Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Kazi za Ubaharia wa Shirika la Kazi Duniani na Azimio la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Vitambulisho vya Mabaharia Na. 185 wa Mwaka 2003 wa Shirika la Kazi Duniani

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Kazi za Ubaharia wa Shirika la Kazi Duniani na Azimio la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Vitambulisho vya Mabaharia Na. 185 wa Mwaka 2003 wa Shirika la Kazi Duniani

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu
Spika, naomba kwanza kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, niwashukuru sana Wabunge wote waliochangia, wote wameunga mkono hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuunga mkono hoja yetu ya leo humu ndani Bunge tunaendana pia na kilio cha Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Nchini (TUCTA), lakini na Vyama vya Wafanyakazi ambavyo vimekuwa vikisimamia sekta ya mabaharia nchini, wamekuwa wakililia sana jambo hili Bunge letu Tukufu liweze kuridhia na hivyo leo wanavyotusikia kwa pamoja, ninaposema kwa pamoja , ukisikiliza Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni leo wameunga mkono Maazimio yote haya mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nichukue nafasi hii kumpongeza sana Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa sababu si kwamba kila jambo jema linalofanywa na Serikali ni lazima kupinga, mambo yanayofanywa na Serikali kama ni jambo jema lina faida kwa Watanzania, Kambi Rasmi ya Upinzani inapounga mkono huu ndio uungwana na huu ndio mwenendo mzuri wa uwakilishi wetu ndani ya Bunge kwa kuhakikisha kwamba tunawawakilisha Watanzania wote. Namshukuru sana Mheshimiwa Mtolea kwa kuliona jambo hili ni la msingi kwa manufaa ya Watanzania wote na kuunga mkono hoja yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati nzima. Wamefanya kazi kubwa sana, Kamati hii na kwa namna ya ajabu kamati ilianza kukutana na wadau mbalimbali, iliamua kuchukua hatua ya kujielimisha kwa kina namna nzuri ya kuendana na hoja ambayo Serikali ilikuwa imeipeleka kwenye Kamati, kwa kweli naomba kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu niishukuru sana Kamati na maoni yao yote tunayachukua na tutayazingatia katika kutekeleza mkataba wenyewe baada ya kuridhiwa na Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nizungumze kidogo kuhusu maoni ya Kambi ya Upinzani; Kambi ya Upinzani wao wamesema kwamba ni kwa nini tunachelewa kuleta mikataba ndani ya Bunge ili iweze kuridhiwa. Kama Serikali ni lazima baada ya kusainiwa kwa mikataba ni lazima Serikali tufanye kwanza tafiti za kina tujiridhishe kabla ya kuridhia kweli mikataba hiyo inaendana na hali halisi ya mazingira katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, lazima tujiridhishe, tufanye tafiti za kutosha, tuangalie sera tulizonazo katika nchi yetu, tuangalie uzoefu wa Mataifa ambayo wamekwisha kuridhia, tuone changamoto ambazo wenzetu wanazipata, kusudi sisi tunapokuja kufanya kazi ya uridhiaji angalau tuone tuko kwenye position ya kujihakikishia kwamba hatutakuwa na shida ya utekelezaji wa mkataba wenyewe ndani ya nchi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimtoe hofu Mheshimiwa Mtolea kwamba, tunafanya hiyo kwa nia njema na sio kwamba tunachelewesha kwa makusudi hapana. Tumekuwa tuna uzoefu baadhi ya mikataba ukiangalia unakuta inakinzana kwa namna moja ama nyingine na mazingira halisi ya utendaji wa kazi na usimamizi wa shughuli mbalimbali za kisheria na za kisera ndani ya nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, tutakuwa tunajitahidi kufanya tafiti za kutosha na tunapokwenda kuridhia mikataba tunaridhia tukiwa na