Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hon. Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuhitimisha hoja, lakini kwa ruhusa yako, kabla sijahitimisha hoja, naomba niseme mambo mawili. La kwanza, kama ambavyo mmesikia Mbunge mwenzetu ameshambuliwa kwa shambulio baya na watu wasiojulikana, lakini taarifa rasmi mtapewa. Tutatoa kwa utaratibu kadiri tutakavyoongozwa na Bunge hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa tu za awali ni kwamba Madaktari wamejitahidi kwa kiwango cha hali ya juu kuweza kutoa huduma ya kwanza. Nimechelewa kuja hapa, nilikuwa pale na Mheshimiwa Spika, briefing ya mwisho tuliyopewa ni kwamba wamefanya vizuri wameweza kudhibiti damu zilizokuwa zinatoka. Kwa hiyo, wamesema hatua ya awali ya huduma ya kwanza waliyotoa imeenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la awali tu kwa upande wa Wizara ya Mambo ya Ndani, japo tutatoa tamko rasmi, lakini tunasema jambo hili lililotokea ni jambo ambalo halikubaliki; nasi kama Wizara ya Mambo ya Ndani na kama Serikali, hatutaruhusu na hatutaacha jambo hili lipite hivi hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeelekeza Polisi Mkoa wa Dodoma waweke vizuizi njia zote zinazotoka Dodoma na zinazoingia Dodoma na wasambae kuweza kuwasaka hao wote ambao wamehusika na tukio hili, tukio ambalo linapaka matope sura na heshima ya nchi yetu na tukio ambalo linapaka matope Serikali yetu ambayo inashughulikia masuala ya usalama wa raia.

Mheshimiwa Naibu Spika, iwe kwa sababu za kisiasa, iwe kwa sababu ya hujuma, iwe kwa sababu za ugomvi na iwe kwa sababu za za kijambazi, yote hayo tutasaka kuhakikisha kwamba wale wote ambao wamehusika na jambo hilo wanafikishwa katika mkono wa sheria ili kuweza kukomesha vitendo hivyo viovu ambavyo havijazoeleka katika nchi yetu. Watanzania wote tumwombee mwenzetu ili Mungu ampe afya njema na afya yake iimarike aweze kuendelea na kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, taarifa rasmi itatolewa kwa utaratibu ambao Kiti chenyewe kitatoa kwa masuala yote ya kiusalama pamoja na kiafya baada ya kuwa wenzetu wamefikia hatua ambayo wanaweza wakatoa taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia, nimeona wameunga mkono Azimio hili. Nami niendelee kusisitiza kwamba Azimio hili ni zuri, lina faida nyingi. Mambo mengi yalikuwa yakifanyika bila kuwa na misingi hii ambayo itakuwa imewekwa na Azimio na baadaye ambayo itapelekea uwepo wa sheria, kanuni na taratibu za kuweza kuyashughulikia mambo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nilisema wakati wa kutoa hoja; na kama ambavyo wachangiaji wameelezea nikitoa na pongezi kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje aliyetoka kusema hivi punde, yatatusaidia katika kushughulikia masuala yaliyo ya kimipaka lakini na yaliyo ya kiujirani mwema hasa yanayohusiana na masuala ya kiusalama wa watu wetu pamoja na mali zao wa nchi hizi mbili na wageni wanaokuja katika nchi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, itatusaidia hata kwenye maisha ya kila siku, masuala haya ambayo tumeyasemea yanayohusu mambo ya migogoro, shughuli za kiuchumi zinazoingiliana katika mipaka yetu. Kwa mfano, watu wetu wanaokaa jirani na mipaka ambao wana shughuli zinazoendana na zinazoingiliana, wao kwa asili zao hawatambui mipaka. Tunaamini uwepo wa Azimio na taratibu za kubadilishana taarifa na kubadilishana uzoefu wa kushughulikia uhalifu, itawasaidia watu wetu waweze kufanya shughuli hizo kwa njia ambayo ni salama na endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kutimiza matakwa ya mikataba ambayo nchi yetu imeingia, nchi yetu ni nchi kiongozi katika uanzilishi wa jumuiya hii na katika uendeshaji wa jumuiya hii. Kwa hiyo, yale ambayo yanakubaliwa kama nchi wanachama ni wajibu wetu pia kama nchi kuweza kutekeleza na kuridhia na hasa baada ya kuwa tumeshajiridhisha na manufaa ambayo nchi yetu itapata kupitia jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, huku tukipokea hoja zote zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge, naomba sasa kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu liridhie Azimio lake la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (The East African Community Protocol on Peace and Security).

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.