Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumnukuu Mwanafasihi wa Kiingereza…
MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Shakespeare aliwahi kusema maneno yafuatayo: “There is a time to hate and time to love”. Nimewasikiliza wenzangu kutoka Zanzibar kwa makini sana. Naheshimu sana mawazo yao kwa sababu kila mmoja anayo haki kwa mujibu wa Katiba kutoa mawazo yake, nayaheshimu sana. Nimekuwa nikijiuliza sisi Watanzania tunaotoka Zanzibar hatudhani kwamba, wakati umefika kufungua ukurasa mpya! Hatudhani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mingi kila baada ya kumalizika uchaguzi tangu mwaka 1995 tunaingia kwenye mifarakano ya kisiasa, watu wengi sana pamoja na mimi, tulifikiri matatizo ya Zanzibar ni ya kisiasa na kwa msingi huo yanaweza kumalizwa kisiasa! Ndiyo maana watu wanaoipenda Zanzibar na marafiki wa Zanzibar walipendekeza kwamba, vyama viwili vikuu, Chama cha Mapinduzi na CUF, wafikirie tena juu ya mfumo wao wa uchaguzi. Walisema huenda tofauti hizi zinazoonekana na mfumo wa mshindi wa uchaguzi kuchukua kila kitu pengine ndiyo sababu ya mfarakano! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana mwaka 2010 ushauri huo ulikubaliwa, vyama vyetu vilishirikiana kufanya marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar na tukaunda Serikali ya pamoja, Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Kwa bahati mbaya tulifikiria sasa ulifika wakati matatizo haya na mifarakano hii itakuwa imekwisha kwa sababu vyama vikuu viwili vyenye nguvu zinazokaribiana vitafungua ukurasa mpya kwa sababu wanafanya kazi katika Serikali ya pamoja. Kwa bahati mbaya sana jambo hilo halikusaidia sana, tumerudi kulekule tulikotoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nina mapendekezo na namwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu anisikilize vizuri, nina ushauri. Kwa kuwa, suluhu ya Zanzibar haikupatikana au haijapatikana katika misingi ya kisiasa, basi Viongozi, tukiwemo Viongozi wa Zanzibar na Viongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, tufikirie mambo mengine, ni yepi hayo! Tumejaribu kwenye siasa hatujafanikiwa vizuri! Naamini uchache wa rasilimali na hali ya uchumi ya Zanzibar inachangia sana kwa kiasi kikubwa hali hii ya mitafaruku isiyokwisha Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitasema jambo moja mtashangaa! Bajeti ya Zanzibar ya mwaka uliopita 2015, ilikuwa takribani bilioni 840 hivi, hata hizo zilizopangwa zilipangwa tu kwenye bajeti. Inawezekana utekelezaji wake umetekelezwa kati ya asilimia 60 mpaka asilimia 70. Sasa mnapokuwa na uchache wa rasilimali na mnapokuwa na siasa za mvutano kama tulizonazo Zanzibar, wanasiasa mara nyingi, wanadhani madaraka ya kisiasa ndiyo yanaweza kuamua kila kitu! Kwa maana hiyo, tunadhani sasa mipango yetu ya kupunguza umaskini yote itamalizwa ukiingia Serikalini, kwa maana hiyo, uchaguzi wetu unakuwa mgumu sana kwa sababu, kila mmoja anakimbilia Serikalini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndipo dhima ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano inapotakiwa ianzie. Uchumi mkubwa ni lazima uchukue dhima usaidie uchumi ulio dhaifu. Nimekuwa Waziri Kiongozi kwa takribani miaka 10 na nimebahatika kufanya kazi kwenye Serikali ya Muungano miaka mitatu, tumezungumza kwa muda mrefu suala la kugawana mapato kati ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar. Ndugu zangu wale tunaoipenda Tanzania na tunaoipenda Zanzibar tufikie mwisho, tulimalize suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, amani ya Tanzania inategemea sana mustakabali wa uchumi wa Zanzibar. Tunaweza kusema hapa, umuhimu wa historia, tuwafundishe vijana umuhimu wa historia, lakini vijana wa leo kwa bahati mbaya sana wanaishi na kuona kile kinachofanyika leo! Naomba sana tujitahidi na Bunge hili lazima litoe uongozi kwenye jambo hili, kadri tunavyoendelea kuchelewa kulifanyia kazi jambo hili, tunaongeza watu wasioutakia mema Muungano bila sababu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuwa kwenye Bunge la Katiba tulizungumza jambo hili na tukapendekeza lifanyiwe kazi. Kwa bahati mbaya sana utaratibu na mchakato wa Katiba iliyopendekezwa hatujui lini Katiba ile itapitishwa! Ushauri wangu…
MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.