Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya ya kupangua safu ya Viongozi wenye kuingizia Serikali hasara.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wa Utawala Bora na Katibu Mkuu wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha katika Ofisi za Serikali kumekuwa na nidhamu ya kazi. Nidhamu ya kazi imerejea kwa wananchi katika upande wa kuwahi kazini na kupunguza utoro wa kazi kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kuendesha zoezi la watumishi hewa kwa uelevu wa hali ya juu. Nimekuwa nikiona jinsi mnavyotoa maelekezo kwa Ma-DC, Wakurugenzi na Maafisa Utumishi kuzingatia masharti ya Utumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mafunzo kazini; ni vyema Serikali ikatenga fungu la Semina Elekezi kwa Viongozi/Wafanyakazi wanaopewa nafasi mbalimbali kwa kuwa semina hizo zitawasaidia Watendaji au Viongozi kutekeleza majukumu yao kwa njia sahihi na kwa uhakika zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uzoefu wa kazi kwa vijana wanaoomba ajira mpya; kipengele hiki ni kigumu sana kwa vijana wetu wanaotoka Vyuoni. Kwa nini wale wanaoenda kwenye Ualimu, Udaktari, Uuguzi, hawaambiwi uzoefu wa kazi na wale wanaoajiriwa kwenye Taasisi za Serikali hata kama ni Daktari anatoka Chuoni anaambiwa awe na uzoefu wa kazi tena?
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu ya kutoa na kupokea rushwa bado inahitajika kwenye jamii. Kuna baadhi ya Shule za Sekondari zina Club za rushwa. Je, TAKUKURU wanazijua hizo na kuzifuatilia? Ni vyema TAKUKURU wakae na Wizara ya Elimu kuweka suala zima la rushwa katika mtaala wa masomo. Tukilea watoto wetu kwa maono ya kuogopa kutoa au kupokea rushwa, hiyo inaweza kusaidia kuondokana na rushwa katika Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya jambo jema kuondoa au kupunguza matatizo katika kaya maskini kupitia TASAF. Naipongeza Serikali kwa kuwa fedha hizi zimewasaidia sana wananchi wetu kusomesha watoto na kuwasaidia kupeleka watoto Kliniki kupima afya zao. Katika Mkoa wa Dar es Salaam wako wananchi ambao hawakupata nafasi ya kuingia kwenye mpango au kwa uwoga au kwa madhumuni mengine, lakini sasa wako tayari kujiunga. Naomba Serikali iwapokee.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya viongozi wetu wa Serikali za Mtaa ndio wanapotosha watu wa TASAF. Wao waende kwa malengo yao, wasivurugwe na Wanasiasa kwa interest zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba TASAF wasaidie wale wenye UKIMWI, ikiwa ameamua kujiweka wazi pamoja na watoto wenye maambukizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.