Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru nami kupata fursa ya kuchangia mjadala unaoendelea. Napenda kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pole sana kwa Mheshimiwa Tundu Lissu kwa yaliyompata na kuungana nao vilevile kumwomba Mwenyezi Mungu amjalie apate afya njema na arudi katika shughuli zake za kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita katika hoja moja iliyotolewa kuhusiana na Azimio la Kuridhia Mkataba Kuanza Kamisheni ya Pamoja Bonde la Mto Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Azimio hili ni muhimu sana kwa nchi yetu na katika hali ya kawaida, limechelewa sana. Kumekuwepo na majadiliano ya kuanzisha Kamisheni ya kusimamia bonde hili kati ya Tanzania na Malawi tokea mwaka 1976. Kwa kweli imechelewa sana kwa sababu rasilimali ambayo inatumika na nchi zaidi ya moja katika hali ya kawaida ingetakiwa iwe na utaratibu wa pamoja wa kusimamia; na katika hali ya kimazingira ambayo bonde lile lipo kwa sasa, kwa kweli Kamisheni hii ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja ilitolewa kwamba kifungu cha convention hii inayozungumzia kuhusu usuluhishi wa migogoro inapingana na sheria ambayo tulipitisha ya Natural Wealth and Resource Permanent Sovereignty Act ya 2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Tundu Lissu alitoa hoja kwamba kwa sababu itifaki ambayo tunaizungumzia inaanzisha utaratibu ambao kama kutakuwa na mgogoro kati ya Malawi na Tanzania kuhusu usimamizi wa Bonge la Mto Songwe, basi itapelekwa kwenye Tribunal la SADC. Yeye aliona inaingiliana na inavunja sheria ambayo tumepitisha hivi karibuni ya kusimamia rasilimali zetu, sheria ambayo nimeitaja ya Natural Wealth and Resource Permanent Sovereignty Act of 2017, hasa katika Kifungu cha 11(1) mpaka (3).

Mheshimiwa Naibu Spika, mikataba hii au sheria hizi ni tofauti. Wakati Mkataba wa Kuanzisha Kamisheni ya Pamoja ya Usimamizi wa Bonde la Mto Songwe inashughulika na uhusiano wa nchi na nchi, yaani katika maana ya bilateral agreement, sheria yetu ile ambayo nimeitaja ya Permanent Sovereignty, yenyewe inahusika na uhusiano wa nchi yetu na wawekezaji au makampuni ambayo yanawekeza katika rasilimali zilizoko katika nchi yetu.

Kwa hiyo, katika hali ya kawaida ni mikataba tofauti; mwingine ni mkataba wa Kimataifa ambao unaongoza ushirikiano kati ya nchi mbili lakini nyingine ni sheria ya ndani inayohusiana tu na mikataba ya kutumia rasilimali zilizopo ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, ni vitu tofauti na wala hakuna hatari yoyote katika sisi kuridhia itifaki hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ni lazima tufahamu kwamba katika hali ya kawaida kama rasilimali ambayo inalindwa na sheria inatumika na zaidi ya nchi moja, haiwezekani sheria ya nchi moja ikawa ndiyo inayotawala rasilimali ile. Kwa hiyo, kwa sababu rasilimali ya Bonde la Mto Songwe ni shared resource, ni rasilimali ya nchi zaidi ya moja, katika hali ya kawaida ni lazima isimamiwe kwa pamoja na kwa sheria ambayo ni ya pamoja. Itifaki hiyo ambayo ndiyo tunasema sasa tunataka ianze kufanya kazi, imetengenezwa kwa utaratibu wa itifaki za Jumuiya ya Kusini mwa Afrika SADC ambayo sisi ni wanachama na Malawi vilevile ni mwanachama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa pamoja tulishakubali huko nyuma tulipojiunga kwamba masuala yote ambayo yanahusiana na maji au rasilimali ambazo zinamilikiwa kwa pamoja, kama kuna migogoro, migogoro ile itaamuliwa kwa kutumia Tribunal au Mahakama ya SADC. Kwa hiyo, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba hakuna sheria yoyote iliyovunjwa, tuko sahihi kabisa. Sisi tukiridhia Azimio hili wala hatutakuwa tumevunja sheria yetu ambayo sisi wenyewe tumeipitisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hoja ile iliekea kutaka kujenga hoja kwamba sisi hatuheshimu sheria za Kimataifa tunapotunga sheria kama ile ya kwetu The Natural Wealth and Resources Permanent Sovereignty Act, 2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunaheshimu sheria za Kimataifa na ndiyo maana hata leo hii tupo hapa tunazungumzia kuhusu Bilateral Convention, ni sheria ambayo kwa mwonekano wake, kwa hali yake ya kawaida ni Sheria ya Kimataifa, bado tunaendelea kuheshimu, lakini kuheshimu kule haitunyimi sisi kuendelea kulinda rasilimali zetu ikiwa ni pamoja na kuweka utaratibu wa kusuluhisha migogoro ambapo tunafikiri italinda zaidi rasilimali zetu, itatupa nafasi kubwa zaidi ya kuweza kusimamia rasilimali zetu bila kuingiliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache, napenda kuunga mkono hoja ya Azimio lililopo mbele yetu. Nashukuru sana.