Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kunipa nafasi hii kuchangia maazimio ambayo yamewasilishwa kwenye Bunge hili. Kwanza ninapongeze kwa uwasilishaji ambao wawasilishaji wote wameyaelezea kwa ufasaha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la amani suala la msingi sana katika nchi yetu. Ili nchi iweze kufanya kazi vizuri ni sharti tuwe na amani ya kutosha, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri alipokuwa anawasilisha ni vema sasa kama Bunge tuli-support Azimio hili kwa ajili ya kulinda amani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sisi tunaoishi mipakani bado kuna shida kubwa sana ya Watanzania ambao wengine wanaishi bila kuwa na uhakika mzuri wa maisha yao, tunaiomba sana Serikali iimarishe suala zima la ulinzi na usalama hasa maeneo ya mipakani. Mimi natoka Mkoa wa Katavi ambao tumepakana na Ziwa Tanganyika pia nchi ya Congo tumepakana nayo. Wapo Watanzania ambao wanaishi mazingira ambayo siyo sahihi. Naomba sana Serikali iweze kuangalia mazingira hasa nchi zile zinazopakana na Maziwa kama ilivyo Mkoa wa Katavi, Rukwa na Kigoma maeneo haya tunahitaji sana kuweka ulinzi shirikishi katika nchi zote tunazopakana nazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania ni watu wakarimu, tumeweza kuwapokea wananchi wa Mataifa mbalimbali kama Congo, Burundi lakini mazingira tunayoishi kule ni mazingira ambayo Serikali inahitaji kuweka ulinzi shirikishi ili kupunguza haya matatizo ambayo yanaweza yakajitokeza. Naipongeza Serikali kwa Azimio lililoletwa, naamini litakuwa suluhisho kwa nchi zote za Afrika Mashariki na zile ambazo ziko nje ya Afrika Mashariki kama DRC-Congo tuweze kuazimia yale ambayo yamewekwa ili yawe na tija kwa Taifa letu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni juu ya Bonde la Mto Songwe. Bonde la Mto Songwe, Azimio lililoletwa ni muafaka lakini lina mazingira ambayo yanafanana na maeneo mengine. Nizungumzie maeneo ya Mkoa wa Katavi.

Tunayo mabonde ambayo yametoka, tuna mito ambayo imetoka maeneo ya kwetu na imeenda mpaka nchi ya DRC- Congo, tuna Mto Lwegere ambao umevuka Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna madhara ya suala zima la mazingira. Upande wa Congo, Ziwa Tanganyika linapeleka maji ambayo yanaleta athari kwa nchi yetu, sasa ni vema tunapoweka mikataba hii tuangalie na maeneo mengine ambayo kimsingi yanaweza yakachangia suala zima la maendeleo na suala zima la mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, nje ya hapo tuna Mto Nile ambao unatoka Ziwa Victoria. Ni vema sasa tuangalie mazingira ambayo yatakuwa ni mazuri kwa nchi yetu, kuwatengenezea mazingira mazuri hasa Watanzania. Mfano, Mto Nile ni mto ambao unatoka kwenye maeneo yetu lakini Wamiliki wakubwa wa Mto Nile ni wenzetu watu wa Misri, ni vizuri tukaangalia maeneo haya, tukayapitia upya ili yawe na manufaa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mazingira ni suala ambalo linahitaji sasa liwekewe kipaumbele na Wizara husika ili tuweze kulinda Mabonde na mito ambayo kimsingi inahama. Bonde la Mto Songwe linahama na ndiyo maana limeletwa hapa kwa sababu mipaka huwa inahama kutoka sehemu moja hadi sehemu nyingine, lakini bado kwenye maeneo yetu ya ndani, leo hii tunapozungumzia mabonde haya ambayo chanzo ni uharibifu wa mazingira, tuna Mto Katuma ambao unapeleka maji kwenye hifadhi ya Katavi na unapeleka maji mpaka kwenye Ziwa Rukwa, leo hii Ziwa Rukwa linapoteza thamani yake na upo uwezekano wa kutoweka kabisa, ni kwa sababu hakuna ulinzi mzuri wa mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Waziri mwenye dhamana aendelee na jitihada ambazo zitatengeneza mazingira mazuri ili kujenga mikakati ya kulinda suala zima la mazingira, lakini cha kufurahisha kwenye Azimio hili ni juu ya mpango wa uwezeshwaji wa kiuchumi kwenye maeneo yote. Tuwaombe sasa Wataalam waweze kushughulikia uhalisia wa kutengeneza mazingira ambayo yatalinda hadhi ya Watanzania waweze kuwezeshwa kiuchumi ili waweze kuendana na uhalisia wa mabonde haya ambayo wamezungukwa nayo kwenye maeneo ya mipakani.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tuwaombe sana wataalam wetu watengeneze mazingira ya kisheria yatakayolinda nchi yetu ili Watanzania na wale ambao wanazunguka katika maeneo hayo wawe na faida na haya Maazimio tunayoyakubali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.