uhakika Watanzania watanufaika na kila kila kitu tutakachokiridhia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka yangu Salum Rehani, Mheshimiwa Mbunge amezungumza sana masuala ya leseni kwenye vyombo vyetu vya majini na namna gani pia mabaharia wetu wanaofanya kazi kwenye vyombo vya majini wanavyokosa mikataba ya ajira na mambo mengine ambayo yangeweza kuwapa haki stahiki kama wafanyakazi katika vyombo vya majini. Naomba nimhakikishie kwamba kwa kuridhia mkataba huu kwanza tutakwenda kuweka mfumo mzuri ambao utawasaidia sana Mabaharia kutambulika ndani na nje ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mabaharia wetu wengi ambao walikuwa wanapata ajira kwenye vyombo vya usafiri na hasa vyombo vya nje walikuwa wanadharauriwa sana, hawakuwa wakipata haki, walikuwa hawatambuliki Kimataifa, kwa hiyo, walikuwa wanapata shida sana. Hata hivyo, mkataba huu sasa unatupa sisi nafasi ya kuzitazama sheria tulizonazo ili kuwafanya Mabaharia wetu wanapopata vile vitambulisho sasa waweze kutambulika hata kwenye medani za Kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wale Mabaharia wanaofanya kazi ndani ya nchi yetu ya Tanzania kwa kutumia vyombo tulivyonavyo ndani ya nchi yetu ya Tanzania na sheria tulizonazo, tutaendelea kusimamia. Namhakikishia Mheshimiwa Salum Rehani kwamba, sasa tumepata nguvu mpya ya kuhakikisha kuwa tasnia hii ya kazi ya Mabaharia inakuwa ni kazi yenye staha, yenye heshima na inayotoa fursa kwa vijana wa Tanzania kujiajiri na kuajiriwa na kupata haki na stahiki sawa ndani na nje ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana umeunga mkono na wewe na umeona jambo lenyewe lina msingi kwa hiyo naomba nimshukuru kwa kuliona hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka Mheshimiwa Machano ametukumbusha IMO ni muhimu na hasa sisi upande wa Bara, tuwe tunashiriki, namhakikishia kwamba tutaendelea kufuatilia vikao hivyo na kushiriki kwa manufaa ya nchi yetu. Hata hivyo, ametukumbusha pia kwamba kumekuwa na shida ya usajili wa meli na tozo ambazo zimekuwa zikitolewa wakati wa usajili wa meli na amefurahi sana mkataba huu sasa utakwenda kutatua matatizo mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema kwamba baada ya kuridhia tutakwenda kukaa ndani ya Serikali, chombo kimoja na kingine kinachohusika na mkataba huu ni lazima huko mbele tutakwenda kufanya marekebisho ya sheria mbalimbali ili kuhakikisha kwamba mkataba unaendana na sheria tulizonazo ndani ya nchi yetu ya Tanzania. Nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge, tutatoa fursa nyingi kwa vijana wa Tanzania na kupata ajira za ubaharia katika vyombo mbalimbali ndani na nje ya nchi. Pia nakubaliana na yeye, kwamba tunavyo vyuo vinavyofundisha tasnia ya ubaharia bara na visiwani katika nchi yetu na ni vyuo vizuri, vinatoa Mabaharia wazuri na wamekuwa wakitambulika ndani na nje ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba huu unatuimarisha kwa sababu unatoa fursa ya kupata utaalam kutoka nje ukaletwa tena na kwenye vyuo vyetu vya ndani na kuwafanya mabaharia wetu waweze kubobea katika medani za ndani na nje ya Tanzania. Kwa hiyo, mkataba huu kwa kweli ni mzuri sana na utatoa fursa nzuri sana kwa Mabaharia wetu na vijana wetu wa Tanzania wanaotaka kufanya kazi kwenye tasnia hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa dada Taska amepongeza vijana wengi sasa angalau ajira zao zitakuwa za staha na zitaweza kutambulika vizuri, nakubaliana na yeye. Ametoa hapa rai kwamba ni lazima tuangalie sheria za usajili wa meli na vitu vya namna hiyo. