Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi uliyonipa. Ninazo hoja chache ambazo nataka kuchangia. Moja, ni ile hoja ya kemikali zenye sumu zinazotumika mashambani ambazo zinazagaa kwenye mazingira na kuathiri vyanzo vya maji na mazingira kwa ujumla. Hoja hii iliulizwa na Waheshimiwa Wabunge katika michango yao na Mheshimiwa Vullu ndio aliuliza. Ni kweli kwamba kwanza tunazo taasisi nyingi sana ambazo zinasimamia kemikali hapa nchini; uingizaji, usambazaji, uzalishaji na utumiaji wa kemikali hapa nchini. Taasisi zote hizo kwa pamoja kila moja inalo eneo lake la kusimamia. Sasa eneo hili la kemikali za mashamba linasimamiwa na TPRI na NEMC.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoweza kusema hapa, tutakachokifanya kule ambako Mheshimiwa anakulalamikia ni kwamba hizi sumu zimekuwa na shida kubwa na zinaathiri wananchi, tutawatuma TPRI pamoja na NEMC waende wakafanye kazi hiyo ili kujua hatua sahihi za kuchukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kwa maana ya kemikali nchini, tumegundua pia kwamba kulikuwa pia na usimamizi dhaifu kule nyuma. Tumeimarisha mfumo mzima wa kuhakikisha kwamba kemikali hapa nchini zinasimamiwa vizuri ili zisiweze kuleta athari kwa wananchi. Moja ya hatua kubwa ambayo tumeichukua ni kuanza maandalizi ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na incinerator kwa ajili ya kuteketeza mabakio ya vifungashio vya hizo kemikali lakini pamoja na kemikali ambazo zimesha-expire.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia sana juu ya Jiji la Dar es Salaam kwamba linazidi kuongezeka ukubwa, watu wanazidi kuongezeka na shughuli za kiuchumi zinazidi kuongezeka, lakini miundombinu ya majitaka haiongezeki. Nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge, ni kweli kwa muda mrefu Jiji la Dar es Salaam ni asilimia 10 tu ya miundombinu ya majitaka. Miundombinu ya majisafi imekuwa ikiendelea kujengwa lakini miundombinu ya majitaka ilikuwa ni asilimia 10 tu toka miaka ya 1970 na kusababisha madhara makubwa sana ya kutapakaa kwa maji taka katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumechukua hatua kubwa na mkisoma katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 74, ndiyo utaona hatua tulizozichukua kupitia Shirika la Serikali za DAWASA ambapo leo tunazungumzia zaidi ya shilingi bilioni 342 ambazo zimetolewa na Serikali ya Korea pamoja na Benki ya Dunia kwa ajili ya kuhakikisha kuwa tunajenga miundombinu ya kuimarisha Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia DAWASA hiyo hiyo, kuna commitment kubwa ya fedha nyingine za kutoka DANIDA pamoja na IFD kwa maana ya Serikali ya Ufaransa ambayo itakuwa na zaidi ya karibu shilingi bilioni 914. Katika hii Serikali ya Awamu wa Tano tunaenda kumaliza kabisa tatizo la majitaka ambalo linazungumziwa na Waheshimiwa Wabunge katika Jiji la Dar es Salaam. Nami nawapongeza DAWASA kwa kazi nzuri hiyo waliyoifanya ambapo ujenzi unaanza mwaka huu tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatutaishia hapo, suala la kutoa vibali kwa ajili ya majengo makubwa pamoja na shughuli nyingine ambazo zinapelekea majitaka kutapakaa, tutazidhibiti kwa karibu zaidi ili kuhakikisha kwamba utapakaaji huo wa majitaka hauwezi kutokea tena. Kwa kwa mipango hii tuliyonayo tu hii ya hivi karibuni kwa maana ya kupitia DAWASA ni kwamba miundombinu hii ikijengwa, asilimia 10 mpaka asilimia 30 tutakuwa tumefikia katika uondoaji wa majitaka katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuishii hapo tu, hata ukiangalia pia Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI alizungumza kuhusu miundombinu ambayo imejengwa na miradi mbalimbali katika Majiji saba pamoja na Halmashauri 18, yote hayo ni kuhakikisha kwamba tunadhibiti utapakaaji wa majitaka na hivyo tunaongeza ubora wa maji yetu tunapouepusha na hizi taka ambazo zinazagaa kila