Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sina budi kuishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka amani na utulivu kwa muda wa miaka 52 hivi sasa Tanzania ipo katika utulivu. Lazima nitoe shukrani kwa Serikali zote mbili kuweza kukaa kwa utulivu na amani na Muungano utaendelea kudumu tena wa Serikali mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi kutoa shukrani za pekee kwa Jemadari Mkuu wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuweza kuweka amani na utulivu kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na tukaweza kurejea uchaguzi kwa amani na utulivu na Wazanzibari chaguo lao likawa CCM wakamchagua Mheshimiwa Ali Mohamed Shein kuwa Rais wa Zanzibar.
Nawaambia Wazanzibari hongereni kwa uchaguzi wenu, haya maneno ya kutupatupa yasiwashtue humu ndani ya Bunge, dua la kuku halimpati mwewe, sasa wanaokaa wakaapiza, wakasema hovyo, wakajilabu hovyo ni sawa na kujishusha tu, lakini hakuna kitakachokuwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwaka 2000 wakati wa Mheshimiwa Salmini walikuwa wanawadanganya wenzi wao hawa uchaguzi utarejewa! Uchaguzi utarejewa! Iko wapi? Tukawaambia hapa Katiba inasema mpaka mwaka 2005, hayakuwa, yamekuwa mwaka 2005! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kazi kuwatia wenzenu drip mkawachoma asubuhi na jioni, wameshachoka kudanganywa! Anasimama mtu anajinasibu eti tutapeleka Mahakamani, hamkwenda Mahakamani hapo mwanzo Mheshimiwa Shein hajakamata nchi, leo mtakwenda Mahakamani nchi imeshakamatwa, siyo mnajidanganya tu? Huko ni kujidanganya, msidanganye wenzenu uchaguzi hapa mpaka mwaka 2020 kama ulivyokuwa nyuma 2000 mpaka 2005 na hii ni mwaka 2015 mpaka na mwaka 2020. Hayo mnayozungumza kama mtakwenda Mahakamani mtakwenda wapi, hiyo danganya toto, ukweli ndiyo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia masuala ya Muungano lakini lazima hawa wenzangu watani wangu niwaambie ukweli waulewe, wasidanganye wenzi wao! Uchaguzi mwaka 2015, msijisumbue tutakwenda Mahakamani! Mwaka huu mtakiona! Kitakuwa nini! Tukione nini na kuna Katiba! Kuna Katiba inazungumza na Jemadari Mkuu namshukuru, Zanzibar imetulia, ndiyo maana mnatuona tuko hapa tunapendeza! Walioweka makoti, walioweka vitenge tumekaa hapa, hakuna anayekwambia anataka kuondoka, miezi mitatu mtatuona humu tunamangamanga na shughuli zetu za Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 51, Kifungu cha 92, Gawio. Nakubaliana na maelezo yote aliyosema Mheshimiwa Waziri, sina matatizo nayo na ile aliyosema 9.9 billion ya gawio sina matatizo nayo, lakini nina ushauri kwamba 4.5 imekaa muda mrefu naona wangekaa tena Serikali hizi mbili wakakokotoa kwamba, hii 4.5 itakwenda mpaka lini? Au ndiyo makubaliano ya Serikali mbili, au ndiyo maamuzi? Naomba hili waliangalie kisha watutolee uamuzi, maana hakuna mtu anayekataa nyongeza na nyongeza huwa inakwenda kwenye fungu! Sasa na hili kama mtalikokotoa mkaliangalia na mkaona hakuna uwezekano wa kutuongezea itakuwa maa-salam, Muungano unazidi kudumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira ya Muungano, ajira ya Muungano kwa maelezo yaliyoelezwa nayakubali sina matatizo. Mgawanyo wa ajira ulivyo sina matatizo, lakini tatizo langu kwa nini Zanzibar hamuweki ofisi ikawa inashughulikia ajira za Muungano? Kama tatizo lilikuwa ni jengo au ofisi, Ofisi ya Makamu wa Rais Zanzibar ni kubwa na ofisi zipo! Mlituahidi mwaka jana kwamba mtachukua ofisi pale! Je, nini tatizo? Kumetokea nini? Au kuna jambo gani hata hadi leo jengo lipo, ofisi haijafunguliwa pale Zanzibar? Mnawafanya akina kaka na akina dada asubuhi kaenda Bara, jioni karudi kufanya interview na siku nyingine asifanikiwe na hela yake imekwenda! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni jengo la Ofisi ya Makamu wa Rais, Zanzibar. Jengo ni zuri lakini linahitaji ukarabati. Ukarabati tulikubaliana mwaka jana, Kamati ya Katiba na Sheria ilivyokwenda iliuona uozo uliokuwepo pale mkasema kwamba, tayari mtalitengeneza. Nimefuatilia halijatengenezwa, mlikwenda mkaligusagusa, lakini mmeliacha liko vile vile na usipoziba ufa utajenga ukuta! Sasa ningewaomba hii kazi na tunataka Makamu wetu wa Rais akae mahali pazuri penye usalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile pale tulikubaliana kwamba sehemu ya nyuma ambapo kuna jengo refu, tukasema Serikali mbili zikae zizungumze ili lile jengo lipate kuondoka au lichukuliwe au mtakavyoamua, lakini tusimpe tabu yule mwenye jengo.
Kutokana na jengo kuweko pale refu, usalama wa Ofisi ya Makamu, usalama wa nyumba anayokaa Makamu haupo, kwa sababu jengo refu, yule akikaa juu anaona wote mle ndani! Sasa usalama uko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hamjatuambia kwenye hiki kitabu mmefikia hatua gani? Kama kweli hii kazi mliifanya na vikao vilikaa, lazima mngeleta mrejesho! Ningeomba na hili kujua kipi kinachoendelea? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na njia ya dharura ambayo kuna njia main road ya kuingilia ambayo ndiyo mnayotokea, lakini tukasema nyuma kuna geti lingine, kujengwe barabara ya dharura ambayo anaweza Mheshimiwa Makamu akaitumia. Tulikubaliana mkasema itakuweko njia ya dharura kwa usalama wa Mheshimiwa Makamu! Hiyo njia hadi leo haijajengwa na sitegemei kama mtaijenga kwa sababu hata kwenye hiki kitabu hamjaelezea! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia nizungumzie vitu ambavyo vitaweza kudumisha Muungano. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliahirisha sherehe za Muungano siyo kwamba kaziahirisha, aliboresha maendeleo akasema zile fedha zipelekwe Mwanza kwa ajili ya maendeleo, sasa kwa ajili zile fedha zilikuwa ni za Muungano na Muungano ni wa nchi mbili, hili gawio ilibidi tulipate na sisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.