Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuzungumzia machache kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, napenda nitoe pongezi kubwa sana kwa niaba ya Wabunge wenzangu kwa Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa nchi hii kwa kura nyingi za kishindo, mimi nampa hongera sana na Wabunge wenzangu wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu niseme maneno yafuatayo kwa niaba ya Wabunge wenzangu kwa Chama changu cha Mapinduzi. Nakipongeza Chama cha Mapinduzi kwa kupata Wabunge 264 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Haikuwa kazi ndogo, ilikuwa kazi kubwa kweli kweli, lakini ukweli umebaki ukwel, keki ya Bunge imeichukua Chama cha Mapinduzi imewaachia robo. Nakishukuru sana Chama cha Mapinduzi kamati zote za kampeni zilifanya kazi nzuri. (Makofi)
Naomba sasa nichukue fursa ya kipekee kuwashukuru wanawake wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kunichagua mimi nije niwawakilishe katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nawaahidi wanawake wa Dar es Salaam nitawafanyia kazi na sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nirudi kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais alitoa ahadi zake kwamba atakapopata Urais ataunda Baraza dogo la Mawaziri. Hili amelitimiza na ameunda Baraza la Mawaziri lenye Mawaziri 19 tu. Mheshimiwa Rais nampongeza kwa hilo. Pia ametuleta Mawaziri mahiri, wachapakazi ambao tuna imani nao kabisa wataivusha Serikali hii kutoka pale ilipo kuipeleka mbele na kukipatia ushindi au mwenendo mzuri Chama cha Mapinduzi na tuonyeshe kwamba sasa tunataka kutengeneza CCM yenye mabadiliko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la TBC. Kumekuwa na maneno mengi sana kuhusu TBC. Mheshimiwa Waziri ameeleza vizuri sana nini tatizo lakini bado maneno yanazungumzwa. Naomba niliambie Bunge mimi Dar es Salam nina tatizo kubwa la mfumuko wa bei ya vyakula. Wananchi wanahangaika, mchele unanunuliwa shilingi 2,500/= mpaka shilingi 2,800/=. Kama kweli kuna hali kama hiyo mtu mwenye njaa anaweza akangalia TV?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali hili suala la TBC tuliangalie kama alivyozungumza Mheshimiwa Waziri kwamba yako matatizo. Kwa hiyo, haya matatizo ni jukumu letu sisi kama Wabunge kukaa chini na kuyatafakari. Hata hivyo, kuna umuhimu gani wa mimi kuonekana sasa hivi wakati sitafanya chochote Jimboni? Hivi kuongea kwangu kunawasaidia nini? Mimi naomba Serikali inisaidie kupunguza mfumuko wa bei jijini Dar es Salaam, vyakula vimekuwa bei juu sana, hilo mimi kwangu ndiyo naona changamoto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuchukua zile fedha zote za sherehe ya Uhuru kuja kutujengea barabara ya Kawawa. Kwanza nasema kwa niaba ya Wabunge wale wa Majimbo waliopelekewa zile hela, Jimbo la Ubungo, Kinondoni pamoja na Kawe ambapo barabara ile ndipo ilipo, napenda nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutuletea zile fedha kuondoa msongamano wa magari barabarani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba wananchi wa Dar es Salaam tunapotaka kufanya maamuzi tuhakikishe tunafanya maamuzi ya kweli kupata watu wa kututetea. Sisi kama Mkoa wa Dar es Salaam, Mheshimiwa Rais katupa hizo fedha ili barabara zetu zitengenezwe leo Mbunge wa Dar es Salaam unatoka nje wakati wa kuchangia hotuba ya Rais, hivi wewe ni kiongozi wa wananchi walio wengi au wa walio wachache?
