Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipatia fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye hoja muhimu sana ya bajeti kwa sababu bajeti ni suala la kisera na ndiyo sababu huwa tunakuja kuitungia Sheria ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu kwamba bajeti hii kwa kweli kama ambavyo wamesema ni ya kihistoria, kihistoria kwa maana gani? Wote tunajua kwamba Wabunge ni wawakilishi wa wananchi lakini jambo linalosikitisha wananchi hao wameachwa holela. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa misingi ifuatayo. Nimeona Wabunge wa CCM wakishangilia sana bajeti hii na kubwa wanalozungumzia ni suala la kuondolewa kwa kodi ya barabarani yaani motor vehicle. Hata hivyo, ukiangalia kimsingi motor vehicle ni vyombo vinavyotumia moto lakini leo mwananchi wa kawaida anayetumia mafuta ya taa, kibatari kijijini anatakiwa akatwe shilingi 40 kila anaponunua mafuta. Kuna Mheshimiwa mmoja hapa amezungumza akasema sasa hivi tunataka kuondokana na air pollution kwamba leo wazazi wetu waliotulea kwa vibatari kijijini tunawaona hawafai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme Serikali basi ingeondoa kwanza mafuta ya taa wahakikishe kwamba wananchi wanajengewa nyumba bora na wapinzani tumekuwa tukiongea muda mrefu kwamba vifaa vya ujenzi vipunguzwe ushuru ili wananchi wengi waweze kujenga nyumba bora na nyumba hizo ziweze sasa kuwekewa umeme, ziweze kuwekewa gesi. Leo mwananchi wa kawaida hata nyumba ya tembe anaenda kukatwa kodi. Inaelekea labda wengine tunatoka maeneo mengine tofauti kwamba hatujui wapiga kura wetu ni wa namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Ndassa ambaye najua ni very senior Mbunge humu ndani, anatuambia kwamba Mheshimiwa Shabiby amesema nauli hazitapanda, sasa najiuliza hivi Mheshimiwa Shabiby yeye ndiye mpangaji wa nauli au ni soko huru? Soko ndiyo lina determine kama nauli itapanda au siyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, simple arithmetic, basi lilikuwa linalipa shilingi 300,000 kwa mwaka hiyo motor vehicle leo basi linalotumia lita 400 kutoka let say Mara mpaka Dar es Salaam ina maana lita hizo 400 akiongeza shilingi 40 kwa kila lita atalipa shilingi 16,000. Ina maana kwa mwezi mmoja tu ni shilingi 480,000, kwa mwaka gari linaloenda na kurudi ni zaidi ya shilingi milioni tano. Ndiyo sababu Serikali imeonyesha wazi kwamba watapata faida. Kwa hiyo, hili suala kwamba wenye magari mabovu watayaleta barabarani siyo hoja kwa sababu haiwezekani watu wote wenye magari mimi naamini wana uwezo hatuwezi ku-justify sisi wenye magari kuongeza shilingi 40 kwa kuwatesa wale ambao hawana magari na hawategemei hata siku moja kununua gari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumeambiwa na Mheshimiwa Ndassa sijui kama yupo amesema kwamba tusome

TAARIFA......

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza siipokei na kwamba ananipotezea muda tu. Mimi nazungumzia suala la kupanda sijazungumzia suala la kushuka, kwa hiyo, aendelee na Umakamu wake kama ameshindwa kuweka bajeti yake vizuri atulie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye hoja yangu ya pili, Mheshimiwa Ndassa amezungumza hapa suala la kwamba wapinzani hatusomi vizuri, hatusomi between lines nikategemea anatuletea facts ni mambo gani ambayo ameona katika bajeti yetu hatujazingatia. Nataka kuwaambia tu kwamba pamoja na kwamba Serikali ina wataalam wa kutosha, sisi wapinzani tumegundua kwamba vitabu vyao vyote vina makosa. Pamoja na kuwa na wataalam wengi wenye Ph.D tunaona vitabu Volume I, II, III and IV ukija ku-totalize ni trilioni 23, ukija kwenye matumizi ni trilioni 26.9, ukija kwenye bajeti ya Waziri ni shilingi trilioni 31, sasa tunajiuliza kama mna wataalam wa kutosha kwa nini kuna hizi variance kubwa namna hii?

