamoto nyingine ambayo ni sugu ni fedha za miradi ya maji kutumika vibaya kutokana na kutokuwepo na usimamizi wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, miradi karibu yote ya kuanzia mwaka 2013/ 2014 ya shilingi bilioni 6.2 ambayo pesa imelipwa zaidi ya nusu miradi hiyo mpaka sasa haifanyi kazi. Kati ya miradi hiyo, ripoti ya CAG inaonesha kuwa malipo yalifanyika bila ukaguzi na kwa kazi ambazo hazikufanyika. Mradi wa Swaya/Lupeta zimelipwa shilingi milioni 120 kati ya shilingi milioni 520 na kazi iliyofanyika haizidi shilingi milioni 50. Pia mradi wa Mbawi na Jojo wa shilingi milioni 804, zimelipwa karibu asilimia 100 lakini mradi haufanyi kazi. Pia mradi wa Horongo/Itimu/Mwampalala zimelipwa shilingi bilioni 1.2 (100%) na uko chini ya kiwango na malipo yalifanyika bila kuzingatia utaratibu wa malipo ya Serikali ikiwemo kutofanyika kwa ukaguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukosekana kwa usimamizi wa miradi ya maji, fedha za miradi ya maji zinatumika vibaya na wananchi wanaendelea kukosa huduma ya maji salama. Pamoja na miradi hiyo kutofanya kazi, ripoti za Wizara ya Maji zinapotoshwa kuonyesha kuwa miradi iliyotajwa hapo juu na mingine ambayo wala haijaanza imekamilika wakati wananchi walengwa katika vijiji hivyo hawana maji. Ripoti hizo za kupotosha zimepelekea kwa makusudi hata majibu ya swali la maji katika Mji Mdogo wa Mbalizi kujibiwa kwa kupotosha kuonyesha hakuna uhaba wa maji na pia kuonyesha vyanzo vya maji ambavyo havipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi kupitia Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya wameniagiza kumwomba Waziri wa Maji atembelee hiyo miradi aliyodanganywa na pia Bunge lielezwe hao wahusika wa upotevu wa fedha za miradi iliyotajwa ni hatua gani zimechukuliwa kwani hadi leo hii miradi iliyotajwa hapo juu haifanyi kazi. Kutokana na changamoto za usimamizi usioridhisha, naunga mkono mapendekezo ya kuanzishwa kwa Wakala wa Maji Vijijini (Rural Water Agency). Kuanzishwa kwa Wakala huyu kutaongeza tija ya bajeti ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na mapendekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji ya kuongeza tozo ya mafuta kwa kila lita ya dizeli na petroli kutoka Sh.50/= ya sasa kufikia Sh.100/=. Ripoti ya EWURA ya mwaka 2015 inaonyesha lita 3,380,097,164 ziliingizwa nchini na kwa tozo ya Sh.100/= kwa lita, mfuko ungekusanya shilingi bilioni 338. Hili ongezeko la tozo ni muhimu kutekelezwa haraka iwezekanavyo ili kunusuru hali ya maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ina vyanzo vingi vya maji ya mserereko. Pamoja na kuwepo vyanzo vingi, zaidi ya asilimia 60 ya wananchi hawana maji salama. Kuna Vijiji vichache kama vya Ngole, Iwala, Idugumbi na Chombe, wananchi wamejihamasisha na kuanzisha miradi ya kujitolea. Vijiji vya Mjete ni eneo la ukame na hakuna maji kabisa. Pia kuna vijiji zaidi ya 100 pamoja na kuwepo vyanzo vizuri vya maji ya mserereko lakini hawana maji salama. Wizara iangalie namna ya kupeleka miradi ya maji katika vijiji hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.