Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii nyeti na muhimu sana ya Maji na Umwagiliaji. Ni ukweli ulio dhahiri kabisa kwamba Wizara hii ni muhimu sana na ni uti wa mgongo wa Taifa hili na pia ninaunga sana ule msemo wa maji ni uhai.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nitoe shukrani zangu za dhati kwa Naibu Waziri wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Mheshimwa Engineer Kamwelwe kwa kufanya ziara muhimu kabisa Jimboni kwangu Mikumi na Wilayani kwetu Kilosa kwa ujumla. Mheshimiwa Kamwelwe alipokuwa Jimboni Mikumi alifanya na kuahidi mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo cha maji cha Sigareti kilichopo kata ya Ruaha, Mheshimiwa Naibu Waziri alituma wataalam wa Wilaya ya Kilosa wakakague chanzo hiki na wataalam walifanya hivyo na kunipa report ya kitaalamu kuwa chanzo hiki cha Sigareti ni chanzo cha mserereko chenye maji mengi, safi na salama, kinaweza kutoa huduma kwa wananchi wa kata ya Ruaha yenye wakazi zaidi ya 30,000 na kata za jirani za Ruhembe na vijiji vyake.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ulikadiriwa kufikia kiasi cha pesa cha shilingi bilioni mbili na kidogo na nilipomletea Mheshimiwa Naibu Waziri aliahidi kuwa kiasi hicho cha pesa kitawekwa kwenye bajeti hii ya mwaka 2017/ 2018. Niliwaambia wananchi wasikivu wa kata ya Ruaha ambao walifurahi sana na kutoa pongezi nyingi kwa Serikali hii kwa kusikia kilio chao cha muda mrefu, lakini cha kusikitisha bajeti ya chanzo hiki muhimu cha maji cha Sigareti haipo kwenye taarifa ya bajeti hii.

Naomba Waziri atimize ahadi yake kwa wananchi wa kata ya Ruaha na kuwawekea au kutenga pesa hizo shilingi bilioni mbili ili mradi huu muhimu wa maji uweze kuanza kujengwa na kuokoa vifo vya akina mama na watoto wa kata ya Ruaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Madibila katika kata ya Mikumi niliwahi kuuliza ni lini Serikali itakarabati miundombinu na intake ya chanzo cha maji cha Madibila ambacho kilijengwa mwaka 1975 wakati idadi ya wakazi wa Mikumi ni watu 6000 tu na sasa imepita miaka 40 miundombinu ni ile ile chakavu sana na wakazi wa Mji Mdogo wa Mikumi wamefikia watu 30,000 na zaidi, Naibu Waziri alianiahidi kwenye majibu yake kuwa wanalitambua tatizo hilo na watalifanyia kazi kuanzia mwezi Julai mwaka huu, lakini sijaona pesa zikiwa zinatengwa specifically kwa ajili ya chanzo hiki muhimu cha maji cha Madibila kwa wakazi wa Mji Mdogo wa Mikumi. Naomba majibu je, Serikali imetenga kiasi gani cha fedha kwa ajili ya mradi huu wa chanzo cha Madibila.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyanzo vya maji vya Iyovi na Mto Mholanzi ni wazi Mji wa Mikumi ni mji wa kitalii na unakua kwa kasi sana kwa kupata wageni na watalii mbalimbali kutoka kona zote za dunia. Tatizo sugu la maji linapunguza sana kasi ya wawekezaji wa mahoteli na sekta mbalimbali za kukuza uchumi wakati Mikumi ina vyanzo vingi sana vya maji kama Mto Iyovi na Mto Mholanzi. Je, ni lini sasa Serikali itavifanyia kazi vyanzo hivi vyenye maji mengi tena ya gravity au mserereko vyenye gharama nafuu kabisa kuokoa wananchi wa Mikumi na kukuza mji na uchumi wa wananchi wa Mikumi kama ambavyo wenzetu wa Kanda ya Ziwa walivyotumia vizuri Ziwa Victoria kupunguza tatizo hili sugu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mradi wa maji wa vijiji kumi katika kata ya Mikumi na Kidodi. Mradi wa Maji wa Visima wa World Bank kata ya Mikumi bado unasuasua na haujakabidhiwa kwa wananchi kama iliyoahidiwa na Mkandarasi Malaika Construction, pamoja na Serikali kumpatia shilingi milioni 208 alizoomba. Pia vituo vya maji 52 