Kwa hiyo, nadhani Mheshimiwa Waziri utakapokuja utuambie inakuaje mapato na matumizi yanatofautiana lakini vilevile bajeti yako kuu uliyotusomea nayo ina tofauti kubwa ya trilioni tatu, mtuambie hizi ziko wapi, mmezitoa wapi. Kwa hiyo, nadhani mtusifu kwamba sisi wapinzani tumesoma kwa kina, tukachambua kwa kina na tukaja na facts. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la property tax ambalo umelizungumza Mwenyekiti umesema kwamba TRA sasa wanazikusanya, lakini nataka niwaambie, naomba nitoe mfano wa Kinondoni Municipality ambayo mimi natoka. Mwaka 2015/2016 tulikuwa tumepanga kukusanya shilingi bilioni kumi na tukaweza kukusanya shilingi bilioni 7.5. Sasa hivi TRA wametuambia watatuletea shilingi bilioni mbili kwa mwaka huu unaoisha, lakini hawajaleta. Kwa hiyo, suala la own source ni la muhimu sana na tunasema kwamba own source ile five percent ya vijana na wanawake inatakiwa itoke mule sasa kama tunakausha hivi vyanzo vya mapato hawa wanawake na vijana wanapata wapi fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, tunaongelea suala la D by D, kama tunagatua madaraka, tunataka Serikali za Mitaa nazo ziweze kufanya kazi sawasawa na kule ndiko kuna wananchi, leo tunakausha vyanzo vyao tunategemea nini? Nataka nijiulize, nadhani labda Serikali tuelewane, kuna Decentralization by Concentration na Decentralization by Devolution, sasa tunaomba tujue sisi Tanzania ni D by D ipi tunayoitumia? Kwa sababu mimi ninayoiona tunafanya Decentralization by Concentration yaani tumeamua kupeleka mambo yote kule lakini hatupeleki fedha, tunanyang’anya tena kile kidogo ambacho walikuwa wanakipata, maana yake ni nini? Ndiyo sababu tunasema ni kweli hii bajeti ni ya ajabu, ni ya kihistoria sijui ni ya kijiografia nadhani tuongeze pia na ya jiografia siyo kihistoria tu kwa sababu inatisha yaani ni tishio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kumekuwa na hoja ya kujisifia sana kwa suala la standard gauge. Nasema mimi kama Mtanzania ni kweli ningependa sana tuwe na standard gauge nchi nzima lakini naomba nije kwenye mahesabu maana yake twende kwa mahesabu. Hii standard gauge wakati tumefunga mkataba na Wachina ilikuwa watujengee kilometa 2,190 kwa dola za Kimarekani bilioni 7.6. Hii ina maana kila kilometa moja ingekuwa ni sawa na dola za Kimarekani milioni 3.4. Leo mkataba ule haupo, tumeenda kwenye mkataba na Waturuki na Wareno kwamba Wareno hawa na Waturuki ambao wanatujengea hiyo kilometa 205 kwa dola za Kimarekani bilioni 1.2 maana yake ni nini? Maana yake ukigawanya, simple mathematics ni kwamba kila kilometa moja itagharimu dola za Marekani milioni 6. (Makofi)

TAARIFA.....

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa iko kwenye maandishi, labda anazungumzia Serikali ya Awamu ya Tano, lakini nazungumzia Serikali iliwahi, hii taarifa niliyonayo labda nitaileta baadaye lakini natambua kwamba tayari kulikuwa na mkataba huo wa Wachina. Nilichotaka kuzungumza ni kwamba tulikuwa na mkataba zamani sasa hivi tunao huu wa Waturuki, hoja ya msingi, kama ilikuwa ni bilioni 3.4 leo ni bilioni sita maana yake ni kwamba tuna-save au tunapoteza? Hiyo ndiyo ilikuwa hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee, nchi hii ni ya wakulima na wafanyakazi. Nimeangalia Kitabu cha Hali ya Uchumi ni jambo la kusikitisha. Ukiangalia suala la kilimo tumesema kwamba kilimo ndicho ambacho kinaweza kusaidia viwanda lakini leo hii ukisoma kitabu hiki cha Serikali yaani mazao ya biashara karibia yote isipokuwa kahawa na mkonge tu ndivyo ambavyo havijashuka kwa asilimia ya uzalishaji. Sasa kama mazao yetu yameshuka kwa kiwango kikubwa namna hiyo, tunategemea viwanda vyetu vitapata wapi malighafi kwa ajili ya viwanda hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wanasema kabisa bila hata aibu kwamba Tanzania eneo lake la umwagiliaji hatujafikia hata asilimia kumi ya umwagiliaji na wanatoa sababu kwamba kwa nini kilimo kimeshuka, wanasema ni kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi.

Mimi nilikuwa naomba niulize Serikali mabadiliko ya tabianchi yapo siku zote, ukame upo siku zote lakini Tanzania ni nchi ambayo ina vyanzo vikubwa vya maji. Leo nchi ya Misri inategemea maji kutoka katika Ziwa letu Victoria inakuwaje tunashindwa kutumia maji yetu wenyewe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, tuna vyanzo vingi mno vya mito lakini hatuvitumii. Leo kuna mvua kunakuwa na mafuriko kila mahali lakini tunashindwa ku- tap yale maji ili yaweze kusaidia kwenye kilimo chetu halafu tunasema asilimia zaidi ya 80 ya wanawake wa Tanzania ni
wakulima, wanalimaje kama hakuna maji? Halafu hii ni nchi wanasema ni ya viwanda, hivyo viwanda ni vya namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika yote wanatuambia kwenye kilimo wameweza kupeleka asilimia tatu tu ya bajeti halafu tunategemea nini katika nchi hii? Kwa hiyo, kwa kweli bado nasema hii bajeti ni ya kihistoria kwa sababu imeacha kabisa wananchi wake, imeacha kabisa kilimo, imeacha kabisa masuala ambayo yanawagusa wananchi moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la elimu. Ukiangalia kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, mara zote wamesema huu ni wakati wa kuboresha elimu yetu lakini ukiangalia hakuna uboreshaji wa aina yoyote. Huwezi kuwa na elimu bora kama huna ukaguzi. Wenyewe wamekiri katika kitabu hiki, ukurasa wa 260 kwamba katika shule zao hakuna ngazi hata moja wameweza kufikia asilimia 50. Kwa maana hiyo bado elimu yetu itaendelea kuporomoka wakati tunajua kipaumbele cha Tanzania ni elimu na bila elimu bora hatuwezi kufika mahali popote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo nataka kuzungumza ni suala la hosteli za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Sijaona limezungumzwa popote na nataka Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje atuambie, tunataka kujua mabweni yanayoitwa Magufuli Hostel ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam yamejengwa kwa gharama za kiasi gani kwa sababu taarifa alizozitoa Mheshimiwa Waziri wa Elimu alisema ni shilingi milioni 500 kwa jengo la ghorofa nne jambo ambalo mimi binafsi sikubaliani nalo. Nilisema kama ni kweli ni shilingi milioni 500 niko tayari kutoa shilingi milioni tano…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siungi hoja hii mkono.