Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami nichangie kwa kifupi tu kuhusu moja ya mazimio yaliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mshituko mkubwa nilioupata kwa taarifa uliyotupa hapa kuhusu Mbunge mwenzetu, naungana nawe kabisa kumwombea mwenzetu apate ahueni haraka na vilevile namwomba Mwenyezi Mungu atupe ustahimilivu mkubwa katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nalazimika kusimama kama nilivyosema, kuchangia kuhusu Azimio la Kuanzisha Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Tanzania na Malawi. Kuanzishwa kwa Kamisheni hii ambako kuna miradi chini yake kadhaa ya maendeleo kwa wananchi, ni sawa kabisa na kutumia jiwe moja na kuua ndege watatu kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa Azimio hili litawanufaisha watu zaidi ya laki tatu; ni idadi kubwa sana hii ambayo iko katika hilo bonde hasa kupitia miradi yao hiyo ya umwagiliaji, miradi hiyo ya maji safi na vilevile miradi ya umeme, kama ambavyo wenzangu wameeleza nisingependa kurudia.

Pili, tutakuwa tumetatua tatizo sugu la muda mrefu la Mto Songwe kupindapinda kubadilisha njia yake kila wakati na kusababisha watu waliokuwa Tanzania kuwa wa Malawi mara nyingine na Wamalawi kuwa Watanzania. TRA najua watashangilia sana kusikia hili, maana wanaowadai kodi, mara nyingine wanashindwa kwenda kuwadai maana tayari wako Malawi kutokana na maamuzi ya huo mto.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingine wengine hapa tunategemea kura kwa Watanzania wetu. Kuna kipindi nimewahi kukuta ngome yangu kubwa yote imehamia Malawi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya ndiyo mambo ambayo watu wote kwa kweli katika Bonde hili watashangilia sana kwamba Azimio hili linaenda kutatua tatizo lililokuwa sugu kati ya Tanzania na Malawi kuhusu mpaka huo ambapo tuliwahi kufikia hata mahali hata eti kufikiria kujenga nguzo katikati ya huo mto. Kutokana na haya mabwawa matatu, hakutakuwa na mafuriko ya kutushangaza tena eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, Azimio hili linatupa fursa maalum, fursa muhimu ya maelewano zaidi kati ya Tanzania na Malawi. Sasa hivi tumeanza ushirikiano, nami nina uhakika huu utakuwa ndiyo msingi wa maelewano zaidi na zaidi kati ya nchi zetu hizi mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuhakikishie tu kitu kimoja kwamba nilikuwa namwangalia rafiki yangu ananiangalia hapa, kwamba mimi eneo langu pale Kyela halijawahi kuhamia Malawi. Sasa tusije tukaanza kueleweka vibaya hapa, halijawahi. Muda wote mimi niko mbali kidogo na huo mto, lakini naongelea tu kwa meneo yote ambayo yanahusika Wilaya ya Kyela.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuipongeza sana Serikali kwa Azimio hili, kwa uamuzi huu kupitia Wizara yetu ya Maji na Umwagiliaji, kwa sababu watakaofaidika sana katika mradi huu; ni pamoja na Wilaya yangu, Jimbo langu la Uchaguzi la Kyela, hasa Kata zetu za Ngana, Katumbasongwe, Ikimba, Njisi, Ikolo, Ngonga, Bujonde, wote hapa katikati tutafaidika sana na Azimio hili tunalolipitisha leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nisipoteze muda wako mwingi, naomba tu kusema, naunga mkono Azimio hili. Ahsante sana.