vimeanza kuharibika kwa kuwa vilijengwa muda mrefu na tanki la lita 300,000 bado wananchi hawaoni mwanga wa kupata maji safi na salama ingawa majaribio yalifanyika na akinamama na watoto wa Mikumi walifurahi sana kuona maji yanatoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kustaajabisha mpaka leo mradi huu haujakabidhiwa kwa wananchi. Tunataka kujua ni lini mkandarasi Malaika atakabidhi mradi huu kama alivyokuahidi wewe na wananchi wa Mji Mdogo wa Mikumi? Pia Mradi wa Msowero uliopo kata ya Kidodo ulikabidhiwa kwa wananchi wa kata ya Kidodo tangu mwaka 2015, lakini cha kushangaza ni kuwa tangu mradi huu umekabidhiwa kwa wananchi maji hayatoki, naomba kauli ya Serikali kuhusu mradi huu muhimu wa Msowero uliopo kata ya Kidodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji wa Lengewaha kata ya Uleling’ombe, tunaomba sana Serikali imlipe pesa mkandarasi wa mradi huu ili arudi site, maana hayupo kwa muda mrefu na tunaomba tujue tatizo liko wapi na kama ameshindwa kazi basi afukuzwe na kuvunja naye mkataba, na kama anadai basi alipwe pesa zake ili aendelee na umaliziaji wa mradi huu muhimu kwa wananchi wa Uleling’ombe, ambao wanakunywa maji machafu ya mto huku waki-share na wanyama na kusababisha magonjwa ya mara kwa mara ya mlipuko na kusababisha vifo kwa mama zetu na watoto wa Kata ya Uleling’ombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu visima, tunaiomba sana Serikali itukumbuke kutuchimbia visima virefu na vifupi hasa kwenye kata za Mhenda, Malolo, Ulaya, Msanze, Kilangali, Mabwerebwere, Tindiga, Ruhembe, Vidunda, Ruaha, Kisanga Zombo, Mikumi, Uleling’ombe na Zombo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa nimalizie na suala la umwagiliaji, nilishawahi kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji ni lini Serikali itatoa tamko na kutuma wakaguzi wakakague mradi wa umwagiliaji wa Bwawa la Dachi lililopo kwenye kata ya Malolo, ambapo Serikali kupitia ufadhili wa Shirika la Kijapan la JICA ambao walitoa zaidi ya shilingi milioni 600 ambazo zimeliwa na bado makingio ya mchanga unaohatarisha Mto Mwega kujaa mchanga, na kupoteza kabisa nia njema ya wananchi wa Kata ya Malolo wanaoutegemea kwa kilimo cha umwagiliaji vitunguu, mboga mboga na mazao mengine muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, makingio hayo yamejengwa chini ya kiwango, michanga bado inajaa kwenye mto mwega, shilingi milioni 600 zimeliwa na hakuna mtu yeyote anayehoji kuhusu ubadhirifu huu mkubwa sana unaohatarisha maisha ya wananchi wetu wa kata ya Malolo. Naomba Waziri akija kuhitimisha atuambie ni lini atakuja kata ya Malolo akiongozana na mimi ili kusikia kilio kikuu cha wananchi hawa kuhusu Bwawa la Dachi na shida yao ya maji ambayo yanahatarisha maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa kumalizia Naibu Waziri akijibu swali langu alijibu kuwa mkandarasi wa Bwawa la Kidete lililopo Wilayani Kilosa mkataba wake umesitishwa na tender itatangazwa hivi karibuni, nimeona kwenye ukurasa wa 47 wa hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji kuwa ni moja kati ya mabwawa yatakayojengwa kwenye bajeti hii ya mwaka 2017/2018. Wananchi wa Wilaya ya Kilosa wanataka kujua ni kiasi gani kimetengwa kwenye ujenzi wa bwawa hili muhimu la Kidete ambalo linasababisha mafuriko ya mara kwa mara Wilayani Kilosa yanaharibu makazi ya watu. Vifo vya wakazi wa Wilaya ya Kilosa na pia mafuriko yanayosababishwa na Bwawa la Kidete yanasababisha uharibifu mkubwa sana, reli yetu ya kati ambayo Serikali inajitahidi kuijenga kwa kiwango cha standard gauge na lini ujenzi huu wa Bwawa la Kidete utaaanza. Ahsante.