mahali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine tutakalohakikisha kabisa ni kwamba hakuna namna yoyote ambayo watu wataendelea kuchafua maji yetu ambayo watu wataendelea kuharibu maji kwa namna yoyote au kwa shughuli zozote zile za kiuchumi ambazo zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ambalo Waheshimiwa Wabunge walilizungumza ni kwamba Serikali kuchukua hatua gani katika suala la vyanzo vya maji? Katika suala la vyanzo vya maji, kuhusu kuvilinda vyanzo hivyo pamoja na madakio yake, sheria mbili zote tunazo; Sheria ya Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira Na. 12 ya mwaka 2009 pamoja na Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004, zote hizi zinatoa nafasi nzuri sana ya kusimamia hivi vyanzo vya maji. Kwa hiyo, la kwanza kabisa ni kuhakikisha kwamba sheria hizi tunazisimamia vizuri ili tuhakikishe kwamba maji yetu yako salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, lazima tuvilinde vyanzo hivyo vya maji na Serikali kwa kuanzia tumehakikisha kwamba TFS imeenda kila Wilaya. Kwa sasa hivi TFS iko kila Wilaya na tunahakikisha kwamba wanachangia angalau miche 150,000 mpaka 500,000 kwa kila Halmashauri na kwa kila Wilaya. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, waoneni TFS kule kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mnapeleka msukumo mkubwa katika upandaji wa miti hasa katika maeneo ya vyanzo vya maji ili kulinda vyanzo hivyo vya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala hili la mabadiliko ya tabianchi. Suala la mabadiliko ya tabianchi ni tatizo kubwa sana hapa nchini sasa. Ni takriban zaidi ya shilingi bilioni 180 Taifa hili linapata hasara kwa mwaka kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Sasa tuamue kuchukua hatua. Tumeingia mikataba na dunia sasa hivi inahangaika makubaliano na mkataba wa Paris tumekubaliana kwamba tusiruhusu gesi joto iongezeke zaidi ya nyuzijoto mbili na kwa sasa hivi ongezeko la nyuzijoto limefikia 0.85.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mkakati wetu sasa ni lazima tukubaliane kama Taifa kuhakikisha kwamba tunafanya kwa nguvu zetu zote; moja ni kupanda miti kama wendawazimu katika Taifa hili ili kuweza kumudu haya madhara ya mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhakikisha kwamba tunabuni miradi mizuri ya kuhimili mabadiliko ya tabianchi sasa. Kama sasa hivi inavyoripotiwa mvua nyingi, maporomoko, mafuriko, wananchi wana matatizo makubwa. Kwa hiyo, sasa kama Taifa, tuamue kuhakikisha kwamba njia bora zitakazotuwezesha kwa ajili ya kuondosha hili tatizo la mabadiliko ya tabianchi tuweze kulihimili, ni kuhakikisha kwamba miradi hiyo tunayoibuni ya kuhimili mabadiliko ya tabianchi tunaifanya kwa nguvu zetu zote. Sasa hivi sekta zote za kiuchumi zimeathirika.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tunachopaswa kufanya ni kuhakikisha kwamba tunao mkakati wa mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2012, kwa hoja za Waheshimiwa Wabunge ambao wamezizungumza hapa; huu mkakati tumeuandaa toka mwaka 2012.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona ni vyema basi, tutaomba kwa nafasi yako ikiwezekana tuendeshe Semina na Wabunge ili tuweze kuwasilisha mkakati wa mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2012 mbele ya Bunge hili. Vile vile tuweze kuwasilisha hali ya mazingira ya Taifa hili ya mwaka 2014. Pia tuweze kuwasilisha mkakati wa kuhifadhi mazingira na ardhi na vyanzo vya maji ya mwaka 2006 pamoja na mkakati wa hatua za haraka za kuhifadhi mazingira ya bahari ukanda wa Pwani; maziwa, mito na mabwawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo, nadhani sasa tutakuwa tumepata mwanzo mzuri wa kwenda pamoja na Bunge hili katika kushughulikia mambo haya ambayo ni makubwa na kuweka mipango ya pamoja ambayo itatuhakikishia kwamba tunatoka hapa tulipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.