Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu pamoja na Wataalam wa Wizara kwa kazi nzuri ikiwa ni pamoja na kuandaa hii bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi ya kusimamia mapato, jukumu la Wizara ya Fedha ni kusimamia udhibiti wa matumizi ya fedha za umma. Matumizi mazuri ya fedha, yanaweza kutekelezeka kama kutakuwepo na utendaji wenye tija kwa kada ya ukaguzi wa ndani pamoja na Kamati za Ukaguzi katika Halmashauri zetu. Imezoeleka kuona Idara ya Ukaguzi wa Ndani kutofanya kazi zake kwa uhuru, kwa muundo tulionao sasa ambapo Mkaguzi wa Ndani anasimamiwa na Mkurugenzi wa Halmashauri. Pia hata Wakuu wa Idara ya Uhasibu imekuwa kawaida kutekeleza kazi zao kinyume na misingi na kanuni za fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya kushangaza imejitokeza katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kwa Mhasibu mwenye sifa na mwaminifu kuondolewa kwenye nafasi yake kwa kuwa alikataa maagizo ya Mkurugenzi kufanya malipo kinyume na kanuni. Huyu Mhasibu mwenye cheti cha juu cha uhasibu (CPA) amehamishiwa kufanya kazi za ukarani kwenye Sekondari ya Kijijini. Pia Idara ya Ukaguzi wa Ndani akiwemo Mkuu wa Idara wapo katika wakati mgumu kwa vile waliandika ripoti iliyoibua ubadhirifu kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ripoti hiyo Baraza la Madiwani lilichukua hatua za kinidhamu kwa wahusika, lakini kwa sasa linapingwa na viongozi kiasi cha kuwagawa Madiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Wizara ya Fedha, kuimarisha Idara ya Ukaguzi wa Ndani ikiwemo idara hii kuwa huru (Independent). Pia Wizara ifanye ukaguzi wa miradi ya maendeleo ambayo kwa kiasi kikubwa kuna upotevu mkubwa wa fedha. Kuwepo na mkakati wa kudhibiti matumizi ya fedha za umma badala ya kusubiri ripoti za Mkaguzi (CAG) ambayo ni postmortem.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Msajili wa Hazina ina umuhimu wa kipekee wa kusimamia Mashirika ya Umma. Mashirika ya Umma ni muhimu na chanzo kikubwa cha mapato yasiyo ya kodi. Lengo kuu la Ofisi ya Msajili wa Hazina ilielekezwa kuboresha utendaji wa Mashirika ili yatoe mchango mkubwa kwenye kuinua uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Msajili wa Hazina ifanye tathmini ya mashirika ambayo hayana tija na kuyatengenezea mkakati wa kuyafufua au kubadilisha malengo kupelekea yawe na tija. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kuna mashamba makubwa yaliyokuwa ya Tanganyika Packers katika Mji Mdogo wa Mbalizi kutokana na Sheria za Mipango Miji mashamba hayo yanakosa sifa za kuwepo Mjini. Kutokana na hali hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imetafuta ardhi kubwa ya zaidi ya ekari 7,000 kuwa mbadala wa haya yaliyokuwa mashamba ya kunenepesha ng’ombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukumbusha Wizara, kukubaliana na ombi la Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ili uwekezaji wa iliyokuwa Tanganyika Packers uhamishiwe kwenye eneo mbadala ambalo ni muafaka kwa mazingira ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za kibenki hazijafika vijijini kama ilivyo mijini. Mabenki karibu yote yanasita kuhudumia wakulima wadogo na wananchi wa vijijini. Huduma za kibenki ni muhimu sana kwa kilimo cha tija ambacho ndiyo mhimili wa uchumi wa Tanzania. Kutokana na changamoto za mtaji wa Benki ya Wakulima (TADB) napendekeza Serikali ielekeze revolving fund ya shilingi milioni 50 kwa kila kiijiji kusimamiwa na TADB. Kwa kuipa TADB jukumu la kusimamia huu mfuko wa milioni 50 kwa kila kijiji utawezesha usimamizi mzuri wa huu mfuko na wakati huo kuiwezesha TADB kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.