Mimi naomba tuangalie sana nini tunakuja kuwafanyia wananchi ndani ya Bunge hili, tunakuja kuwasemea wananchi wetu tulete maendeleo. Leo mimi ningezungumza na mwenzangu wa Kawe, Ubungo nafikiri Mheshimiwa Rais angepata salamu zetu naye angeharakisha mradi huo. Nawaomba wananchi, CCM sasa ina mabadiliko na sisi tumejifunza, Wabunge tunakuja tukiwa wakali kwa lengo la kuwatetea wananchi wetu. Sasa kazi imeanza na tutafanya hivyo, hatukubali tena. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais, ukurasa wa 15, amesema tutajenga viwanda ili kukuza uchumi lakini pia kuleta ajira kwa vijana. Nimuombe Mheshimiwa Rais pamoja na yote tuangalie viwanda vilivyokufa na vinavyosuasua pia. Kuna viwanda vingi Dar es Salaam kama Aluminium Africa, Metal box, Bora Shoes, National Battery, Tanzania Cables, Mbagala Sheet Glass, Tanita Mbagala, National Milling, Tangold Africa, Urafiki-Ubungo, UFI-Ubungo, hivyo vyote ni viwanda ambavyo miaka hamsini iliyopita vilikuwa vikifanya kazi na leo vingine vimegeuzwa maghala.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Kiwanda cha TANITA Mbagala kilikuwa kinawapatia ajira kina mama. Kiwanda cha Tanita ni cha korosho kilikuwa kinabeba akina mama leo kiwanda kile kimegeuzwa ghala sijui watu wanahifadhi madudu gani, takataka tupu mle ndani, hivi kweli tutafika kwa hali hii? Niiombe Serikali katika hii sera yetu ya kutaka kuvumbua viwanda hivi tuyaangalie na maeneo hayo ili wananchi na vijana wetu waweze kupata ajira.
Naomba sasa nizungumzie suala zima la elimu. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kusema kwamba elimu itatolewa bure kwa ngazi ya shule ya msingi na sekondari. Ninao mfano wa wazi kabisa katika Kata ya Charambe - Mbagala wameandikisha watoto 6,000 wa darasa la kwanza. Hii inaonyesha wazi kwamba kumbe watoto wengi walikuwa wako majumbani wanashindwa kupata kile kiasi cha fedha cha kuingilia shuleni. Kwa hiyo, nampongeza kabisa Mheshimiwa Rais kwa hili wazo lake ambalo amelitekeleza. Pia ziko changamoto kwenye hayo makundi au mchanganuo wa fedha zile na hasa katika fedha za utawala, naomba fungu kidogo liongezwe pale kwa sababu ya walinzi. Pia changamoto ndogo ndogo zinazowakuta walimu hata kupata sukari kilo moja kwa siku angalau na wao wanywe chai kwa asubuhi tu. Niombe sana Serikali hilo nalo liangaliwe. Awamu ya Rais Mkapa ilikuwa zinakuja fedha za capitation kama hizi kulikuwa na fungu la utawala.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie Watanzania hizi fedha zitategemea sana utendaji wa Mwalimu Mkuu. Mwalimu Mkuu aliye bora akizisimamia vizuri fedha hizi kwa kweli mambo yatakwenda vizuri. Maana naona yako matatizo yanaletewa Serikali kumbe ni ya ubinafsi wa mtu, amepelekewa fedha ameshindwa kuzitumia vile inavyotakiwa matokeo wazazi wanaleta maneno. Mimi ni mwalimu pia niwaombe walimu wenzangu waunge mkono hizi jitihada za Rais kwa kutumia mafungu hayo vizuri kama vile walivyoagizwa na siyo vinginevyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nichangie upande wa nishati. Hotuba ya Mheshimiwa Rais, ukurasa wa 6, imeeleza itaboresha na itaondoa kabisa matatizo ya kukatikakatika kwa umeme. Naona juhudi kubwa ya Mheshimiwa na nampongeza sana na mfano na sababu ya kumpongeza ninazo. Juzi nimepigiwa simu na watu wa Kigamboni eneo la Ungindoni wanasema haijawahi kutokea, wameomba umeme lakini wameletewa mita majumbani bila ya wenyewe kuwepo. Mita zimepelekwa, wenyewe hawajui, wamepewa namba za simu, mita wameikuta iko nyumbani jambo ambalo halikuwa la kawaida. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hotuba hii ya Mheshimiwa Rais, nimwambie peleka zile fedha kwenye barabara ya Kawawa mara mvua itakapoisha na siku ya kufungua uniite. (Makofi)