Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Itifaki ya Nagoya ya Kusimamia Upatikanaji na Mgawanyo Sahihi wa Faida zitokanazo na Matumizi ya Rasilimali za Kijenetiki.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Itifaki ya Nagoya ya Kusimamia Upatikanaji na Mgawanyo Sahihi wa Faida zitokanazo na Matumizi ya Rasilimali za Kijenetiki.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kunipa nafasi nitoe mchango wangu katika kuridhia hii itifaki ambayo imewasilishwa leo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kama mwasilishaji alivyosema kwamba tunazo faida mbalimbali ameziainisha hapa, faida ambazo tungeweza kuzipata anasema kwamba ni kuimarisha uchumi, kuongeza mazao ya bahari pamoja na ushirikiano wa kikanda. Lakini wazo langu au maoni yangu ni kwamba kwanza kabisa niungane na Kambi Rasmi ya Upinzani yale maoni ambayo wameyatoa naishauri Serikali iendelee kuyazingatia kwa umakini kabisa, kwa sababu tatizo letu siyo tu kuridhia hii mikataba kwanza ni mipango dhabiti ya utekelezaji wa mikataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Tanzania imekuwa na kawaida ya kusuasua sana kutekeleza mikataba mbalimbali ambayo tunaingia ya Kimataifa. Kwa mfano, sasa hivi tunakwenda kuridhia hii itifaki ambayo tunaizungumzia leo, lakini je, Serikali iko tayari kuleta sheria, kutunga sheria za utekelezaji ambayo itasimamia kwa uhalisia kabisa kulingana na matakwa ya mikataba hii ambayo tunakwenda kuiridhia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia tunayo taasisi ambayo kama msemaji aliyepita alisema Taasisi ya Uhifadhi wa Mali/Bidhaa za Bahari. Lakini je, hii taasisi kama Serikali mmeiwezesha kwa kiwango gani ili hayo matakwa yaweze kutekelezeka kama ambavyo tumeridhia? Vilevile kwenye utafiti mara nyingi tumekuwa tukiibiwa rasilimali zetu nyingi za baharini na nchi kavu na hawa watu wanaojiita watafiti. Ni kweli kabisa mara nyingi watafiti wanapofanya utafiti wanaondoka na viumbe hai, wanaondoka na mali zetu, lakini sisi wenyewe tumejidhatiti kwa kiwango gani, hizi tafiti badala ya kufanyika na watu wa nje na wenyewe tuweze kufanya hizi tafiti ili taasisi yetu kwa mfano, Maritime Institute pale Dar es Salaam sijui kwamba na yenyewe imeimarishwa kwa kiwango gani ili tafiti nyingine ziweze kufanyika hapa nchini badala ya kwamba hawa watu wanakuja kutuibia, wakati wenyewe tuna uwezo nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia mara nyingi Watanzania tumekuwa na kigugumizi sana. Mimi sijaelewa Serikali inakuwaga na kigugumizi cha namna gani, kwa sababu ukiangalia mikataba mingi tuliyoridhia kwanza tunachukua muda mrefu sana kuiridhia na baada ya kuiridhia tunakuwa na kigugumizi sana katika utekelezaji. Naiomba Serikali izingatie ushauri ambao umetolewa na Kambi Rasmi ya Upinzani na Wabunge mbalimbali ambao wanachangia hapa. Hili wote tunajua kwamba tunafanya hivi kwa kuhifadhi mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema ukweli kwa upande wa baharini, kwa kweli Serikali tumesahau sana bahari, kwa sababu ukiangalia uchumi Tanzania tumezungukwa na Pwani kutoka Tanga mpaka Mtwara, lakini ni kiwango gani tunanufaika? Serikali inanufaikaje na fukwe hizi? Tumewekeza kwa kiwango gani? Utakuta uwekezaji tuliouwekeza huku ni mdogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema hapa wakati tunachangia bajeti ya kilimo na uvuvi wakasema kwamba sekta binafsi ndiyo wameachiwa wao ndiyo wanunue meli kubwa za uvuvi ili tuweze kuvua na ndio jambo linalopelekea mpaka leo hii tunakula samaki kutoka China. Hivi kweli kwa utajiri huu tulionao Tanzania kuanzia Tanga mpaka Mtwara leo hii hatuna hata meli moja ya uvuvi wa kisasa, hivi tunategemea ulinzi huu wa hizi rasilimali zetu za baharini huyo mlinzi atatoka wapi? Hivi ni kweli hawa Watafiti ambao tunawategemea kutoka nje ndiyo waweze kulinda mali zetu? Kwa kweli jambo hili silioni kama lina tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwa dhati kabisa tutoke tuwekeze kwenye bahari ili nasi tuweze kunufaika nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa hayo machache naunga mkono hoja.