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Taska kwamba, Serikali inalichukua kwa sababu ni suala ambalo litabidi lifanyiwe mazungumzo ya pande zote mbili za Muungano. Tutaendelea kujadiliana na kuona namna nzuri ya kurekebisha utaratibu na mifumo yetu ili pande zote mbili za Muungano ziweze kufaidika na mkataba huu, lakini na sheria zote ambazo zinasimamia masuala yote ya usajili wa meli lakini na masuala ya ajira kwa vijana wetu kwenye tasnia hii ya ubaharia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Shangazi amezungumza hapa kwa urefu na amesema tumechelewa. Ni kweli tumechelewa lakini tumechelewa kwa makusudi maalum nimesema hapo mwanzo na lengo letu lilikuwa ni kujiridhisha kile tunachoenda kufanya kama kweli kitaendana na hali halisi ya mazingira katika nchi yetu ya Tanzania lakini kitakuwa na tija kwa Watanzania ambao wameingia kwenye tasnia hiyo ya ubaharia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ametukumbusha hapa kwamba ni lazima tuangalie tunalinda mipaka yetu kwa sababu kuna vyombo ambavyo vingine vimesajiliwa na vitatakiwa kuendeshwa na mabaharia lakini viko katika maji ya maziwa kwenye nchi yetu. Kwa hiyo, ametukumbusha ni lazima tuhakikishe vinasajiliwa kwa sheria tulizonazo kuepusha ajali na usalama wa abiria, vilevile mabaharia wanaoendesha vyombo hivyo waweze kuwa na viwango vinavyotambulika. Naomba nimwambie Mheshimiwa Shangazi kwamba, tunalichukua hilo na tutalizingatia kwa sababu hata mkataba wenyewe ndio unatutaka tufanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Shangazi ametuambia kwamba ni lazima tuangalie fursa nzuri za kuwatambua Mabaharia tulionao katika nchi yetu Kitaifa na Kimataifa na tuwe na data maalum ya kufanya hivyo, mkataba unatuagiza kuandaa database ya kuwatambua Mabaharia wetu. Kwa hiyo, tutafanya hivyo na tutaweka mfumo na mkataba umetuelekeza Nchi Mwanachama atakayeridhia ni lazima afungue database ya kuwatambua Mabaharia wote. Hiyo pia itatusaidia kuondoa nafasi za kuwepo na Mabaharia ambao watajiingiza katika masuala mengine kama ya uharamia na vitu vingine vya ugaidi na kahdalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo namwambia Mheshimiwa Shangazi tutayazingatia hayo maoni aliyoyasema. Nakumbuka aliyazungumza sana wakati wa Kamati nikiwa pale na naomba tu kumhakikishia kwamba tunayachukua na tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mtolea amezungumza kwamba tuangalie ni namna gani tunawasaidia wavuvi katika kupata hivi vitambulisho. Naomba tu niliambie Bunge lako Tukufu kwamba, vitambulisho hivi kwanza ni kwa ajili ya Mabaharia lakini wavuvi nao hawakatazwi kusomea ubaharia katika vyuo vyetu na wao wakapata vitambulisho hivi na wakaweza kufaidika na mkataba huu lakini tasnia ya ubaharia katika nchi yetu. Vile vile ametuagiza na ametuomba tuharakishe sana kuona sheria zetu tulizonazo zinaweza kuendana sambamba vipi na mikataba hii tuliyoridhia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu, kama nilivyosema mwanzo wakati nawasilisha, tayari tunazo sheria kwa pande zote mbili Bara na Visiwani. Vilevile tunayo nafasi nyingine nzuri baada ya uridhiaji na kuwasilisha hati ILO tukaangalia pia je, sheria hizi sasa zinaendelea kuwa rafiki kwenye mikataba hii? Kama hazionyeshi kuwa rafiki basi Bunge hili tutakuja kwenu tutashirikiana na nyie. Lengo letu siku ya mwisho ni kuwafanya Watanzania waweze kunufaika na kufaidi fursa hii muhimu ya kazi za staha kwenye tasnia hii ya ubaharia ndani na nje ya nchi ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Baada ya kusema hivyo, naomba sasa kutoa hoja Maazimio haya ya Bunge yote mawili kwa pamoja yaweze kuridhiwa na Bunge lako Tukufu ili yaweze kuendelea na hatua nyingine zinazostahiki kwa manufaa ya nchi yetu na kwa manufaa ya Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.